Mahubiri ya Papa Benedikto XVI ambayo hayakuchapishwa yanatolewa kwa Kiingereza
Vatican News
Toleo jipya la Kiingereza la "Bwana Anatushika Mkono" linawapatia wasomaji mkusanyiko wa mahubiri ambayo hayajachapishwa ya Papa Benedikto XVI, na kuwaruhusu kusikia tena sauti ya Joseph Ratzinger kama mhubiri, mtaalimungu, na mchungaji. Kitabu hicho kilichochapishwa awali kwa Kiitaliano na Nyumba ya Uchapishaji ya Vatican chini ya kichwa "Il Signore ci tiene per mano," kinakusanya mahubiri yaliyotolewa kati ya 2005 na 2017 wakati wa vipindi vya kiliturujia vya Majilio, Kwaresima, na Pasaka. Kimehaririwa na(LEV), Riccardo Bollati, Luca Caruso, na Padre Federico Lombardi, SJ, kitabu hiki kinajumuisha utangulizi wa Askofu Mkuu Georg Gänswein, katibu wa zamani wa Papa Benedikto XVI, na utangulizi wa Padre Lombardi, Rais wa Mfuko wa Vatican wa Joseph Ratzinger-Benedikto XVI.
Misa za Kibinafsi, mashuhuda
Mahuburi haya yalitolewa wakati wa Misa "za faragha" zilizoadhimishwa na Papa Benedikto XVI pamoja na wahusika wa Nyumba ya kipapa na wageni wa mara kwa mara, mahubiri yote ni ya wakati alipokuwa Papa na baadaye kama Papa Mstaafu. Baadhi yalihubiriwa katika Kikanisa cha Jumba la Kitume, na mahubiri mengine yalitolewa katika Monasteri ya Mater Ecclesiae huko Vatican, ambako Papa Benedikto XVI aliishi baada ya kujiuzulu kutoka upapa. Ingawa yanazungumzwa katika mipangilio ya faragha, matini hufungua dirisha kwa kina na usahili wa mahubiri ya Papa Benedikto XVI. Yanafunua uwezo wake wa kusoma Maandiko Matakatifu kwa njia mpya kabisa, yakitoa nuru kutoka katika imani, sala, na maisha ya Kikristo ya kila siku.
Kristo katikati
Kurasa za kitabu pia zinaonesha jinsi ambavyo Joseph Ratzinger alivyoweka katikati ya imani yake si hoja za kufikirika au kavu, bali uhusiano wa kibinafsi na Kristo. Katika mahubiri, Papa Benedikto XVI anarudi tena na tena kwenye fumbo la Bwana anayewasindikiza watu wake, anawategemeza, na kuwashika mkono. Kichwa chenyewe kinaelezea hisia hiyo kuu: maisha ya Kikristo si njia ya pekee, bali ni safari inayoongozwa na uwepo na huruma ya Mungu. Mkusanyiko pia unaakisi mwendelezo kati ya kazi ya kitaalimungu ya Papa Benedikto na huduma yake ya kichungaji. Tafakari zake zinaashiriwa na uwazi, kina cha kiroho, na mwelekeo unaozingatia Kristo ambao ulibainisha upapa wake.
Mpango mpana zaidi
“Bwana Anatushika Mkono” ni kitabu cha kwanza cha mahubiri ya Papa Benedikto XVI ambacho hakijachapishwa. Kitabu cha pili, kilichojitolea wa ajili ya mahubiri kutoka Wakati wa Kawaida, kinatarajiwa kufuata. Toleo la Kiitaliano liliwasilishwa mnamo Mei 17 katika Maonesho ya Vitabu ya Kimataifa huko Torino nchini Italia wakati wa mkutano ulioitwa “Benedikto XVI: ‘Kristo ni wakati ujao!’ Mahubiri ambayo hayajachapishwa.” Wazungumzaji walijumuisha Padre Lombardi na mwimbaji-mtunzi wa nyimbo za kiitaliano, Giovanni Lindo Ferretti, huku majadiliano yakiongozwa na Andrea Tornielli, Mkurugenzi wa Uhariri wa Baraza la Mawasiliano. Kwa kuchapishwa kwa toleo la Kiingereza, maandishi haya ambayo hayajachapishwa hapo awali sasa yanapatikana kwa wasomaji wengi zaidi, yakitoa mkutano mpya na mahubiri ya Papa Benedikto XVI na mwaliko wake wa maisha yote wa kumweka Kristo katikati ya imani na historia.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here.