Poland:Vyombo vya Habari vya Vatican vyaheshimiwa kwa kukuza amani
Karol Darmoros – Warsaw, na Angella Rwezaula – Vatican.
Tuzo ya Benemerenti yaani ya sifa bora, iliwasilishwa kwa Idhaa ya Kipoland ya Radio Vatican–Vatican News na Osservatore Romano “kwa kukuza maadili ya amani na usalama.” Hafla ya tuzo hiyo ilifanyika tarehe 21 Januari 2026 katika Jumba la Makumbusho la Kijeshi la Poland jijini Warsaw, wakati wa hafla ya kuadhimisha miaka 35 ya kurejeshwa kwa Ofisi ya Kijeshi ya Kawaida. Mapambo ya tuzo yaliwasilishwa na Askofu Wiesław Lechowicz, ambaye alielezea kuridhika kwake hasa na uwepo wa wawakilishi wa vyombo vya habari vya Vatican, akielezea kwamba "uthibitisho wa vyombo vya habari vinatumikia amani na usalama." Aliongeza kuwa "Baraza la Kipapa la Mawasiliano linabeba sauti ya Papa na ya Kanisa, likimtumikia Yesu, ambaye ni Mfalme wa Amani".
Askofu aliwashukuru waandishi wote wa habari wa Vatican, akibainisha kuwa "katika Ulimwengu wa leo, uliojaa migogoro mingi na ambapo maadili kama vile ukweli, upendo, amani, haki, na mshikamano hayathaminiwi kila wakati, vyombo vya habari vya Vatican vinaendelea kukuza na kushuhudia maadili haya."
Mawasiliano katika huduma ya amani
Akizungumza kwa Kipoland, Dk. Andrea Tornielli, Mkurugenzi Mkuu wa Uhariri wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano alisisitiza: "Dhamira yetu ni kuendelea kuipeleka sauti ya Mrithi wa Petro kila kona ya dunia. Timu ya uhariri ya lugha ya Kipolandi imekuwa mfano, na kwa mfumo wetu mzima wa vyombo vya habari, na Kipoland kinasalia kuwa mojawapo ya lugha saba kuu ambazo vyombo vya habari vya Vatican vinaendelea kuwasiliana, miaka 21 baada ya kifo cha Mtakatifu Yohane Paulo II," alisisitiza.
Dk. Tornielli aliakisi utamaduni mrefu wa Radio Vatican, mchango wa Kijesuit katika maendeleo yake, na kazi iliyofuata ya timu iliyoongozwa na Padre Paweł Rytel-Andrianik. Alisisitiza kwamba uwasilishaji wa taarifa za kweli, ujenzi wa mahusiano, na mawasiliano yenye uwajibikaji ni miongoni mwa kazi za msingi za vyombo vya habari vya Kikatoliki. Pia alisisitiza jukumu muhimu linalotrndwa na Idhaa ya Kipoland katika utume huu, kufikia hadhira pana nchini Poland na nje ya nchi. Katika mwaka uliopita pekee(2025), vipindi vilivyotolewa kwa Kipoland na vyombo vya habari vya Vatican vilirekodi na kusikilizwa kwa takriban watazamaji bilioni moja.
Umuhimu wa lugha ya Kipoland
Massimiliano Menichetti, Naibu Mkurugenzi wa Uhariri wa Vyombi vya habari vya Vatican na mkuu wa Idhaa ya Radio Vatican–Vatican News, alielekeza umakini kwenye nafasi maalum ya lugha ya Kipoland katika historia na Utume wake wa sasa wa vyombo vya habari vya Vatican kwa ujumla. "Lugha ya Kipoland imekuwa na jukumu kuu ndani ya vyombo vya habari vya Vatican. Ilihifadhi imani wakati wa miaka ya giza ya utawala wa kidikteta na leo hii, kupitia Radio Vatican, Vatican News, na Osservatore Romano, inatangaza uzuri wa Injili na kutafsiri kila habari kupitia lenzi ya mafundisho ya kijamii ya Kanisa," alisema.
Menichetti aliongeza kuwa katika ulimwengu unaojaa vurugu na ukosefu wa haki, vyombo vya habari vya Vatican vinatoa "upeo wa matumaini" na, kama Papa Francisko alivyokumbusha mara nyingi, vinakuza " aina ya mawasiliano isiyo na silaha na inayoondoa silaha.” Tuzo hiyo ilipokelewa kwa pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Uhariri Dk Andrea Tornielli, naibu wake Massimiliano Menichetti, na Padra Paweł Rytel-Andrianik, mkuu Idhaa ya Kipolandi. Zaidi ya hayo, wakurugenzi wa vyombo vya habari vya Vatican na wafanyakazi wa Idhaa ya Kipoland pia walitunukiwa medali za Milito Pro Christo kwa kujitolea kwao kukuza amani.
Heshima za ziada
Tuzo za Benemerenti za mwaka huu 2026 kutoka kwa Jeshi la Kawaida pia zilitolewa kwa majenerali wakuu na taasisi muhimu za Jeshi la Poland, ikiwa ni pamoja na Amiri Mkuu wa Uendeshaji ya Vikosi vya Kijeshi, Mkaguzi wa Usaidizi wa Vikosi vya Jeshi, na Bendi ya Mwakilishi wa Karol Kurpiński wa Jeshi la Anga. Ofisi ya Kijeshi ya Poland ilianzishwa mwaka 1919 na imekuwa na jukumu muhimu, hasa wakati wa Vita vya Pili vya Dunia. Wakati wa kipindi cha ukomunisti, mamlaka za serikali zilisimamisha huduma ya kichungaji kwa wanajeshi. Miaka thelathini na tano iliyopita, Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili alirejesha Jeshi la Kawaida. Hivi sasa, zaidi ya mapadre 130 wa kijeshi wanahudumu ndani ya miundo yake.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here