Tafuta

Papa Leo XIV,Kisiwa cha Kanari:Hadhi ya binadamu haina pasipoti,haipotezi thamani inapovuka mpaka!

Haitoshi kusimamia wanaowasili,kusambaza idadi,kuimarisha mipaka au kuomboleza vifo mara tu vinapotokea.Kila boti inayofika haileta wahamiaji tu bali swali:tumejenga ulimwengu wa aina gani ikiwa kaka na dada zetu wengi wanahatarisha kifo wakitafuta maisha?Hadhi ya binadamu inahitaji njia salama,ushirikiano wa kweli dhidi ya wafanyabiashara haramu.Amesema hayo Papa Leo XIV,Juni 11 wakati wa Mkutano huko Las Palmas ya Kisiwa cha Kanari.

Na Angella Rwezaula – Vatican.

Baba Mtakatifu Leo XIV amewasili katika moja ya Kisiwa kikubwa cha Kanari  kilichomsubiri kwa hamu sana, Alhamisi tarehe 11 Juni 2025 ikiwa ni hatua yake nyingine ziara yake ya Kitume nchini Hispania. Kwa njia hiyo alikutana na hali halisi ya wataalamu wa ujumuishaji wa wahamiaji katika uwanja wa ukingo wa pwani ya Bahari ya Arguineguín huko  Las Palmas ya Kisiwa kikubwa cha Kanari. Baba Mtakatifu alisikiliza awali ya yote Askofu wa Jimbo hilo na kufuatia na ushuhuda kutoka kwa watu wa nne: Kapteni wa baharia, ushuhuda wa mtu wa kujitolea wa Caritas, mwakilishi wa mwathirika wa biashara haramu ya binadamu na hatimaye mfanyabiashara kutoka Amerika Kusini.

Papa akibariki baada ya kufika
Papa akibariki baada ya kufika   (@Vatican Media)

 

Baba Mtakatifu Leo IV alitoa hotuba yake kwamba, tumesikia  tu mojawapo ya vifungu vyenye changamoto kubwa katika Injili. Tunajua kwamba sura hii hii pia ina onyo ambalo hakuna mwamini anayeweza kulichukulia kirahisi (Mt 25:41-45). Leo, kwenye ufukwe  wa bahari, Neno linakuwa halisi: maisha mengi yaliyojeruhiwa yanafika hapa, yakiwa yamevuliwa karibu kila kitu, lakini kamwe,  hayana hadhi yao. Hapa Injili inatutoa kwenye kiti cha starehe cha mtazamaji na kutuweka mbele ya ndugu anayefika. Inatuuliza kama tumeweza kumtambua Kristo ndani ya wale wanaoshuka, wakiwa na kovu la hofu, njaa, na vurugu, baada ya jangwa, usiku, na bahari.

Aliyesoma historia ya mwathirika wa biashara haramu ya binadamu
Aliyesoma historia ya mwathirika wa biashara haramu ya binadamu   (@Vatican Media)

Papa Leo XIV alisema kwamba “Kisiwa hicho, kidogo kwa ukubwa lakini kikubwa katika ubinadamu, kimeona maelfu ya watu wakichukuliwa kutoka nchi yao na kukabidhiwa kwa udhaifu wa cayuco. Kuna watu waliookolewa baharini na miili isiyo na uhai ikipatikana kutoka majini. Hii ndiyo sababu Mrithi wa Petro hawezi kupuuza kutua huku. Kanisa haliwezi kupuuza maji haya, wala mahali popote ambapo njaa, kiu, vurugu, hofu, au uhamisho vinaendelea kuumiza heshima ya binadamu. Wanafunzi wa Yesu hawawezi kupuuza kelele za wale wanaolia kutoka usiku kama wageni.

Katika lugha ya kibiblia, “bahari inaweza kuwa taswira ya tishio, giza, na machafuko. Kunaonekana Leviathani, mfano wa nguvu na  Rahabu, jina linaloamsha kiburi cha nguvu zinazoinuka dhidi ya Mungu na dhidi ya uzima. (Zab 74,13-14; 89,10-11; Is 27,1; 51,9; Ay 26,12).  Hata leo hii wanyama wakali hujificha katika bahari hizi, ambapo Papa amewafananisha na vikundi vya kihalifu kama vile mafia wanaosafirisha watu kama bidhaa, wafanyabiashara wanaowatumikisha wanawake na watoto, na kutojali kwa wengi kunakoruhusu maskini kumezwa na unyonyaji au kusahaulika.

Lakini imani haizuiliwi na nguvu ya bahari. Tunaamini katika Mungu anayeshinda machafuko, anayeweka mipaka juu ya uovu, na kufungua njia wakati kifo kinaonekana kushinda. Hiki ndicho watu wa Israeli walichopitia walipovuka Bahari Nyekundu ili kuepuka utumwa na safari ya kuelekea uhuru (Kut 14:21-31). Na kwa hivyo tunamtafakari katika Kristo, anayetembea juu ya maji na, akikabiliwa na dhoruba, anasema neno kuu: "Amani, tulia!" (Mk 4:39; Mt 14:25-27). Sauti hiyo inaendelea kusikika dhidi ya nguvu zinazowameza, kuwatumikisha, na kuwatupa kaka na dada zetu wengi. Pale ambapo Kristo anaamuru bahari iwe kimya, Kanisa haliwezi kukaa kimya mbele ya wale walioachwa kwenye maji yake.

Bondi ya uokoaji
Bondi ya uokoaji   (@Vatican Media)

Maana ya kuokoa maisha

Asante kwa ushuhuda wako; kwa kutukumbusha maana ya kuokoa maisha ya María; asante kwa kutukumbusha kile ambacho Caritas, parokia, na wengine wengi hufanya kila siku. Maneno yako yanatuonesha mahali ambapo ubadilishaji wa mtazamo huanza: wakati mhamiaji anapoacha kuwa "mmoja wa wengi," anaacha kuwa kategoria na mtu. Hapo ndipo tunapoelewa kwamba msichana huyo mdogo anaweza kuwa binti yetu, nyuso hizo zinakuwa sehemu ya familia yetu; na kisha, dhamiri yetu haina visingizio zaidi. Huruma  huanza na ishara ndogo: wakati mwingine na biskuti chache na maziwa kidogo; wakati mwingine, na mikate mitano na samaki wawili  (Mt 14:17-21). Sio kuhusu kutatua kila kitu, bali kuhusu kuweka kila kitu mikononi mwa Mungu na kuwepo popote ambapo wanadamu wanateseka, ambapo rasilimali hazitoshi na hakuna lugha ya kawaida, lakini ambapo ishara bado zinaweza kuzungumza. Shukrani za dhati kwa wale wote wanaojiunga katika juhudi za kutoa misaada, makaribisho, na usindikizaji, wakishuhudia kwamba huruma halisi inaweza kuokoa na kubadilisha maisha ya watu wengi.

Ushuhuda wa Blessing

Mpendwa Blessing hata kama hayupo hapa leo, sauti yako iko hapa. Asante kwa kushirikisha historia  yako nasi.” Jina lako linamaanisha "baraka" na linatukumbusha kwamba maisha ya kila mwanadamu ni baraka kutoka kwa Mungu. Hakuna awezaye kuinunua, kuiuza, kuitumia au kuitupa, kwa sababu sura na mfano wa Muumba huangaza ndani ya kila mtu(Mwa 1:27). Akimnukuu, Papa alisema “Ulituambia kwamba uliiacha nchi yako, si kwa sababu ulitaka, bali kwa sababu hakukuwa na chaguo lingine. Kwa maneno yako tunasikia janga la  watu wengi kulazimishwa kuondoka kwa sababu umaskini, vita, vitisho au unyonyaji vimewafungia kila njia nyingine.”

Wakati wa hotuba na kusikiliza shuhuda
Wakati wa hotuba na kusikiliza shuhuda   (@Vatican Media)

Mungu hajawahi kuacha  mtu

Ni katika muktadha huo, ambapo Papa Leo XIV alisema kuwa,  “Ninapenda  ujumbe huu ukufikie wewe na wanawake wengi walioathiriwa na biashara haramu na unyonyaji: ikiwa wengine wameweka bei kwenye mwili wako, Mungu hajawahi kuacha kukutazama kama mtu mwenye thamani isiyopimika. Kama walivyotaka kukufungia katika historia yenye uchungu, Mungu anaendelea kutamka ahadi ya wakati ujao. Kama walikutendea kama kitu, Kanisa linataka kukuambia leo hii: wewe ni binti na dada, wewe ni baraka. Maisha yako si ya wale waliokuumiza; mwili wako si wa wale waliokutumia vibaya; Siku zako si za wale waliotaka kuwafunga kwa hofu! Maisha yako ni ya Mungu na yanahifadhi heshima ambayo hakuna mtu anayeweza kukunyang'anya. Na tunataka kutembea nawe, hadi ukweli huo usikike tena, wenye nguvu kuliko maumivu.”

Kwa wahamiaji:ninyi siyo idadi,ni watu na ndoto

Wahamiaji wapendwa: Kabla ya kusema jambo lingine lolote kwenu, Papa aliongeza “ninataka kuinama mbele ya heshima yenu. Nyinyi si watu wa idadi, wala mafaili! Nyinyi ni watu wenye familia na nyumba mliyoiacha, wenye ndoto ambazo hakuna mtu mwenye haki ya kuzidharau. Lakini pia nataka kuwaambia kwamba maisha yenu lazima yalindwe. Msiwakabidhi uhai wenu kwa wale wanaofanya biashara hiyo. Msiwaamini wale wanaoahidi mbingu rahisi badala ya mwili wenu, pesa zenu, ukimya wenu, au uhuru wenu. Ahadi hizo za uongo ni "nyimbo za king'ora," viwanda vya kifo. Hali yenu lazima iwe uchunguzi wa dhamiri: kwa mataifa ya asili, ambayo lazima yaunde hali ya amani, haki, na maendeleo; kwa mataifa ya usafiri, yaliyoitwa kulinda na kutowaacha wanyonge kwenye mitandao ya uhalifu; kwa Ulaya, ambayo haiwezi kutangaza heshima ya binadamu na kuzoea Mediterania na Atlantiki kuwa makaburi bila mawe ya makaburi; kwa jumuiya ya kimataifa, iliyoitwa kwa ushirikiano mzuri na unaoendelea.”

Papa akipokea maua kutoka kwa wahamiaji
Papa akipokea maua kutoka kwa wahamiaji   (@Vatican Media)

Kanisa lazima lichangamotishwe

Papa Leo XIV alisisitiza kwamba “Kanisa lazima pia lijiruhusu kupingwa. Kuwakaribisha wahamiaji hakuwezi kuwa jukumu la pili, wala haliwezi kukabidhiwa kwa watu wachache wa kujitolea pekee. Tunapiga magoti mbele ya madhabahu ili kumwabudu Kristo aliyepo katika Ekaristi, ambayo tunapokea nguvu na motisha ya kufanya matendo ya upendo. Kwa hivyo, hatuwezi "kupita" mbele ya waamini, kwani kila ibada hutoka kwenye sala na kila ahadi hurudi kwake (Lk 10:31-32). Kutoka kisiwa hiki, ningependa sauti za wale waliozungumza leo ziwafikie wale walio na majukumu muhimumamlaka ya kiraia, mabunge, serikali, na mashirika ya kimataifa—pamoja na jumuiya za Kikristo, mila zingine za kidini, na wanaume na wanawake wote wenye mapenzi mema.

Kila Boti hailet wahamiaji tu bali swali

Haitoshi kusimamia waliofika, kusambaza takwimu, kuimarisha mipaka, au kuomboleza vifo mara tu vitakapotokea. Kila mashua inayofika haileti wahamiaji pekee; inaleta swali: tumejenga ulimwengu wa aina gani ikiwa kaka  na dada zetu wengi wanapaswa kuhatarisha kifo wakitafuta maisha? Utu wa binadamu unahitaji njia salama na za kisheria, unafuu na usaidizi, ushirikiano wa dhati dhidi ya wafanyabiashara haramu, ulinzi mzuri wa waathiriwa, michakato ya mapokezi na ujumuishaji makini, na sera zinazomruhusu kila mtu kuishi kwa heshima katika nchi yake.  Ikiwa kuna haki ya kutafuta kimbilio wakati maisha yanatishiwa, pia kuna haki ya kutolazimika kuhama: haki ya kubaki nyumbani bila njaa, bila vita, bila mateso, bila vurugu, bila dunia kuwa isiyokaliwa, bila rushwa kuiba mkate kutoka kwa maskini, bila silaha kuharibu mustakabali wa watoto. Hatuwezi kuzoea kuhesabu wafu. Utu wa binadamu hauna pasipoti, wala haupotezi thamani unapovuka mpaka. Mungu ambaye "katika machweo ya maisha atatuhukumu kwa upendo" (tazama Mtakatifu Yohane wa Msalaba, Ushauri na Sentensi, 57) atujalie kumtambua leo katika maskini na wageni, na atuachilie mbali na kutazama maumivu ya wengine kana kwamba hayakuwa yetu.

Papa akitupa maua baharini
Papa akitupa maua baharini   (@Vatican Media)

Papa wakabidhi kwa Mama Yetu wa Mlima Karmeli.

Mama Yetu wa Mlima Karmeli awasindikize wale waliofika, awafariji wale waliopoteza wapendwa, awaunge mkono wale wanaowakaribisha, na kuamsha ndani yetu sote ujasiri wa rehema. Na historia isitushtaki kwa kubadilisha maumivu ya wale wanaoteseka kuwa kitu kinachojulikana kwenye pwani zetu. Kwa sababu leo, hapa, kwenye ufuo wa bahari, kila uhai mpya unaokuja hutuuliza ni nini kimebaki katika ubinadamu wetu. Mapema au baadaye, tutajua kama tumeweza kuhifadhi ubinadamu huu au kama tumeruhusu kutojali kutusemea. Asante sana. Mara baada hotuba  Baba Mtakatifu alipewa zawadi, na pia kutupa shada la mauwa kwa ajili ya heshima ya waliokufa baharini. Ilifuatia Neno la Mungu na hatimaye kuhitimisha kwa sala na Baraka.

Chini ya mama wa Mlima Karmeli
Chini ya mama wa Mlima Karmeli   (@Vatican Media)
Mkutano na wahamiaji katika Kisiwa cha Kanari
11 Juni 2026, 13:40