Papa Leo XIV: Kristo Yesu Ni Ufunuo wa Baba wa Milele: Someni na Kutafakari Neno la Mungu
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, lilikuwa ni tukio la matumaini ndani ya Kanisa na Ulimwengu katika ujumla wake. Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, wakatambua dhamana, wajibu na changamoto iliyokuwa mbele yao, wakaamua kujadili vipengele mbalimbali na hatimaye, kuvipigia kura. Ni Mtaguso uliowakusanya viongozi kutoka sehemu mbali mbali za dunia, ili kujadili maisha na utume wa Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, chini ya uongozi na usimamizi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro, wakati huo akiwa ni Mtakatifu Yohane XXIII; Ukatafsiriwa kwa vitendo na Mtakatifu Paulo VI pamoja na Mtakatifu Yohane Paulo II. Baba Mtakatifu Benedikto XVI akapyaisha mafundisho yake kwa Katekesi makini kuhusu: Imani, Sakramenti za Kanisa, Maisha Adili na Sala. Hayati Baba Mtakatifu Francisko akaendelea kujipambanua kwa kutaka ushiriki mkamilifu wa watu wa Mungu ili kuchangia katika maisha na utume wa Kanisa la Kristo Yesu, kila mmoja kadiri ya karama, wito na dhamana yake ndani ya Kanisa. Baba Mtakatifu Francisko katika maadhimisho ya Miaka 60 tangu kuzinduliwa kwa Maadhimisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican tarehe 11 Oktoba 1962, katika mahubiri yake, alikazia kuhusu: Upendo ambao Kristo Yesu ameonesha kwa Kanisa lake, licha ya dhambi, udhaifu na mapungufu ya kibinadamu na hata wakati mwingine, kumezwa na malimwengu, changamoto na mwaliko kwa Kanisa kurejea tena katika chemchemi ya upendo ule wa awali ulioneshwa na Kristo Yesu kwa Kanisa lake: Moja, takatifu, katoliki na la mitume. Hili ni Kanisa linalotumwa kutangaza na kushuhudia furaha ya Injili inayomwilishwa katika imani tendaji. Kanisa katika upendo, unyenyekevu na sadaka, linakabidhiwa utume wa kutangaza na kushuhudia Ufalme wa Kristo na wa Mungu; kutangaza Habari Njema ya Wokovu sanjari na utamadunisho, ili kushiriki: furaha na matumaini; uchungu na fadhaa ya walimwengu.
Mkazo ni ushiriki mkamilifu wa ukuhani wa waamini wote unaowawezesha kushiriki sadaka ya Ekaristi Takatifu, kwa kupokea Sakramenti za Kanisa, kwa kusali na kwa njia ya ushuhuda wa maisha matakatifu, toba, wongofu wa ndani, kwa kujikana na kwa upendo wenye utendaji; Umoja wa watu wa Mungu ukipewa kipaumbele cha kwanza. Kanisa litambue kwamba, maskini wanao upendeleo wa pekee mbele ya Mwenyezi Mungu. Kwa hakika Kanisa ni Sakramenti ya umoja inayowaunganisha watu kiundani na Mwenyezi Mungu na hivyo kuleta umoja kati ya wanadamu wote. Ni jukumu la Mama Kanisa kuendelea kujikita katika Mapokeo, sera na mikakati ya shughuli za kiuchungaji. Mwaliko wa kuendeleza majadiliano ya kidini, kiekumene na kitamaduni. Huu pia ni ni mwaliko wa kujenga na kudumisha ushirika wa Kanisa, ili wote wawe na umoja kama Kristo Yesu alivyojisadaka kwa ajili ya kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti. Baba Mtakatifu Leo XIV anasema baada ya Maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 2025 ya Ukristo, kuanzia Jumatano tarehe 7 Januari 2026 anaanzisha mzunguko mpya wa Katekesi unaojikita katika Maadhimisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na Usomaji Mpya wa Nyaraka zake, ili kugundua tena uzuri na umuhimu wa tukio hili la Kikanisa, Kipindi cha neema ambacho kwa hakika, Mama Kanisa amekifaidi sana katika Karne ya ishirini. Kumbe, hiki ni kipindi cha Kanisa kujikita zaidi katika Nyaraka Kuu 4 za Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican yaani: “Dei verbum” yaani “Ufunuo wa Kimungu”, “Sacrosanctum concilium” yaani “Juu ya Liturujia”; “Lumen gentium” yaani “Fumbo la Kanisa” pamoja na “Gaudium et spes” yaani “Kanisa katika ulimwengu mamboleo.”
Katekesi hii imenogeshwa na sehemu ya Maandiko Matakatifu: “Wakumbukeni wale waliokuwa wakiwaongoza, waliowaambia Neno la Mungu; tena, kwa kuuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, iigeni imani yao. Yesu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele. Msichukuliwe na mafundisho ya namna nyingine nyingine, na ya kigeni.” Ebr 13: 7-9.Hati ya Kusikiliza kwa Uchaji Ufunuo wa Neno la Mungu “Dei verbum” inagusia kwa undani kuhusu: Ufunuo wenyewe; Urithishaji wa Ufunuo wa Kimungu; Uvuvio wa Kimungu na Ufafanuzi wa Maandiko Matakatifu; Agano la Kale, Agano Jipya; pamoja na Maandiko Matakatifu Katika Maisha ya Kanisa. Baba Mtakatifu Leo XIV anasema, Mwenyezi Mungu kwa njia ya Kristo Yesu, Ufunuo wa Baba wa milele, anazungumza na wanadamu kama mtu anavyo zungumza na rafiki yake. Huu ni mwaliko kwa waamini kujenga na kudumisha utamaduni wa kusoma, kulitafakari na hatimaye, kulimwilisha Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha yao pamoja na kujikita katika maisha ya sala!
Katekesi ya Baba Mtakatifu Leo XIV “Hati ya Kusikiliza kwa Uchaji Ufunuo wa Neno la Mungu “Dei verbum”, Jumatano tarehe 21 Januari 2026 imenogeshwa na sehemu ya Maandiko Matakatifu kuhusu Kristo Yesu Ufunuo wa Baba wa Milele: “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. Kama mngalinijua mimi, mngalimjua na Baba; tangu sasa mnamjua, tena mmemwona. Filipo akamwambia, Bwana, utuoneshe Baba, yatutosha.” Yn 14:6-8. Kwa hakika Mwenyezi Mungu anajifunua kwa njia ya majadiliano na Agano linalofumbatwa katika maisha, mwaliko wa kujenga na kudumisha mahusiano na Kristo Yesu, Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, katika Roho Mtakatifu; katika ufunuo wa upendo huo, Mungu anaongea na binadamu kama na marafiki; katika historia ya wokovu na katika maneno yanayotangaza kazi na kuliangaza fumbo lililomo ndani yake. Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican wanasema, “kwa njia ya ufunuo huo, ukweli kamili juu ya Mungu na juu ya wokovu wa wanadamu unang’ara kwetu katika Kristo Yesu, ambaye Yeye mwenyewe ndiye mshenga na utimilifu wa ufunuo wote.” DV 2. Kristo Yesu ametumwa na Baba na kwa njia yake, wanadamu wanaweza kushiriki katika Fumbo la Utatu Mtakatifu, ili kuweza kulifahamu fika kuna haja ya kujenga mahusiano na Kristo Yesu pamoja na Roho Mtakatifu kama anavyosimulia Mwinjili Luka kuona furaha ya Kristo Yesu kwa jinsi amnavyo Injili hufunuliwa kwa watoto wachanga katika Baba na Mwana. “Saa ile ile alishangilia katika Roho Mtakatifu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya umewaficha wenye hekima na akili; umewafunulia watoto wachanga; Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyokupendeza. Akasema, Nimekabidhiwa vyote na Baba yangu, wala hakuna amjuaye Mwana ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba ila Mwana, na ye yote ambaye Mwana apenda kumfunulia.” Lk 10:21-22.
Kristo Yesu anakamilisha ufunuo wa Baba yake wa milele. Maana alimtuma Mwanawe, yaani Neno wa Milele, anayewaangazia watu wote, ili akae kati ya wanadamu na kuwafunulia siri za Mungu. Rej. DV, 4. Na Baba yako aonaye sirini atakujazi na kwamba, Baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba. Rej Mt 6; 4.6.8; 62; 32. Baba Mtakatifu Leo XIV anasema kwa njia ya Kristo Yesu, mwamini anaweza kuufahamu ukweli kuhusu Mungu Baba na wao wenyewe kujifahamu kuwa waana katika Mwana. “Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana. Na kwa kuwa ninyi mmekuwa wana, Mungu alimtuma Roho wa Mwanawe mioyoni mwetu, aliaye, Aba, yaani, Baba. Kama ni hivyo, wewe si mtumwa tena bali u mwana; na kama u mwana, basi, u mrithi kwa Mungu.” Gal 4: 4-6. Baba Mtakatifu Leo XIV anasema, Mwenyezi Mungu amejifunua kwa njia ya Kristo Yesu kwa kutumia mwili wake. Kwa kumwona Kristo Yesu, watu wanamwona pia Baba aliyemtuma. Rej Yn 14:9. Kwa uwepo na ushuhuda wake; kwa maneno na kazi zake, kwa alama na miujiza aliyotenda lakini zaidi ni kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wake mtukufu kutoka kwa wafu na hatimaye, kwa kumtuma Roho wa kweli. Rej DV, 4. Ili kuweza kumfahamu Mungu katika Kristo Yesu, kuna haja kwa waamini kuupokea ubinadamu wake katika ukamilifu wote kwani “Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wo wote; Mungu Mwana pekee aliye katika kifua cha Baba, huyu ndiye aliyemfunua.” Yn 1:18.
Kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko wake, Kristo Yesu katika ubinadamu wake wote: Katika Fumbo la Umwilisho, anazaliwa, anatunza, anafundisha, anateseka, anakufa na kufufuka kwa wafu, bado anaendelea kubaki kati pamoja na waja wake, changamoto na mwaliko kwa waamini kulitukuza Fumbo kuu la Umwilisho ambalo si tu kwamba, limekuwa ni njia ya kutangaza kweli za kiakili. Kristo Yesu anawaalika waja wake kushiriki kikamilifu katika kuangalia kweli, fadhaa na wasi wasi za maisha akisema: “Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao.” Mt 6:26. Baba Mtakatifu Leo XIV anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kufuata kikamilifu njia ya Kristo Yesu, watu wanaweza kugundua kwamba, hakuna kitu chochote kinachoweza kuwatenga na upendo wa Mungu kama anavyosema Mtakatifu Paulo, Mtume na Mwalimu wa Mataifa katika utenzi wake kuhusu upendo wa Mungu; “Basi, tuseme nini juu ya hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu? Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye? Rum 8:31-32. Ni kwa njia ya Kristo Yesu, Mkristo anamfahamu Mungu Baba Mwenyezi na hivyo kujiachilia mikononi mwake kwa imani.
