Tafuta

Baba Mtakatifu Leo XIV, Ijumaa tarehe 8 Mei 2026 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Pompei Baba Mtakatifu Leo XIV, Ijumaa tarehe 8 Mei 2026 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Pompei  (@Vatican Media)

Hija ya Kichungaji Pompei na Napoli: Ibada ya Misa Takatifu

Tarehe 8 Mei 2025 Papa Leo XIV alipokabidhiwa dhamana ya: Kuongoza, Kufundisha na Kuwatakatifuza watu wa Mungu; Siku ya Sala maalum kwa ajili ya Bikira Maria wa Pompei. Kumbe, hija hii ya kitume inapania pamoja na mambo mengine, kuiweka huduma na utume unaotekelezwa naye kama Khalifa wa Mtakatifu Petro chini ya ulinzi na tunza ya Bikira Maria wa Pompei na kwamba, katika maisha na utume wake, anaendelea kufuata nyayo za Papa Leo XIII.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Utenzi wa Bikira Maria, ni mtazamo mpya kuhusu Mwenyezi Mungu na ulimwengu. Ni utenzi wa toba na wongofu wa ndani unaowahimiza waamini kujenga na kudumisha utamaduni unaomwilisha huruma na upendo wa Mungu katika uhalisia wa maisha. Utenzi wa “Magnificat” una mwelekea Mwenyezi Mungu, ambaye ni mkuu, mwingi wa huruma na mapendo, mtakatifu na enzi zote ni zake na kwamba, huruma yake kwa watu wanaomcha hudumu kizazi hata kizazi. Baba Mtakatifu Leo XIV Ijumaa tarehe 8 Mei 2026 katika Ibada ya Misa takatifu kwenye Uwanja wa Madhabahu ya Bikira Maria wa Pompei amesema, Utenzi wa Bikira Maria, “Magnificat”; Wimbo wa Zakaria “Benedictus” pamoja na wimbo wa Mzee Simeoni “Nunc Dimitis” ni nyimbo na tenzi ambazo zinaboresha Sala ya Kanisa pamoja na kumwangalia binadamu katika mchakato wa ukombozi wake. Msingi wa ujenzi wa Madhabahu ya Bikira Maria wa Pompei uliwekwa takribani miaka 150 iliyopita, baada ya miaka 79 tangu alipozikwa Mtakatifu Bartolo Longo, Muasisi mwenza wa Madhabahu haya, kielelezo cha Mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu.

Ibada ya Misa takatifu kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Pompei
Ibada ya Misa takatifu kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Pompei   (@Vatican Media)

 

Mtakatifu Yohane Paulo II tarehe 7 Oktoba 2003 alizindua Mwaka wa Rozari Takatifu uliokita mizizi yake katika mchakato wa Uinjilishaji mpya, unaosimikwa katika ushuhuda wenye mvuto na mashiko changamoto na mwaliko kwa watu wa Mungu kumtangaza na kumshuhudia Kristo Yesu aliyeteswa, akafa na kufufuka kwa wafu; na kuendelea kumwilisha katika uhalisia wa maisha tunu msingi za Kiinjili, kwa watu wanaopoteza hata kumbukumbu za amana na utajiri wa maisha ya kiroho! Ilikuwa ni tarehe 8 Mei 2025 Baba Mtakatifu Leo XIV alipokabidhiwa dhamana ya: Kuongoza, Kufundisha na Kuwatakatifuza watu wa Mungu kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, Siku ya Sala maalum kwa ajili ya Bikira Maria wa Pompei. Kumbe, hija hii ya kitume inapania pamoja na mambo mengine, kuiweka huduma na utume wa kichungaji unaotekelezwa naye kama Khalifa wa Mtakatifu Petro chini ya ulinzi na tunza ya Bikira Maria wa Pompei na kwamba, katika maisha na utume wake, anaendelea kufuata nyayo za Papa Leo XIII, ambaye pamoja na mambo mengine, ni Kiongozi wa Kanisa aliyejibidiisha kuweka msingi wa Mamlaka fundishi ya Kanisa yaani “Magisterium” kuhusu Rozari Takatifu pamoja na yeye mwenyewe kumtangaza Mwenyeheri Bartolo Longo, Mtume wa Rozari Takatifu kuwa ni Mtakatifu.

Ekaristi Takatifu ni chacho na kilele cha maisha na utume wa Kanisa
Ekaristi Takatifu ni chacho na kilele cha maisha na utume wa Kanisa   (@Vatican Media)

Salam ya Malaika Gabrieli kwa Bikira Maria, ulikuwa ni mwaliko wa furaha na faraja kutoka kwa Mwenyezi Mungu; Ufunuo wa upendo na huruma ya Mungu kwa njia ya Kristo Yesu, ili kuwawezesha watu wote kuweza kuunganika na Bikira Maria “Mama kweli wa viungo vya Fumbo la mwili wa Kristo yaani Kanisa, ili waweze kushiriki katika imani na katika mapendo. Na ukubali wa Bikira Maria unakuwa ni mwanzo wa kuzaliwa kwa Kristo Yesu, na hivyo Bikira Maria anakuwa ni “Theotokos” yaani “Mama wa Mungu” na Kanisa kwa njia ya Roho Mtakatifu, mwanzo wa Sala na Takatifu ya Rozari Takatifu, inayokita mizizi yake katika historia ya ukombozi. Hii ni Sala ambayo inawawezesha waamini: Kumwabudu, Kumtafakari na hatimaye, waamini wanaweza kumwilisha Rozari hii katika uhalisia wa maisha yao: “Nimesulibiwa pamoja na Kristo; lakini ni hai; wala si mimi tena, bali Kristo yu hai ndani yangu; na uhai nilio nao sasa katika mwili, ninao katika imani ya Mwana wa Mungu, ambaye alinipenda, akajitoa nafsi yake kwa ajili yangu.”

Mashuhuda wa Kristo Yesu aliyeteswa, akafa na kufufuka kwa wafu
Mashuhuda wa Kristo Yesu aliyeteswa, akafa na kufufuka kwa wafu   (@Vatican Media)

 

Madhabahu ya Bikira Maria wa Pompei ni mahali ambapo sadaka ya Ekaristi Takatifu, chemchemi na kilele cha maisha yote ya kikristo inaadhimishwa na kwamba, Ekaristi Takatifu ni Rozari hai na kwamba, Mafumbo yote ya Rozari Takatifu yanapata mwanga wake kutoka katika maadhimisho ya Ekaristi Takatifu; kumbu kumbu hai ya mateso, kifo na ufufuko wa Kristo Yesu kutoka kwa wafu. Hii ni Sakramenti ya Sadaka: Shukrani, Kumbukumbu na Uwamo na kwamba, kiini cha mafundisho ya Kanisa kumhusu Kristo Yesu na Fumbo la Ekaristi Takatifu. Baba Mtakatifu Leo XIV anasema, kabla ya Kristo Yesu kupaa kwenda mbinguni na Roho Mtakatifu kuwashukia Mitume, ilikuwa ni fursa ya kutafakari kwa kina maisha na utume wa Kristo Yesu na huo ukawa ni mwanzo wa maadhimisho ya Mwaka wa Liturujia wa Kanisa na kwamba, Rozari Takatifu inatoa muhtasari wa maisha na utume wa Kristo Yesu kama sehemu ya kazi ya ukombozi.

Ibada ya Misa Takatifu ni kilele cha maisha na utume wa Kanisa
Ibada ya Misa Takatifu ni kilele cha maisha na utume wa Kanisa

Baba Mtakatifu Leo XIV anawataka waamini kusali na kutafakari matendo ya Rozari Takatifu na wala wasiisali kama “Kasuku.” Waamini watambue kwamba, Rozari Takatifu inachota amana na utajiri wake kutoka katika: Maandiko Matakatifu, Maisha ya Kristo Yesu na Tafakari ya kina. Waamini wanaposali Rozari Takatifu wanakuza ndani mwao: Ukweli na upendo kwa Mungu na jirani zao unaomwilishwa katika huduma ya upendo kwa maskini na wahitaji zaidi. Huu ni mwaliko kwa kusali kwa ajili ya kuombea: familia, haki na amani inayopata chimbuko lake kutoka katika sakafu ya moyo wa mwanadamu. Ni katika muktadha huu, Mtakatifu Yohane Paulo II kunako mwaka 1986 aliwaalika viongozi wote wa Jumuiya ya Kimataifa kusali kwa ajili ya kuombea amani duniani, kama alivyofanya pia Hayati Baba Mtakatifu Francisko na kama anavyofanya sasa Papa Leo XIV. Waamini wasikubali hata kidogo kumezwa na utamaduni wa kifo. Madhabahu ya Bikira Maria wa Popei pawe ni mahali pa sala kwa ajili ya kuombea: haki na amani duniani na kwamba, waamini wanapaswa kusali kwa imani na matumaini. Mtakatifu Bartolo Longo mintarafu imani kwa Bikira Maria alimwita kuwa ni mwenye uwezo wote kwa neema. Kwa maombezi yake, Mungu wa amani amimine wingi wa rehema, yenye kugusa mioyo, kutuliza chuki na uhasama kwa kuwaangazia viongozi wa Serikali ili kutekeleza vyema nyajibu zao.

Papa Leo XIV Kumbukizi ya Mwaka mmoja kama Khalifa wa Mt. Petro
Papa Leo XIV Kumbukizi ya Mwaka mmoja kama Khalifa wa Mt. Petro   (@VATICAN MEDIA)

Kwa upande wake, Askofu mkuu Tommaso Caputo, Mwakilishi wa Kitume kwa ajili ya Madhabahu ya Bikira Maria wa Pompei, mara baada ya Misa Takatifu amemshukuru Baba Mtakatifu Leo XIV kwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Madhabahu ya Bikira maria, Hekalu la Imani na Upendo na Ngome ya Amani, mahali ambapo waamini wanasali na kutafakari Uso wa Kristo Yesu kupitia kwa Bikira Maria, watu wa Mungu wanaweza kuhudumiwa katika umaskini na unyonge wao. Hii imekuwa ni fursa kwa Baba Mtakatifu kuwaimarisha watu wa Mungu katika imani, matumaini na mapendo na hivyo kuendelea kumkimbilia Bikira Maria ili aweze kuwaonesha: Njia ya udugu wa kibinadamu, majadiliano na amani. Hii ni hija ya kichungaji, kumbukizi ya miaka 150 iliyopita, mwaliko kwa watu wa Mungu kuwa na imani na Khalifa wa Mtakatifu Petro pamoja na Kanisa.

Ibada ya Misa Takatifu
08 Mei 2026, 16:03