Kard.Parolin:Balozi wa Kitume mjenzi wa madaraja na mpatanishi
Isabella Piro na Angella Rwezaula - Vatican.
Katika siku ya kuwekwa wakfu kwa Askofu Mkuu Relwendé Kisito Ouédraogo, Balozi Mpya wa Vatican katika Jamhuri ya Congo na Gabon, iliyofanyika Jumamosi asubuhi tarehe 7 Machi 2026 katika Kanisa Kuu Ndogo la Mama Yesu wa Yagma, nchini Burkina Faso, nchi ya asili ya Askofu huyo Mkuu, Kardinali Pietro Parolin, Katibu Mkuu wa Vatican alitoa shukrani zake, na kumsifu kwa uaminifu na kumtia moyo. Alibainisha hayo akiongoza Ibada ya Misa Tafakari kwa ajili ya tukio hilo la kuwekwa wakfu na ambaye alihudumu kwa muda mrefu kama Katibu binafsi wa Kardinali Parolini.
Ilikuwa mnamo Januari 2010, Askofu Mkuu Mpya Kisito alianza huduma yake katika Kitengo cha Masuala ya Jumla ya Sekretarieti ya Vatican, ambapo alibaki hadi tarehe 28 Januari 2026, wakati Baba Mtakatifu Leo XIV alipomteua kuwa Balozi wa Vatican huko nchini Congo Brazzaville, akimpandisha hadhi ya kuwa na kiti cha Ilta, na hadhi ya Askofu mkuu. Na wakati huo huo, Baba Mtakatifu mnamo tarehe 10 Februari 2026 aliteuliwa tena kuwa mwakilishi wa Papa huko Libreville - Gabon.
Miaka yake mingi ya utumishi katika Sekretarieti ya Vatican
Kwa kufunguliwa na salamu kutoka kwa Askofu Mkuu Prospet Kontiebo, Askofu Mkuu wa Ouagadougou, ambaye eneo lake linajumuisha hata Madhabahu ya Mama Yetu wa Yagma, Misa hiyo iliudhuriwa na Maaskofu na Mapadre kutoka Burkina Faso, Jamhuri ya Congo, na Gabon pamoja na waamini wengi kwa sherehe nzuri ya misa huku ikihuishwa na nyimbo na ngoma za kiutamaduni.
Katika mahubiri yake, Kardinali Parolin alikumbusha kwa furaha ya kukaa kwa muda mrefu na Askofu Mkuu mpya Ouédraogo jijini Roma: "Tuliweza kushiriki kazi, kila wakati ikiwa nzito sana," alibainisha, "matatizo yanayotokana nayo, lakini pia furaha na kuridhika kwa kuwa washirika katika huduma ya Papa kwa wote." Lakini miaka hii mirefu, aliongeza, ilitumika kumwandaa mwakilishi wa Papa "kwa ajili ya utume mpya ambao Bwana, kupitia Papa, amemtuma." Kwa hivyo, sasa, Askofu Mkuu "anarudi bara la Afrika alikotoka," Katibu wa Vatican aliendelea, "bara ambalo amekuwa akifungamana nalo kila wakati na ambalo ameliwakilisha vyema Roma.
Kauli mbiu ya kiaskofu inaongozwa na maneno ya Bikira Maria
Kardinali Parolin aidha katika mahubiri yake alimshukuru sana Askofu Mkuu Ouédraogo, "kwa msaada na ushirikiano wote" uliotolewa sio bila sadaka." Wakati huo huo, alimhimiza "kukabiliana na kazi hii mpya na isiyotarajiwa kwa utulivu na ujasiri mkubwa," kwa maneno yale yale yaliyo katika kauli mbiu ya kiaskofu iliyochaguliwa: "Fanyeni chochote atakachowaambia" (Yh 2:5). Maneno haya, yaliyosemwa na Bikira Maria kwenye karamu ya harusi ya Kana, yatakuwa msukumo kwa safari ya baadaye ya Askofu Mkuu Ouédraogo, Kardinali Parolin alielezea. "Hakika, kutakuwa na wakati mgumu, aliongeza; hata hivyo, kutafuta kufanya mapenzi ya Mungu kila wakati tu, ndiko kunatia moyo, utulivu na amani moyoni."
Kupeleka Amani,Umoja na Ukweli katikati ya migawanyiko na manabii wa uongo
Katibu Mkuu wa Vatican aliendelea kusema, dhamira ya Balozi wa Kitume kwamba ni "kupeleka ukweli na nuru, amani na umoja, katikati ya giza la dhambi, mgawanyiko, na uongo."Hakuna uhaba wa "manabii wa uongo" ambao, "wakiongozwa na kiburi tu, huchangia kugawanya au kupotosha kundi la Yesu Kristo kwa mafundisho ya uongo." Kwa hivyo, himizo la kuwa "mhubiri wa ukweli, mchungaji kulingana na moyo wa Yesu," tayari kutoa maisha yake, kama Kristo, kwa ajili ya kundi lake, alisititiza Kardinali Parolin.
Kutangaza Injili bila kuchoka
Kardinali Parolin kisha alilenga neno "nuncio," ambalo linachukua maana ya utume. "Nuntius," "Tangazo "alielezea, "ndiye mtoa neno la mwingine: lile la Kristo, kuhusu huduma ya Askofu, na lile la Baba Mtakatifu, kuhusu utume wa kidiplomasia." Kwa hivyo, alimwalika Askofu Mkuu Ouédraogo kutangaza Injili "kwa uaminifu na bila kuchoka" kwa wote, akiishi "katika maisha ya kila siku," faragha na katika mikutano rasmi.
Daima kujenga madaraja na mahusiano
Akiwa ametumwa "kuponya na kuwafariji," Askofu lazima aoneshe "upendo wa huruma ya Mungu kwa wanadamu wote" na, "katika utekelezaji wa utume wake wa kidiplomasia," lazima apeleke "maneno ya uponyaji na faraja kwa niaba ya Baba Mtakatifu, hivyo kuonesha wasiwasi wake kwa wote ili kila mtu ajue kwamba Kanisa liko tayari kufanya chochote kwa ajili ya upendo." Zaidi ya hayo, akiwa ametumwa kwa kazi ya "kutunza umoja," Askofu Mkuu Ouédraogo kamwe hatakuwa peke yake, kwa sababu atatenda "sub umbra Petri" "chini ya Kivuli cha Petro kila wakati, yaani, katika ushirika na Papa, mrithi wa Petro. Na kwa kuwa "mhamasishaji wa udugu miongoni mwa watu," Askofu mkuu mpya lazima ajitahidi kila wakati kujenga "uhusiano na madaraja, hata pale ambapo ni vigumu zaidi."
Maombi yasiyokoma na utendaji wa upendo
Mahubiri ya Katibu Mkuu wa Vatican alisisitiza wito wa sala ili mjumbe aweze "kumwomba Mungu bila kuchoka na kumtolea sadaka ya watu, na kuwa mjumbe wa kundi kwa Baba." Kwa maana hiyo, "Askofu Mkuu Kisito lazima awatazame waamini ili imani yao ikue, uaminifu wao uimarike, na upendo wao kwa Mungu usitawi." Wakati huo huo, akijifanya kuwa mfano wa Mchungaji Mwema ambaye hawasahau wale waliopotea, Balozi mpya lazima awe tayari kila wakati kuonesha upendo wa Kristo kwa wanadamu. Hatimaye, Kardinali Parolin alimkabidhi Askofu Mkuu mpya kwa Bikira Maria na kwa mashahidi watakatifu wa Uganda, mmoja wao, mdogo zaidi, aliyekufa akiwa na umri wa miaka 14 tu, ndiye alipewa jina la Askofu Mkuu Ouédraogo.
Asante kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here