Papa Leo XIV kwa Familia Takatifu:Tunapoinua macho yetu kwa mfufuka,tuinue nyuso za walio mavumbini
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV aliongoza Ibada ya Misa Takatifu katika Basilika ya Familia Takatifu huko Barcelona jioni tarehe 10 Juni 2026 akiwa katika Ziara yake ya 4 ya Kitume nchini Hispania. Mara baada ya kufika Basilika hiyo alikwenda kusali mbele ya Sakramenti Takatifu na kutembelea kaburi la Antoni Gaudí, ambaye maono yake yaliifanya Basilika hiyo kuwa jambo muhimu la imani ya Kikristo kupitia usanifu, mwanga, rangi na ishara.
Misa hiyo ilikuwa pia ni kumbukizi ya miaka mia moja ya kifo cha mwanzilishi Kanisa hilo kuu, Gaudí na hatimaye kulikuwa na baraka ya Mnara wa Yesu Kristo. Lilikuwa ni tamasha zuri wakati wa kuuzindua.
Ni katika muktadha wa Msalaba ambapo Baba Mtakatifu Leo XIV alijikita kutafakari wito wa Injili ya imani na kusisitiza kwamba imani halisi katika Kristo haiendani na vurugu, kutojali, na kupuuza wale wanaoteseka. "Hatuwezi kumwamini Yesu na kupigana vita. Hatuwezi kumwamini Yesu na kuwaua wasio na hatia. Hatuwezi kumwamini Yesu na kuwaacha wale wanaoteseka, wale wanaolia, wale wanaokimbia umaskini. " Papa alisisitiza "Kanisa hili ni jengo moja, lililoundwa na mawe mengi. Nyumba inayokua kwa kasi kwa miaka mingi, kulingana na mpango unaofanana. Sisi sote ni mawe hai ya kazi hii, ambayo Kristo ndiye msingi na kilele chake, mwanzo na mwisho wake.
Basilika, iliyowekwa wakfu mwaka 2010 na Papa Benedikto XVI kama "ishara inayoonekana ya Mungu asiyeonekana," bado ni eneo la ujenzi leo hii, ambalo, Papa Leo XIV alisema, "linatukumbusha kwamba maisha ya Kikristo daima ni safari, kwa sababu ni mpango, ambao Mungu hukamilisha." Kwa hivyo, hatuishi katika kazi ambayo haijakamilika, bali ni hekalu ambalo bado linajengwa. Ukamilifu wake si kasoro, kwa sababu unathibitisha hamu; haimaanishi upungufu, lakini unaonesha ahadi, ambayo tunataka kuiheshimu kila wakati. Kwa hivyo kujitolea kushirikiana na mpango wa Mungu wa kutufanya kuwa kazi yake bora. "Ni yeye anayetupa mahali, na mahali anapotupatia ni moyo wake: mahali pa Mwana, kwa ajili yetu tuliokuwa wageni; mahali pa Mpendwa, kwa ajili yetu sisi wenye dhambi."
Kwa kutazama usanifu wa Basilika hiyo na maana yake ya ndani kabisa, Papa Leo XIV alisisitiza kwamba sura tatu za Familia Takatifu ni marejeo ya Msalaba wa Yesu. Kwa hivyo, jioni hii, tunakumbuka kwamba Msalaba wa Kristo, uliowekwa juu ya Basilika hii ni Msalaba wa walio wa mwisho wanaokuwa wa kwanza, wa wenye dhambi wanaokuwa watakatifu, na wa wafu watakaofufuka tena." Kwa kushangilia Mnara wa Yesu Kristo, ambao Papa Leo XIV mwenyewe aliuzindua na chini yake kuna maandishi "Tu solus Sanctus, Tu solus Dominus, tu solus Altissimus," " Kwa kuwa wewe ndiye Mtakatifu, uliye Bwana na aliye juu." Papa Leo XIV alitoa mwaliko wa kuinua macho yetu juu ili kupata ukweli, kama ilivyo kauli mbiu ya ziara yake.
Kwa hivyo, Mnara wa Msalaba unakuwa bendera ya upendo, kwa sababu Mungu anatupenda hivyo, akibadilisha chombo cha kifo kuwa ishara ya tumaini. Msalaba huu unang'aa mchana, ukiakisi mwanga wa jua, na unang'aa usiku, ukiangaza mji kama taa inayoangalia Bahari ya Mediterania. Msalaba ni ishara inayong'aa ya upendo wa Mungu, na "Kristo atakapoinuliwa, ubinadamu wake mkuu," Papa alisisitiza, "unang'aa kwa utukufu, na kazi zetu zinamtukuza Mungu.
Ni kazi za imani, na sanaa inazidi miongoni mwa hizi." Imani huumba mawe, hutoa maana kwa kile kilichojengwa kwa sababu Mungu ndiye msanii wa kweli, na mwanadamu "analingana na kazi ya Mungu kwa werevu wake mwenyewe," na kuifanya iwe sifa kwake. Kama mbunifu mwenye bidii katika imani, mtumishi wa Mungu Antoni Gaudí alibuni nafasi hizi kwa nia ya kusimulia mafumbo ya maisha ya Bwana: kwa njia hii, alipendekeza hija ya kiroho, na kusababisha kukutana na Kristo, aliyezaliwa, aliyekufa, na aliyefufuka kwa ajili yetu.
Akiwashukuru wale ambao baada ya muda wamechangia kufadhili Sagrada Familia, "kito cha usanifu," Papa Leo XIV alisisitiza kuwa ni "ambacho pia ni katekesi fasaha iliyotengenezwa kwa mawe, rangi, na mwanga." Alisisitiza tena kwamba likiakisi ufunuo wa Biblia wa makanisa makuu ya kale, hata leo hii katika Basilika hii ni dhahiri ya "jinsi sanaa na uzuri zilivyo njia kuu za uinjilishaji."
