Papa Leo XIV:Tusali kwa ajili ya kaka na dada zetu waliopoteza maisha yao baharini
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV akiwa katika Ziara yake ya Kitume na kituo chake cha Mwisho huko Visiwa vya Kanari aliongoza Ibada ya Misa Takatifu, Alhamisi jioni, tarehe 11 Juni 2026 ikiwa ni tayari kwenye Mkesha wa Sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu. Misa ilifanyika katika Uwanja wa michezo huko Las Palmas ambapo waamini 50,000 waliudhuria tukio hili muhimu. Na ndiyo ilikuwa hitimisho la siku yake ya kwanza katika uwanja wa mji huu.
Sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu
Baba Mtakatifu akianza mahubiri alisema: “Wapendwa kaka na dada, baada ya siku yenye wingi wa kukutana na kushiriki, sasa, nikisherehekea Ekaristi hii pamoja nanyi, kwanza kabisa nataka kumshukuru Bwana kwa mema mengi yanayofanyika hapa kila siku, nikimkabidhi Yeye kujitolea kwa wote na wakati huo huo mateso ambayo nchi hii inashuhudia. Pia ninawaalika kusali pamoja, katika Misa hii Takatifu, kwa ajili ya kaka na dada waliopoteza maisha yao baharini. Tunaleta kila kitu madhabahuni, pamoja na mkate na divai, tunapoingia, pamoja na sherehe ya jioni ya Mkesha, katika Sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu, ambayo nchini Hispania yote imewekwa wakfu kwake. Tumwombe Bwana kwamba kwa wakati huu hisia zile zile za ubinadamu, upole na huruma za Moyo Mwokozi ziweze kuwa hai ndani yetu.”
Mungu anawakumbusha Waisraeli kuhusu upendo
Baba Mtakatifu aliendelea kusema, “Tujiruhusu kuongozwa katika kutafakari kwetu kwa masomo tuliyosikia. Kwanza kabisa, Mungu anawakumbusha Waisraeli kuhusu upendo usio na masharti ambao aliwapenda nao. Hakuwachagua kwa sababu walikuwa na mapendeleo, zawadi, au sifa zozote maalum, bali kwa upendo safi (taz. Kum 7:7-9), na ataendelea kuwapenda siku zote, hata wakati, kwa sababu ya mioyo yao migumu, hawarudishi hisia zake. Huu ni upendo wa Mungu, ambapo wito wetu wa kupenda umejikita. Hautegemei hesabu, wala hisia tu, wala hauwezi kupunguzwa kuwa upendo rahisi, bali unaenea katika nafsi yetu yote.
Moto kwa ajili ya roho, mwanga kwa ajili ya akili, msukumo usiozuilika wa uhuru, amani na wakati huo huo mateso kwa ajili ya moyo, ambao hudunda kwa upatanisho na mioyo mingine, ikimhusisha mtu mzima. Kwa sababu upendo ni wa asili kwa wanadamu; kiukweli, ni sharti la ukamilifu wa kuwepo. Hivi ndivyo upendo unavyooneshwa kwetu katika ubinadamu wa Mwokozi na katika harakati za Moyo wake Mtakatifu Zaidi: usiobadilika na mwaminifu hata katika hali ya kutoelewana na kukataliwa, hofu, huzuni na upinzani wa kibinadamu(Lk 22,39-46).
Mwitikio bora wa upendo kwa moyo wa Yesu ni kwa kaka na dada
Na ni katika uso huu wa Mungu, daima "katika upendo," ambaye anatamani sana mema yetu na furaha yetu kamili, Papa alieleza " ndipo tunapotambua njia ya maisha, kujifunza njia mpya ya kuishi na kuhusianisha, kigezo tofauti cha kutathmini maamuzi, mtindo mpya na wa kuchochea wa kujenga ushirika. Katika suala hili, Papa Francisko, akizungumzia upendo wa Kristo, alisema kwamba: "mwitikio bora kwa upendo wa Moyo wake ni upendo kwa kaka na dada zetu" (Dilexit nos, 167) na akaongeza: "hakuna ishara kubwa zaidi tunayoweza kumpa ili kurudisha upendo kwa upendo.
"Kurudisha upendo kwa upendo": Huu ni ubadilishanaji wa ajabu, "biashara ya kupendeza" ambayo Injili inatualika tuvutwe, ikitafsiri kipimo kisicho na kikomo cha upendo wa Mungu kuwa ukarimu ambao tunamtumikia, kila siku, katika kaka na dada katika Yeye mwenyewe anayemweka njiani mwetu. Hasa kwa wale walio na uhitaji mkubwa, wasio na ulinzi, wasioweza kutoa chochote (taz. Lk 6:32-36).
Papa aliwapongeza kwa ukarimu kwamba "Kama inavyotokea kisiwani hapa, katika kukaribisha, kushiriki, katika kutoa bila ubinafsi.” Hata hivyo, kujitolea kwa Moyo wa Kristo hakuishii hapo. Kunaendelea zaidi, kujitoa kumsaidia kila mtu si tu kuishi, bali pia kupata tena kujiamini na kuanza safari yake, kukua na kustawi kikamilifu katika upekee wake, kwa manufaa ya wote. Katika suala hili, Papa Benedikto XVI aliandika kwamba upendo "ambao Yesu Kristo alishuhudia kwa maisha yake ya kidunia [...] ndiyo nguvu kuu ya kuendesha maendeleo halisi ya kila mtu na ya wanadamu wote." (Caritas in veritate, 1).
Mungu alituma mwanae wa pekee
Baba Mtakatifu Leo alijikita kutazama katika somo la pili, kwamba "Mtakatifu Yohane alitukumbusha kwamba “Mungu alimtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa njia yake” (1 Yoh 4:9). Maneno yake yanarudia yale ya Yesu, ambaye alisema kwamba alikuja ili tupate uzima, na kuupata tele (taz. Yh 10:10), na ambaye alimwagiza yule aliyepooza na kuponywa kuwa: “Inuka, beba kitanda chako, utembee” (Mk 2:9). Katika misemo hii, tunatambua mwaliko wa kukumbatia mateso kwa upendo wa kimama, lakini wakati huo huo kuwaandaa na kuwatia moyo waliojeruhiwa ili waweze kuinuka na kusonga mbele tena, kuelekea maisha huru na yenye heshima.
Tumaini katika safari
Hakika, Papa Leo alionya kuwa "upendo wetu haupaswi kuwa msaada tu, bali ujumuishaji wa watu kwa ajili ya utambuzi wao kamili, kiroho, kiakili, na kimwili na ujumuishi wao wenye hadhi na kujenga katika jamii (taz. Fratelli tutti, 129). Ni kwa njia hiyo tu, ndipo kukutana kwetu, hata katika kukabiliana na matukio magumu na yenye uchungu, kutakuwa fursa za kupanda mbegu za matumaini katika safari ya wanadamu kuelekea mustakabali bora.
Moyo wa Kristo:utajiri unatupofusha
Papa alikazia kusema alivyopenda kuzingatia "Neno la Mungu tulilosikia, kuhusu sifa moja ya mwisho ya Moyo wa Kristo: unyenyekevu (taz. Mt. 11:29). Moyo wa Yesu ni mnyenyekevu, na ndiyo maana mapigo yake hayasikiwi na "wasomi," "wenye hekima," yaani, wale wanaojiona kuwa wanajitosheleza, kujua kila kitu, kutohitaji Mungu wala wengine. Kiukweli, watu hawa, wamezidiwa na kelele za "umimi" wenye majivuno, waliopo kila mahali, na wenye kufadhaika, hawana ukimya unaohitajika kusikia ndani yao wenyewe na ndani ya kaka na dada zao mapigo ya upendo yaliyofichwa.
"Mara nyingi, utajiri hutupofusha, hadi kufikia hatua ya kufikiria kwamba furaha yetu inaweza kupatikana tu ikiwa tutaweza kuishi bila wengine"(Dilexi te, 108). Yesu, kwa upande mwingine, anatufundisha kinyume chake: ili kupata furaha ya kweli ya maisha, ambayo inakaa katika upendo, ni muhimu kujiondoa kutoka kwenye misingi ya kiburi inayogawanya, na kujikuta katika unyenyekevu unaotuunganisha kama kaka na dada.
Mtakatifu Agostino:palipo na upendo kuna amani
Mtakatifu Agostino alisema: “Pale palipo na upendo, kuna amani, na palipo na unyenyekevu, kuna upendo”(Katika Barua ya Kwanza ya Mtakatifu Yohane kwa Waparthi, Dibaji). Ndivyo ilivyo. Pale palipo na unyenyekevu wa kweli, kuna upendo, na palipo na upendo, kuna amani, Papa alikazia tena, kwa sababu aliongeza " ni katika unyenyekevu pekee ndipo tunapojua kweli sisi ni akina nani na, kwa hivyo, tunaweza kupendana, kukutana, kujitolea kwa kila mmoja, na kusameheana kiukweli.
Tunaabudu Moyo Mtakatifu wa Yesu
"Kaka na dada wapendwa, Papa Leo XIV aliongeza:"leo tunaabudu Moyo Mtakatifu wa Yesu, moyo ambao mara nyingi tunauonesha ukivikwa taji la miiba na kuwaka kwa moto, kulingana na maono ya Mtakatifu Margaret Mary Alacoque. Tukumbuke kwamba sisi ni uwepo hai wa Bwana duniani (Lumen Gentium,8). Kwa hivyo, “tutazame kila mmoja wetu, si leo tu, bali kila wakati, kwa heshima na uaminifu, na tupyaishe, katika ufahamu huu, kujitolea kwetu kutimiza ndani yetu, kupitia upendo, kile kilichopungua katika mateso ya Kristo, kwa ajili ya mema ya Kanisa (taz. Kol 1:24).” Kwa kuhitimisha Papa Leo alisema kwamba “Tukiwa tumechochewa na upendo wa Moyo wake, tuwe wabebaji wa huruma yake na amani yake, ili vita vikome duniani na ubinadamu mpya, uliopatanishwa katika upendo, uweze kukua karibu nasi.”
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here
