Congo,DR zaidi ya watu 200 wamekufa kutokana na maporomoko ya Rubaya
Vatican News
Zaidi ya watu 200 walifariki kufuatia maporomoko makubwa ya ardhi katika eneo la uchimbaji madini la Rubaya Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo. Vyanzo vya serikali mjini Kinshasa vilithibitisha habari hiyo, vikibainisha kuwa mgodi huo, unaochukua kilomita za mraba kadhaa na unadhibitiwa na wanamgambo kutoka kundi la waasi la M23, uko katika eneo la Masisi, yapata kilomita 70 magharibi mwa Goma, mji mkuu wa Mkoa wenye matatizo huko Kivu Kaskazini.
Idadi ya vifo inawezekana kuwa kubwa zaidi
Hata hivyo, inahofiwa kwamba idadi ya watu waliofariki kutokana na maafa hayo inaweza kuwa kubwa zaidi. Watu wengi bado hawajulikani walipo. Miongoni mwa waathiriwa waliothibitishwa ni takriban watoto sabini. Watu wengi waliojeruhiwa, baadhi wakiwa katika hali mbaya, wamehamishiwa kwenye vituo vya matibabu huko Goma, kulingana na vyanzo kutoka Wizara ya Madini ya Congo. Eneo hilo linalosimamiwa na Kampuni ya Madini ya Bisunzu(Société Minière de Bisunzu), inajulikana kwa uchimbaji madini wa kienyeji, mazingira hatarishi ya kazi, na majanga ya asili ya hivi karibuni, kama vile maporomoko ya ardhi yaliyosababisha vifo vya watu wengine 220 mwezi Januari uliopita.
Mji wa madini wa Rubaya, ambao hutoa kati ya 15% na 30% ya uzalishaji wa koltani duniani, unaochimbwa kwa mikono na wenyeji ambao hupata pesa kidogo kila siku, ulianguka chini ya udhibiti wa M23 mnamo Aprili 2024. Madini haya, ya kimkakati hasa kwa tasnia ya vifaa vya elektroniki, yanapatikana sana katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, ambayo inakadiriwa kuwa na angalau 60% ya akiba ya koltani duniani. Coltan pia hutumika kutengeneza tantalum, chuma kinachostahimili joto kinachotumika kutengeneza vipengele vya anga za juu, kompyuta, simu za mkononi, na turbini za gesi.
Maeneo ya vita
Katika jaribio la kutwaa tena eneo la madini kutoka kwa waasi, Kinshasa ilianzisha mashambulizi makubwa katikati ya Februari ikiongozwa na wanamgambo wa Wazalando wanaounga mkono serikali. Mfululizo wa mashambulizi ulianzishwa katika eneo la Masisi, kuelekea migodi ya Rubaya. Baada ya kushinda miji ya Kasenyi, Chugi, na Kinigi, vyanzo kadhaa vya ndani vilithibitisha kusonga mbele kwa Wazalando kuelekea vijiji vya Runigi, Kabara, Kiruli, na Kanyalu, takriban kilomita 10 kutoka eneo la mgodi. Hata hivyo, mashambulizi ya kijeshi yamesababisha watu kuhama katika maeneo yaliyoathiriwa. Kwa kuogopa kukamatwa katika mapigano hayo, familia nyingi zimeacha nyumba zao, zikielekea Ngungu, Bihambwe, na Mushaki, au kuvuka mpaka na kuingia mkoa jirani wa Kivu Kusini. Wengi wa waliohama walikimbia bila kuweza kuchukua mahitaji muhimu ya maisha.
Asante kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here