Barcelona,Pad.F.John Mlelwa:'Ziara ya Papa inatutia moyo kwa ajili ya hudumu ya kichungaji'
Na Sr. Christine Masivo,CPS,Paul Samasumo na Angella Rwezaula–Vatican.
Katika siku yake ya tano ya ziara yake ya kitume nchini Hispania tarehe 10 Juni 2026 alasiri, Baba Mtakatifu Leo XIV alitembelea Kanisa la Mtakatifu Agostino, linalojulikana sana kama "Kanisa Kuu la Maskini," katika kitongoji cha wafanyakazi cha El Raval, katikati ya Ciutat Vella, mji wa zamani wa Barcelona. Baba Mtakatifu alikutana na mashirika ya upendo na ustawi ya Jimbo Kuu hilo ambapo alisikiliza ushuhuda wa wafanyakazi watatu.
Kabla ya Mkutano huo, vyombo vya Habari vya Vatican, vilifanya mahojiano na Paroko wa Parokia hiyo, ambaye ni Padre Faustine John Mlelwa, anatoka Tanzania, Parokia ya Mavanga, Jimbo Katoliki la Njombe. Yeye ni miongoni mwa mapadre wa Shirika la Mtakatifu Agostino wanaotoa huduma ya kichungaji katika Parokia hiyo, na amekuwa katika huduma ya upadre kwa takribani miaka thelathini tangu upadrisho wake mwaka 1996.
Akielezea historia yake, alibainisha kuwa baada ya kufanya utume wake nchini Tanzania alihudumu kama misionari nchini Peru, kwa miaka saba na baadaye alihamishiwa Barcelona, Hispania, katika mchakato wa kubadilishana mapadre kati ya majimbo kutokana na changamoto za upatikanaji wa mapadre wazawa, hasa kwa kazi za kichungaji katika mazingira ya mijini na jamii mchanganyiko.
Huduma kwa Wakimbizi na Jamii ya Wahamiaji
Akiwa Barcelona, Padre Mlelwa alisimulia jinsi alivyoanza kama Paroko msaidizi kabla ya kuteuliwa kuwa Paroko wa Parokia yake ya sasa, na ambapo amehudumu kwa takribani miaka minne. Huduma yake huko Barcelona alisema, “inalenga zaidi wakimbizi na wahamiaji kutoka maeneo mbalimbali duniani. Jumuiya anayohudumia inajumuisha watu kutoka Amerika Kusini kama vile: Peru, Bolivia, Paraguay na Ecuador, pamoja na wengine kutoka Afrika Kaskazini na Asia, hasa Pakistan na Ufilipino.”
Parokia yake inafanya kazi kwa kushirikiana na mashirika ya kidini na kijamii, likiwemo miongoni mwa hayo Shirika la Masista wa Upendo la Mtakatifu Teresa wa Kalkuta ambao wanapika na kugawa chakula kwa mamia ya watu kila siku. Padre alisimulia kwamba “kila Jumatano, Parokia hupanga ugawaji wa chakula kwa wahitaji kupitia mfumo wa msaada wa moja kwa moja. Huduma hii inalenga kuhakikisha kwamba hakuna mtu anayebaki bila chakula, bila kujali dini au asili yake.” Kanisa linasisitiza utoaji wa huduma bila ubaguzi, likiwahudumia Wakristo, Waislamu na watu wote wasio na imani sawa.
Changamoto na Matarajio ya Kijamii na Kikanisa
Padre Faustine kadhalia alieleza kuwa “mazingira ya kazi Barcelona yana changamoto kubwa, ikiwemo hali ngumu ya maisha ya wakimbizi, usalama mdogo maeneo fulani, na changamoto za kijamii kama matumizi ya dawa za kulevya na ukosefu wa makazi.” Hata hivyo, alisisitiza kuwa utume wake “ni wa utii na huduma, bila kujali mazingira.”
Akiendelea kufafanua zaidi alieleza pia matumaini makubwa ya ziara ya Baba Mtakatifu katika eneo hilo, ambayo inalenga kuhamasisha wahudumu wa kijamii na kuwatia moyo “kuendelea na huduma kwa wahitaji. Ni Matarajio ya Padre Mlelwa kwamba “Ziara hiyo inatarajiwa kuonesha mshikamano wa Kanisa na watu maskini na wakimbizi, na kuimarisha wito wa huruma na upendo katika jamii ya Barcelona na Kanisa kwa ujumla.”
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here
