Papa Leo XIV,Angola:Mambo muhimu,Aprili 19,kusali Rozari na Misa
Na Angella Rwezaula - Vatican.
Ni takriban kilomita 130 kutoka mji Mkuu Luanda nchini, kwenye kingo za Mto Kwanza, mkubwa zaidi nchini Angola, ambao una mimea mingi kwenye kingo zote mbili, na kwa karne nyingi Bikira amekuwa Mamã Muxima, maana yake Moyo wa Mama, kama anavyoitwa katika lugha ya Kimbundu. Ni eneo la Kihistoria ambalo lilikuwa ni sehemu ya wakoloni wa Ureno walipopanga watu kama bidhaa, kwa kuwauza na kuwapeleka utumwani nchini Brazil.
Kila mwaka panaheshimika mahali hapo patakatifu, pa karne ya 17 penye sanamu ya kale ya Bikira Maria Mkingiwa dhambi ya Asili. Madhabahu hiyo ilitangazwa kuwa kituo cha hija kitaifa kunako 1924, na ndiyo madhabahu inayopendwa zaidi na watu wengi nchini Angola. Maelfu ya Mahujaji humiminika kwa wingi kutoka nchini kote Angola, wakitafuta neema, uponyaji, upatanisho wa kifamilia, amani ya ndani, na ulinzi kutokana na hatari za maisha. Ni eneno kwa hiyo la kumkabidhi Mama Maria wasiwasi na huzuni zao, furaha na matumaini yao.
Kwa kawaida na kama mtindo karibu wa kiafrika, wanapofika hapo wengine hukaa hata siku nyingi karibu na Moyo wa Mama, wakipiga kambi karibu na kuvumilia hata magumu kama ishara ya upendo wao kwake. Na ndiyo ilikuwa wakati wanamsubiri Papa ambapo walikesha kwa sala na kupiga kambi.
Kwa njia hiyo, katika fursa ya Ziara ya Baba Mtakatifu Leo XIV nchini Angola imekuwa tena furaha kubwa Dominika tarehe 19 Aprili 2026 kushiriki kama mhujaji kwenye sala ya Rozari Takatifu na waamini wapatao takribani 30,000 huko Muxima, katika Jimbo Katoliki la Viana, ili kumwomba Maria.
Kabla ya kufika Baba Mtakatifu Waamini walimsubiri Papa kwa hamu kubwa na maandalizi mazuri.
