Tafuta

Juma la Kuombea Umoja wa Kikristo 18-25 Januari 2026. Juma la Kuombea Umoja wa Kikristo 18-25 Januari 2026.  (@Vatican Media)

Juma la Kuombea Umoja wa Kikristo 2026:"Kuna Mwili Mmoja na Roho Moja"

Ratiba ya matukio yaliyoandaliwa na Jimbo Kuu la Roma kunzia Januari 18-25,yanajumuisha Masifu ya Jioni na Papa Leo XIV katika Basilika ya Mtakatifu Paulo Nje ya Ukuta.Alhamisi Januari 22,Mkesha saa 12.30 jioni mkesha wa Jimbo katika Kanisa la Mtakatifu Lucia.Sala na Tafakari zimeandaliwa na Waamini wa Kiorthodox wa Armenia.

Na Angella Rwezaula, - Vatican

"Kuna mwili mmoja, Roho mmoja, kama vile Mungu alivyowaita katika tumaini moja." Ndiyo Wito wa ushirika ambao ni  kauli mbiu itakayoongoza Juma la  Maombi kwa ajili ya  Umoja wa Wakristo, kuanzia Dominika tarehe 18 hadi Dominika 25 Januari 2026. Katika tarehe ya mwisho, ambayo ni Sherehe  ya Uongofu wa Mtakatifu Paulo Mtume wa Watu, saa 11:30 jioni katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Paulo Nje ya Ukuta, Papa Leo XIV atahitimisha Juma hilo kwa sherehe ya Masifu ya II ya  jioni

Mkesha wa Kiekumeni wa Jimbo Kuu

Miongoni mwa matukio mbalimbali yaliyopangwa, ya kati itakuwa mkesha wa kiekumeni wa Jimbo Kuu la Roma siku ya  Alhamisi, tarehe 22 Januari 2026,  saa 12:30 jioni,  saa za Ulaya katika Parokia ya Mtakatifu Lucia(Circonvallazione Clodia, 135). Wawakilishi wa madhehebu mbalimbali ya Kikristo waliopo Roma watazungumza katika ibada ya maombi; itaongozwa na Kardinali Baldo Reina, Makamu wa Papa Jimbo Kuu la Roma huku mahubiri yakitolewa na Askofu Mkuu wa Kiorthodox Khajag Barsamian, mwakilishi wa Kanisa la Kitume la Armenia katika Kiti Kitakatifu.

Matukio mengine mjini Roma

Pia kutakuwa na matukio mbalimbali katika makanisa na jumuiya zingine. Mikesha miwili itafanyika Jumatatu tarehe 19 Januari, mmoja saa 12:30 jioni katika Parokia ya (Dio Padre Misericordioso)Mungu Baba wa Huruma, na nyingine saa 1:15  usiku  huko (Santa Maria delle Grazie al Trionfale)Mtakatifu Maria wa Neema ya Ushindi. Siku ya Jumanne, saa 1:00 usiku, ibada ya maombi ya kiekumeni imepangwa katika Kanisa la (Santa Maria degli Angeli e dei Martiri), Mtakatifu Maria wa Malaika na Mashidi, wakati huo0 Ijumaa, tena saa 1:00 usiku mikesha itafanyika Parokia ya Mtakatifu Gioacchino huko Prati na Wakatifu Mario na Wenzake Mashahidi.

Tarehe 23, saa 2:00 Usiku, Askofu Mkuu wa Kianglikana Anthony Ball ataongoza katika Kanisa la Mtakatifu Maria huko Trastevere,  na wakati huo  wanafunzi kutoka Kituo cha Kiekumeni cha Bossey watakuwepo. Ibada itaendelea Jumamosi tarehe 24, saa 7:00 usiku katika Parokia ya Mtakatifua Caterina. Katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Maria huko Njia ya  Lata, Mabinti wa Kanisa, katika Kituo cha Ekaristi cha Kiekumeni wanasali kila jioni kulingana na ibada mbalimbali za Kikatoliki za Mashariki na Magharibi.

Sala zilizoandaliwa na waamini wa Kitume wa Armenia

Mwaka huu 2026, sala na tafakari zitakazotumika wakati wa Juma la Maombi kwa ajili ya Umoja wa Kikristo zimeandaliwa na waamini wa Kitume wa Armenia, kwa kushirikiana na kaka na dada zao wa Makanisa Katoliki na Kiinjili ya Armenia. Nyenzo hizo zilitayarishwa, kuhaririwa, na kujadiliwa katika makao makuu ya kihistoria ya kiroho na kiutawala ya Kanisa la Kitume la Armenia, Surp Etchmiadzin huko Yerevan, wakati wa baraka ya Muron (mafuta matakatifu) na kuwekwa wakfu tena kwa Kanisa Kuu la Mama, lililofanyika kati ya Septemba 28 na 29, 2024, kufuatia ukarabati mkubwa wa miaka kumi.

Adhimisho hili liliwapa watu wa Armenia na wanachama wa kikundi cha kiekumeni cha wenyeji fursa ya kutafakari na kusherehekea imani yao ya pamoja ya Kikristo. Nyenzo hizo hupata msukumo kutoka kwa tamaduni za karne nyingi za sala na maombi, ambazo kwa kawaida hutumika na watu wa Armenia, pamoja na nyimbo za kidini zinazotokana na monasteri na makanisa ya kale ya Armenia, ambazo baadhi yake zinaanzia karne ya 4.

Kutumia “Urithi wa Pamoja wa Kikristo”

Juma la  Maombi kwa ajili ya Umoja wa Kikristo 2026 inawaalika waamini kutumia urithi huu wa pamoja wa Kikristo na kuimarisha ushirika katika Kristo unaowaunganisha Wakristo duniani kote. "Tasaufi nchini Armenia ni ya kina na ya kale sana," alisema Monsignor Marco Gnavi, mwakilishi wa Jimbo  kwa ajili ya umoja wa kiekumeni na mazungumzo baina ya dini. "Mnamo mwaka 301, Ukristo ulipitishwa kama dini ya serikali. Maandiko yaliyopendekezwa kwa Juma la  Maombi yanazungumzia mwanga. 'Nuru kutoka kwa nuru' ni kifungu kikuu katika Imani ya Nicea, ambayo maadhimisho yake ya miaka 1700 tulisherehekea hivi karibuni. Kristo ndiye nuru yetu, na hii inatusaidia kuishi kwa matumaini katika wakati huu mgumu.

"Mashahidi wa Umoja"

Mada iliyochaguliwa ni mwaliko na wito wa umoja: "Sala," aliendelea, "inatuomba tujivuke sisi wenyewe, tufikie kila mmoja wetu, bila kusahau mizizi yetu, tukikubali mwaliko wa kutembea kuelekea umoja, si kwa sababu tu tunauhitaji, bali kwa sababu ulimwengu mzima unahitaji mashahidi wa umoja. Mafundisho ya Papa Leo XIV yako wazi na ya wazi katika suala hili, yanatualika kuzingatia amani kama matunda ya kutafuta umoja, kwanza miongoni mwetu na kisha miongoni mwa watu."

Juma Kuombea umoja 18-25 Jan

Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here

17 Januari 2026, 11:35