Mchango wa kuhamasisha amani katika ngazi za kikanda na mahalia!
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Mfuko wa Kipapa ulitangaza kuidhinisha zaidi ya dola milioni 15 kwa mwaka 2026, kwa kusaidia kuweka rekodi zaidi ya mipango 144 katika nchi 75. Ufadhili huo utaendeleza miundombinu muhimu, programu na misaada ya kibinadamu iliyotambuliwa na Vatican, ikihudumia jumuiya zenye uhitaji mkubwa ulimwenguni kote. Mzunguko wa fedha wa mwaka huu unawakilisha ufikiaji usio wa kawaida wa kimataifa na kilele kipya katika historia ya miaka 38 ya Mfuko huo, uliojitolea kuhudumia vipaumbele vya Baba Mtakatifu duniani kote. Alisema hayo Bwana David Savage, Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Kipapa.
Kusaidia Kanisa la Kimataifa na wale walio na mahitaji zaidi
Fedha za mwaka 2026 zitafadhili mipango mbalimbali kwa maskini wa Kanisa, ikiwa ni pamoja na ujenzi na ukarabati wa shule za Kikatoliki, madarasa, monasteri, na vituo vya watoto yatima na kliniki za matibabu katika nchi nyingi; mabweni ya kuwaokoa wasichana kutokana na ndoa za mapema, biashara haramu na unyanyasaji wa kijinsia, na wavulana wanaoacha shule nchini Tanzania; shule salama kwa watoto wa kikabila waliotengwa nchini India; kituo cha maktaba na teknolojia katika Jamhuri ya Afrika ya Kati; mafunzo ya kitaalamu ya TEHAMA kwa wanawake walio katika mazingira magumu nchini Ufilipino; na kisima na mnara wa maji katika Jamhuri ya Guinea.
"Kuunga mkono msaada wa fedha hizi zinazobadilisha maisha ndio msingi wa dhamira ya Mfuko wa Kipapa. Matokeo tunayo kwa maskini na walio katika mazingira magumu zaidi ni zawadi ya shirika kwa Kanisa na zawadi ya Kanisa Katoliki kwa watu wake kote ulimwenguni," alisema Ward Fitzgerald, Rais wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Kipapa. "Fedha za mwaka huu ni ushuhuda wenye nguvu wa kile kinachoweza kufikiwa kupitia usimamizi mwaminifu na utume wa pamoja. Kila mpango unawakilisha matumaini, kukidhi mahitaji ya dharura na kuimarisha azimio la jumuiya ya Kanisa Katoliki katika mataifa yanayoendelea."
Mchakato mkali wa mapitio
Mchango huu wa 2026 ni matokeo ya mchakato kamili wa tathmini unaoongozwa na Kamati ya Mfuko huo wa Kipapa unaoongozwa na mdhamini Dk. Tammy Tenaglia wa Jimbo Kuu la Philadelphia, Marekani. Kamati ilipitia maombi yaliyowasilishwa na Vatican katika kipindi cha vuli 2025 na, kwa usaidizi mkubwa kutoka katika Kamati ya Mfuko wa Utume kwa kupendekeza mipango 144 kwa ajili ya kuidhinishwa. Kwa ujumla, Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Kipapa iliidhinisha mgao wa zaidi ya dola milioni 15, ikiwa ni pamoja na dola milioni 12,502,765 katika fedha za sasa na dola milioni 3 za ziada zitakazosambazwa kupitia Mfuko huo na washirika wake kabla ya mwisho wa 2026.
Ukuaji unaoendelea katika usimamizi na ushirikiano
Jumuiya inayopanuka ya Wasimamizi wa Mtakatifu Petro katika Mfuko huo inaendelea kuchochea matokeo yake yanayoongezeka. Kuongezeka kwa familia 25 mpya tangu kuchaguliwa kwa Papa Leo XIV kunaashiria kasi kubwa na kuongezeka kwa ushiriki miongoni mwa Wakatoliki waliojitolea kuunga mkono dhamira ya Baba Mtakatifu ya kuwahudumia maskini. Hija ya kila mwaka ya wanachama wa Mfuko huo jijini Roma na Vatican iliwaleta pamoja familia 56 za Wasimamizi, ikiwa ni hija ya kwanza tangu kuchaguliwa kwa Baba Mtakatifu, Papa Leo XIV, na ya pili kuongozwa na Mwenyekiti wa Mfuko wa Kipapa, Kardinali Timothy Dolan, Askofu Mkuu Mstaafu wa New York.
Safari hiyo ilijumuisha ziara katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro, Kanisa Kuu la Mtakatifu Yohane na Jumba la Lateran, Angelicum, Rozari kwa kuwasha mishumaa katika Basilika ya Mtakatifu Maria Mkuu, na Mkutano na Baba Mtakatifu, ambapo Wasimamizi walishirikisha furaha na shukrani zao kwa uongozi wake wa Kanisa letu.
"Ukuaji tunauona na unatia moyo sana, kwani unaonesha kujitolea kwa pamoja kutumikia, kutoa, na kufanikisha utume wa Kanisa kwa njia zenye maana kote ulimwenguni,"aliongeza kusema David Savage, Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Kipapa.
Urithi wa Imani katika Vitendo
Papa Leo XIV kadhalika alisema kuwa: “Tangu kuanzishwa kwake, Mfuko wa Kipapa umesambaza zaidi ya dola milioni 270 kama mfano wa ufadhili wa masomo, namisaada ya kibinadamu kwa zaidi ya mipango 2700 iliyochaguliwa na Papa Leo XIV, Papa Francisko, Papa Benedikto XVI, na Mtakatifu Yohane Paulo II. Kwa maelezo zaidi kuhusu Mfuko huo wa Kipapa unaweza kutembelea:https://www.thepapalfoundation.org/
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here