Tafuta

Katika maisha yetu ya kila siku ya ufuasi wetu, kwa nyakati mbalimbali tunakutana na Hofu, kukataliwa na kujihisi upweke na huzuni moyoni. Katika maisha yetu ya kila siku ya ufuasi wetu, kwa nyakati mbalimbali tunakutana na Hofu, kukataliwa na kujihisi upweke na huzuni moyoni.  

Tafakari Dominika 12 Mwaka A wa Kanisa: Msiogope! Tumaini na Ushuhuda!

Katika maisha yetu ya kila siku ya ufuasi wetu, kwa nyakati mbalimbali tunakutana na Hofu, kukataliwa na kujihisi upweke na huzuni moyoni. Tunajihisi kusahauliwa, tunajihisi kusalitiwa na kuachwa peke yetu katika mahangaiko yetu. Liturjia na Neno la Mungu katika Dominika hii inatupa moyo kwamba, katika hali hiyo hatupo peke yetu. Mwenyezi Mungu anasimama daima katikati yetu akitualika, “Tusiogope, Tumtumainie na Tumshuhudie kwa ujasiri.” Ondoa hofu!

Na Padre Bonaventura Maro, C.PP.S., -Kolleg St. Josef, Salzburg, Austria.

Utangulizi: Wapendwa Familia ya Mungu, ni Dominika ya 12 mwaka A wa Kanisa. Baba Mtakatifu Leo XIV, Jumamosi tarehe 20 Juni 2026 amefanya hija ya kichungaji kwa kutembelea Mkoa wa Lombardia, Kaskazini mwa Italia katika miji miwili ya Pavia na Sant’Angelo Lodigiano; miji ambayo imeacha chapa ya kudumu katika maisha na utume wa Baba Mtakatifu Leo XIV. Mtakatifu Augustino ni Muasisi wa Shirika la Waagostiniani: “The Order of St. Augustine, OSA.” Tangu mwanzo wa maisha na utume wake, Baba Mtakatifu Leo XIV alitia nia ya kutembelea maeneo ya maisha na utume wa Mtakatifu Augustino. Mji wa Pavia unahifadhi masalia ya Mtakatifu Augustino, Askofu na Mwalimu wa Kanisa ambaye katika mafundisho yake aliutazama unyenyekevu kama msingi wa imani ya Kikristo. Kwa tajiriba ya maisha na utume wake, Mtakatifu Augustino hatimaye alitambua kwamba ni mtu tu aliye na unyekekevu ndiye anaweza kumfuasa Kristo Yesu ambaye ni unyenyekevu wenyewe maana “hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho, bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu.” (Flp. 2:6-7.) Katika maisha yetu ya kila siku ya ufuasi wetu, kwa nyakati mbalimbali tunakutana na Hofu, kukataliwa na kujihisi upweke na huzuni moyoni. Tunajihisi kusahauliwa, tunajihisi kusalitiwa na kuachwa peke yetu katika mahangaiko yetu. Liturujia na Neno la Mungu katika Dominika hii inatupa moyo kwamba, katika hali hiyo hatupo peke yetu. Mwenyezi Mungu anasimama daima katikati yetu akitualika, “Tusiogope, Tumtumainie na Tumshuhudie kwa ujasiri.” Katika Dominika hii tumshukuru Mwenyezi Mungu; yeye aliyetuita, akatustahilisha na kututuma kuishuhudia Injili, anatupa nguvu kila mara tunapohisi hofu, upweke, kukataliwa na mahangaiko mbalimbali katika safari yetu ya ufuasi. 

Mwanadamu ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, ana utu na heshima yake.
Mwanadamu ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, ana utu na heshima yake.   (@Vatican Media)

Somo la Kwanza ni kutoka katika Kitabu cha Nabii Yeremia 20:10-13. Katika somo la kwanza tumesikia habari za Nabii Yeremia. Ni mmoja wa Manabii ambaye maisha na utume wake vilikumbwa majaribu na mateso muda wote, mwishoni mwa karne ya 7 BC na mwanzoni mwa karne ya 6BC. Kisiasa ni wakati ambapo taifa kubwa la Wababiloni lilianza kukua kwa kasi na kushambulia na kuchukua mateka maifa mengine. Taifa la Yuda nalo likawa katika hatari na hofu kubwa ya kuanguka na kupelekwa utumwani Babeli. Kwa nini walikuwa wapelekwe utumwani? Ni kwa sababu walikosa uaminifu kwa Amri na Agano la Mungu. Rushwa, matumizi mabaya ya madaraka, unyanyasaji wa maskini na dini ya juu juu vilikua ni mambo aliyoshamiri wakati huo. Yeremia anatumwa na Mungu kutabiri katika kipindi hiki kigumu, juu ya adhabu atakayoitoa Bwana kwa watu wa Yerusalemu. Matokeo yake watu walimkataa, walimdhania kuwa ni mchochezi, msaliti na mhaini, wakamtisha, wakamshtaki na baade wakamwua. Yeremia anasikia mashutumu kila mahali, hofu kutoka kila kona, hata marafiki zake wakasubiri kwa hamu kubwa maanguko yake kwa sababu ya kusimamia kweli ya Neno la Mungu. Katika somo hili ningependa tutafakari mambo yafuatayo yatakayotusaidia kuelewa ujumbe ambao Mama kanisa amependa kututafakarisha katika dominika hii ya 12 mwaka A wa Kanisa. Jambo la kwanza: Katika safari yetu ya maisha na wito tutegemee nasi kukutana na magumu.  Nabii Yeremia anatupa picha ya maisha yetu sisi pia ya kila siku katika kuiishi na kuishuhudia imani yetu. Nyakati za Yeremia, changamoto zilizokuwepo, vikwazo vilivyokuwepo ndio aina ya changamoto na vikwazo ambavyo nasi kama jamii, kama Kanisa kwa Ujumla, kama wabatizwa na kila mmoja katika wito wake binafsi anayoyapitia hata leo. Nabii Yeremia alitumwa kutangaza Neno la Mungu katika nyakati ngumu kijamii, kisiasa na kidini pia, katika jamii iliyopotoka, jamii iliyoacha mbali misingi ya Agano na Sheria ya Mungu, jamii iliyoishi imani ya nje nje tu. Licha ya hayo Nabii Yeremia alisimama imara, akiliishi na kulitangaza Neno la Mungu kwa vitendo. Matokeo yake aliishia kuteseka, kukataliwa, kupuuzwa kushutumiwa, kuonekana mchocheza na msaliti na mchonganishi. Baadaye tunaambiwa alifukuzwa na ilisemekana kuwa alifia huko Misri.

Waamini Jengeni hofu ya Mungu na Ibada ya kweli
Waamini Jengeni hofu ya Mungu na Ibada ya kweli   (@Vatican Media)

Somo hili linatupa nafasi kila mmoja binafsi, kama familia, kama jumuiya, kama Kanisa. Ni mara ngapi ndugu mpendwa tumekutana na hali ya kukataliwa, kupuuzwa, kusingiziwa, kushutumiwa na kudhaniwa vibaya katika safari yetu ya maisha, wito na utume wetu? Tumtazame Yeremia. Tunaishi kwenye jamii hali kadhalika na ulimwengu uliopotoka, ulimwengu unaokwenda asilimia kubwa kinyume na ukweli wa Injili, amri na sheria za Mungu. Mambo mbalimbali yasiyofaa kama vile rushwa, unyanyasaji kwa maskini, ukiukwaji wa haki za binadamu, matumizi mabaya ya madaraka, kutokuwajibika ipasavyo katika familia na katika Kanisa, matumizi mabaya ya madaraka na mambo na changamoto nyingine nyingi. Tunaishi katika nyakati ambazo ukweli unafichwa na kuogopwa kusemwa na kushuhudiwa kwa sababu ya hofu, na faida binafsi. Zipo pia nyakati mbalimbali ambapo tumesalitiwa na kukatishwa tamaa ya kuendelea kutenda tena wema hata kwa marafiki zetu, ndugu hata na jamaa zetu. Wapo watu pia waliosubiri kwa hamu, na kupanga au kuratibu maanguko yetu, na kuturudisha nyuma, kama ilivyokuwa tu kwa Yeremia. Huu ni uhalisia wa maisha yetu ya kila siku, ni uhalisia wa safari yetu ya wito na imani. Nabii Yeremia hakukata tamaa, nasi hatupaswi kamwe kukata tamaa. Nyakati hizi zipo, na zitaendelea kuwepo, lakini hazipaswi kutuvunja moyo. Zitusaidie tukue na tutoke imara kuliko mwanzo.

Jengeni hofu ya Mungu na Ibada ya kweli
Jengeni hofu ya Mungu na Ibada ya kweli   (@Vatican Media)

Jambo la pili: Katikati ya hofu, mashaka na mahangaiko na misukosuko yote katika safari yetu ya maisha, Mwenyezi Mungu yupo pamoja nasi, hatupaswi kuogopa wala kufa moyo. Nini jibu la Yeremia katika mapito na mahangaiko yake yote? Nini mtazamo wake katika yale yote aliyokuwa akiyapitia, katika nyakati zake hizo ngumu za kutisha? Katika somo hili la kwanza, Nabii Yeremia anatuonesha njia katika nyakati au hali hizi za hofu, mashaka, upweke na mahangaiko yetu. Katikati ya hali hii Yeremia anatamka maneno ya kutia moyo na kuamsha tena matumaini mapya, “Lakini Bwana yu pamoja nami, mfano wa shujaa mwenye kutisha, kwa hiyo hao wanaonionea watajikwaa, wala hawatashinda, watatahayarika sana.” Ndugu mpendwa, imani haimaniishi kutokuwepo kwa hofu, bali ni kuwa na tumaini thabiti na lisilotetereka hata katikati ya hofu. Yeremia alitumaini kwamba hata kama wanadamu hawakumwelewa, kumkubali na kumpokea Mungu alimwelewa, na kwake alipata daima kimbilio. Alitambua ya kuwa, Mungu, Bwana wa majeshi ndiye anayewajaribu wenye haki na anaona yeye mwenyewe mioyo yao. Yeye mwenyewe ndiye atakamuhesabia kuwa mwenye haki. Hivyo Yeremia katika changamoto na mapito yake, hakulaumu, hakukata tamaa, hakumlaani Mungu, hakupanga kulipa kisasi, hakukimbia kazi ya Mungu, bali aliona tumaini imara na thabiti mbele. Sehemu hii ya somo hili inaishia kwa namna ya kipekee. Yeremia anamsifu na kumtukuza Bwana, anaona ushindi mbele yake akiwa na Bwana hata kabla hajaufikia. Anaimba na kumtukuza Mungu ambaye kwake alitumainia ushindi, “Mwimbieni Bwana, msifuni Bwana, kwa maana ameiponya roho ya mhitaji, katika mikono ya watu watendao maovu.”

Changamoto ni sehemu ya vinasaba vya maisha ya Mkristo
Changamoto ni sehemu ya vinasaba vya maisha ya Mkristo   (@Vatican Media)

Nabii Yeremia anatoka kwenye hofu na kutumaini, anatoka kwenye mahangaiko hadi kumsifu Mungu ndio kiini cha sehemu hii ya somo hili la kwanza. Je, hata sasa ndugu mpendwa bado unajihisi mpweke, unajihisi kuwa peke yako, unajihisi yatima aliyetelekezwa katika mapito yako? Mwenyezi Mungu anasimama nawe hata kama ulimwengu mzima upo kinyume nawe. Yeye anatusaidia tuendelee kutumaini hata katikati ya bonde la uvuli wa mauti, hata katikati ya kilindi cha huzuni, hofu na mashaka ya maisha yetu. Tunaalikwa kushukuru, kwa kuwa tunaye Mungu anayeona undani wa mioyo yetu. Maneno ya watu, shutuma, masengenyo, visituvunje moyo. Tusitafute katika maisha kujitetea sana mbele za watu, kwa kuwa Mungu anaona ndani kabisa ya mioyo yetu. Inatosha Mungu akituhesabia kuwa wenye haki mbele zake, inatosha Mungu akikuelewa hata pale unapoonekana kutoeleweka kabisa kwa sababu ya imani yako, kwa sababu ya tumaini lako, kwa sababu ya uadilifu wako, kwa sababu ya kujitoa na kujituma kwako kutimiza wajibu wako wa kila siku. Je, umefanya nini, nimefanya nini nyakati ambazo nilijikuta nami au nilikuwepo au hata sasa nipo katika hali kama hii ya Yeremia? Katika familia, katika kazi zetu za kila siku, katika wito wako na katika majukumu yetu na katika jamii yetu.

Katika shida na changamoto za maisha, waamini wawe na imani thabiti
Katika shida na changamoto za maisha, waamini wawe na imani thabiti   (@Vatican Media)

Somo la Injili: Ni Injili kama ilivyoandikwa na Mathayo 10:26-33. Katika Injili Takatifu Dominika iliyopita, dominika ya 12 mwaka A, Kristo Yesu aliwachagua Mitume wake kumi na wawili, akawapatia nguvu na mamlaka, kisha akawatuma kwenda kuitangaza Injili. Mitume hawa walipaswa kuyahubiri kwa watu wote yale waliyoyasikia kutoka kwa Kristo, faraghani na hadharani, yaani Habari Njema ya Wokovu. Kristo alitambua kuwa, kama ilivyokuwa kwa manabii, kama hata yeye mwenyewe alivyopata upinzani mkubwa, hali kadhalika na mitume nao wategemee hayo hayo. Lakini Yesu anawatia moyo kwamba, wasiogope. Katika somo hili ningependa tutakafakari mambo yafutayo: Jambo la kwanza: Ukweli wa Injili hauwezi kufunikwa wala kufichwa kwa nguvu zozote za kidunia. Ipo thawabu kwa wale watakoishuhudia kiaminifu imani yao kwa Kristo. Katika somo hili la Injili Kristo anaanza kwa kuwasihi wanafunzi wake kwamba, “Msiwaogope, kwa maana hakuna Neno lililositirika, ambalo halitafunuliwa, wala liliofichwa ambalo halitajulikana. Aya zilizotangulia sehemu hii yaani 16-25, Bwana wetu Yesu Kristo alitoa maelekezo juu ya namna utume wao utakavyokuwa, kwamba, watachukiwa, watasalitiwa, watakamatwa na kupelekwa barazani na watafukuzwa. Hayo yote ni kwa sababu ya Injili, ni kwa sababu ya jina lake. Kisha sehemu inayoanza katika Injili ya leo, Kristo anawapa moyo tena, kwamba, wasiogope. Yesu alijua kabisa kuwa ulimwengu utajaribu kufunika na kuzima ukweli wa Injili, lakini ukweli na nguvu ya Neno hilo vitasimama na vitadhihirika mwishoni. Walichokipokea kwa faragha sasa wanapaswa kukisema juu ya paa bila kuogopa mamlaka za kidunia.

Waamini wanaitwa na kutumwa kutangaza na kushuhudia tunu msingi za Injili
Waamini wanaitwa na kutumwa kutangaza na kushuhudia tunu msingi za Injili   (@Vatican Media)

Ndugu mpendwa, kama ilivyokuwa katika nyakati za Nabii Yeremia, tunaishi kwenye ulimwengu ambapo ukweli wa Injili unajaribu kufunukwa na kupotezwa. Tupo kwenye ulimwengu ambapo tunu njema za Injili taratibu muda unavyozidi kwenda, zinatoweka. Vita, unyanyasaji, dhuluma, ubinafsi, rushwa, mmomonyoko wa maadili na mambo mengine mengi vinashamiri kwa kasi kubwa, huku jitihada kubwa pia zikifanyika kuuzima ukweli wa Injili. Yesu anatualika sote kuishuhudia imani yetu. Mambo ni mawili tu, au kumshuhudia Kristo au kumkana. Haitoshi tu kuhudhuria misa Takatifu, haitoshi tu kupokea Sakramenti, haitoshi tu kusoma Neno la Mungu, bali tunapaswa kuishuhudia kwa matendo imani yetu na kuiishi, kusimama imara juu kabisa na kwa ujasiri mkubwa na kuitangaza bila woga hata kama inakwenda kinyume na mitazamo ya kidunia. Je, katika wito kazi yangu nimemshudia namna gani Kristo? Kristo Yesu mwishoni mwa Injili hii anawaambia wanafunzi wake kwamba, “Basi, kila atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele ya Baba yangu aliye mbinguni. Bali mtu yeyote atakayenikana mbele za watu nami nitamkana mbele za baba yangu aliye mbinguni. Kumbe Kristo anatufundisha kuwa haiwezekani kuwa Mkristo wa kificho au vuguvugu kwa kuogopa macho ya watu. Kumkiri Yesu maana yake ni kusimamia misingi ya Injili kama vile haki, upendo, na uaminifu mbele ya jamii, hata kama mazingira yanayotuzunguka hayapendi misingi hiyo. Kipimo cha uaminifu wetu duniani ndicho kitakachokuwa kipimo cha Yesu kututambua mbele ya Baba yake wa mbinguni.

Ushuhuda wa imani inayomwilishwa katika matendo adili na matakatifu
Ushuhuda wa imani inayomwilishwa katika matendo adili na matakatifu   (@Vatican Media)

Jambo la Pili: Katika kumtumikia Mungu, hofu na uchaji wetu kwa Mungu vinatusaidia kushinda hofu zote za kiulimwengu. Bwana wetu Yesu Kristo anaendelea kwa kuwaambia wanafunzi wake kwamba, “Msiwaogope wauwao mwili, wasiweze kuiua na Roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuungamiza mwili na roho pia katika Jehanamu” Bwana wetu Yesu Kristo hapa anachora mstari kati ya kile kinachoweza kuharibiwa na mwanadamu na kile kinacholindwa na Mungu. Wanadamu wanaweza kuua mwili kwa maana ya maisha ya kibaolojia ya hapa duniani, lakini hawawezi kugusa roho yaani maisha ya milele. Hili ndilo lilimpa Nabii Yeremia nguvu ya kuendelea kutumaini. Hili ndilo liliwapa mitume hata baada ya Kristo kumaliza utume wake hapa duniani, nguvu ya kuitangaza Injili bila hofu na wengi kweli waliteseka sana kufa kifo dini kwa ajili ya Kristo. Ndugu mpendwa, Bwana wetu Yesu Kristo anatufundisha namna tunapaswa kuwa na mtazamo tofauti juu ya hofu, juu ya magumu, juu ya maumivu, juu ya mateso na madhulumu tunayokutana nayo, au tutakayoendelea kukutana nayo katika kuishuhudia imani yetu. Hofu pekee ya kweli na ya kimungu tunayopaswa kuwa nayo ni kumheshimu Mungu pekee, ambaye ana mamlaka ya milele juu ya maisha yetu. Tukimwogopa Mungu pekee, tunakuwa huru dhidi ya hofu zote za wanadamu. Lakini mara nyingi inakua rahisi kumwacha Mungu na kuyashikilia yale yanayotupa hofu za muda za hapa duniani, vyeo, mamlaka, mali, utajiri, sifa na heshima, nguvu nk. Haya yote kwa yenyewe bila Mungu yatatukosesha Mungu, kwa kuwa yatatupa ulinzi dhidi ya mwili ilihali tutazipoteza roho zetu.  Tunahamisha hofu ya Mungu na kuwa na hofu juu ya mambo ya ulimwengu huu. Kama Mitume walivyopaswa kutokuwa na hofu juu ya masuala ya kiulimwengu, hali kadhali nasi leo tuombe neema ya kuwa na hofu ya Mungu kama tulivyosali katika sala ya mwanzo kwamba, “Ee Bwana utujalie tuliche daima jina lako takatifu na kulipenda, maana huwanyimi kamwe uongozi wako, wale uliowaimarisha katika upendo wako.”

Mwanadamu ana thamani kubwa machoni pa Mungu
Mwanadamu ana thamani kubwa machoni pa Mungu   (@Vatican Media)

Jambo la Tatu: Sisi tu wenye thamani kubwa sana machoni pa Mungu. Kristo anawaambia wanafunzi wake na anatuambia sisi sote kwamba, sisi tu wa thamani kubwa sana machoni pa Mungu, na Mungu ndiye anayetutegemeza. Anatoa mfano katika mazingira ambayo ulifahamika vyema sana; Je, shomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu. Katika masoko ya Kiyahudi ya karne ya kwanza, shomoro walikuwa ndio ndege wadogo, wa hali ya chini, na wa bei rahisi zaidi waliouzwa kama chakula cha maskini sana, wawili wakiuzwa kwa sarafu moja ya shaba. Walionekana kama viumbe wasio na thamani kubwa mbele ya macho ya jamii. Ndugu mpendwa nini maana ya mfano huu wa Kristo kwa wanafunzi wake? Maana ya mfano huu ni kwamba, ikiwa Mungu anajali na kufuatilia maisha na kifo cha Shomoro, kiumbe mdogo, asiye na thamani kubwa na wa bei rahisi namna hiyo, hakika ameshikilia maisha yetu sisi wanadamu ambayo kwake yana thamani kubwa sana. Mungu hausiki tu na mambo makubwa ya ulimwengu, bali anajali na anahusikia hata na mambo madogo madogo kabisa ya kila siku ya viumbe vyake. Kristo anaeendela na fundisho hili kwa kusema, “Lakini ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabika zote. Msiogope basi, kwa kuwa ninyi ni bora kuliko mashomoro wengi.” Kawaida nywele ni kitu kidogo sana mwilini ambacho kinakua, kinakatika, na kuanguka kila siku bila sisi wenyewe kuzihesabu au kujali idadi yake. Hatujui tuna nywele ngapi kichwani kwa sababu hazina uzito mkubwa kwetu. Mwenyezi Mungu anatujua kwa undani. Anajua mambo yetu madogo ambayo hata sisi wenyewe hatuyajui au hatuyatilii maanani. Hakuna undani wa maisha yako, maumivu yako, au hofu zako unaoweza kufichika mbele ya Mungu. Wakati tunapopitia mateso, kukataliwa, au dhiki kwa kusimamia ukweli kama Nabii Yeremia katika somo la kwanza, ni rahisi kufikiri kuwa Mungu ametusahau au hatujali. Yesu anatumia shomoro na nywele kututhibitishia kuwa, hatuwezi kupotea machoni pa Mungu. Kila jaribu tunalolipitia anajua uzito wake. Usalama wako wa milele uko mikononi mwake, kwa sababu thamani yako kwake ni kubwa kupitiliza.

Ukweli wa Injili lazima utangazwe na kushuhudiwa
Ukweli wa Injili lazima utangazwe na kushuhudiwa   (@Vatican Media)

Somo la Pili: Ni kutoka katika Waraka wa Mtume Paulo kwa Warumi 5:12-15. Katika somo hili la pili Mtume Paulo anatufundisha kuwa, kupitia mtu mmoja Adamu, dhambi na mauti viliingia duniani na kuenea kwa wanadamu wote, jambo linalosababisha mateso na uadui tunaoshuhudia leo katika historia ya Mwanadamu. Lakini Adamu wa pili, yaani Bwana wetu Yesu Kristo ameleta neema nyingi zinazoshinda dhambi na adhabu zake. Ukombozi wetu kwa njia ya neema ya Yesu Kristo una nguvu na thamani kubwa zaidi kuliko uharibifu uliosababishwa na dhambi, na hiki ndicho kiini cha somo la waraka huu wa Mtume Paulo. Neema hii kimsingi haikufuta tu makosa, bali imetupa hadhi na thamani kubwa tena ya kuwa wana wa Mungu. Mtakatifu Paulo anatukumbusha tena kuwa tuko salama chini ya ulinzi wa Kristo ambaye tayari ameshashinda dhambi na mauti ya mwili kwa njia ya kifo chake msalabani. Hitimisho: Katika Dominika hii tuombe neema ya Mungu ya kuwa tayari kuitika wito wa Mungu kwa kuwa yeye BWANA mwenyewe, ndiye nguvu na wokovu wetu.

Tafakari D 12 Mwaka A
20 Juni 2026, 17:16