Papa Leo XIV apongeza Mfuko wa “Weltkirche-Weltmission"kwa huduma yake!
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV alikutana wanachama wa Mfuko wa Weltkirche-Weltmission, inayojulikana kama Ofisi ya la Kanisa la Ulimwengu na Mazungumzo, iliyoanzishwa miaka 50 iliyopita katika Jimbo Kuu la Cologne nchini Ujerumani na kutoa maneno ya shukrani, kwa lugha ya Kiingereza, mbele watu hao tarehe 30 Aprili 2026, mjini Vatican. Papa Leo XIV alisema kuwa ziara yao, imejikita katika kipindi cha Pasaka, wakati Kanisa lote linafurahi katika Ufufuko wa Bwana na kufufua tumaini lake katika maisha mapya yaliyozaliwa na Fumbo la Pasaka.
Tafakari juu ya Ulimwengu wa Kanisa
Hii ni fursa inayofaa ya kutafakari juu ya ulimwengu wa Kanisa na umuhimu wa mazungumzo. Kwa kuzingatia Ufufuko wa Kristo, Kanisa linajitambua kama limetumwa kwa watu wote, halijilazimishi, bali likishuhudia ukweli katika upendo. Mazungumzo, kwa upande wake, huimarisha ushirika, hufungua njia za uelewa, na hutumikia sababu ya amani. Kwa njia hiyo, Kristo huvuta vitu vyote kwake na kulifanya Kanisa kuwa ishara ya umoja na matumaini kwa ulimwengu.
Papa alisema kuwa vipengele hivi vimejikita sana katika historia ya Jimbo Kuu, ambalo limeonyesha uwazi wa kinabii katika mwelekeo wa Ulimwengu wa Kanisa, unaooneshwa kupitia nia ya kukutana, kubadilishana, na mazungumzo kati ya watu na tamaduni. Chini ya uongozi wa Kardinali Josef Frings na Askofu Mkuu Josef Teush, Jimbo Kuu la Cologne lilianzisha ushirikiano na Jimbo Kuu la Tokyo mnamo 1954, la kwanza na la aina yake nchini Ujerumani. Pia walikuwa waanzilishi katika kuanzisha mipango muhimu ya misaada kama vile Misereor na Adveniat, hivyo kuweka msingi wa kuanzishwa kwa Weltkirche-Weltkirche-Weltmission mnamo 1976.
Maono ya Kanisa yawe zaidi ya mipaka ya Ulaya
Maono haya ya Kanisa kama la ulimwengu wote, Papa Leo alisema “limeitwa kuwa na mshikamano zaidi ya mipaka ya Ulaya na kudumishwa kupitia utamaduni wa mazungumzo” ambapo “linaendelea kuwa msingi wa utambulisho wa shirika lao.” Likisukumwa na roho hiyo, Baba Mtakatifu alisema kuwa, “Jimbo Kuu la Cologne likawa mwanachama mwanzilishi wa Muungano wa Mashirika ya Misaada kwa Makanisa ya Mashariki (ROACO) na, kwa miaka mingi, limetoa msaada kwa maeneo yaliyoathiriwa na njaa, mafuriko, vita, na migogoro mingine.” Kwa hiyo “ Jimbo Kuu pia linadumisha uhusiano wa usaidizi na makanisa mengine katika nchi zaidi ya mia moja, likizingatia hasa Mashariki ya Kati na Makanisa ya Mashariki.
Pia linatoa ufadhili wa masomo kwa ajili ya malezi ya kipadre na usaidizi kwa makuhani wazee.” Kabla ya urithi huu tajiri, Papa alipenda kutoa shukrani za dhati kwa mipango mingi ambayo wanaendelea kushiriki. “Kupitia huduma yenu ya ukarimu, mwelekeo wa Kanisa kwa wote unaonekana na kuwa thabiti, ukikuza mshikamano, ukiimarisha vifungo vya umoja, na kutoa ushuhuda wa Injili ya amani katika ulimwengu ambao mara nyingi hujulikana kwa mgawanyiko na mateso. Ushuhuda huu unahitajika leo zaidi ya hapo awali.”
Kuendelea kuunga mkono wa uwepo wa Wakristo wa Mashariki ya Kati
Papa Leo XIV kadhalika alisema kuwa, “Kaka na dada zetu Wakristo wengi wamelazimika kuondoka katika nchi zao kwa sababu ya vita, vurugu, na umaskini, na wengi wanategemea moja kwa moja kujitolea na wema wenu kwa ajili ya kuishi kwao. Kwa hivyo, ninawahimiza kuendelea katika utume huu wa upendo, ili waweze kuendelea kuhisi ukaribu wa Kanisa la ulimwengu wote.” Kwa njia maalum, Papa Leo XIV aliongeza kusema “ninawaomba muendelee kuunga mkono uwepo wa Wakristo katika Mashariki ya Kati, ili kuhakikisha kwamba tamaduni zinazoheshimika za Makanisa ya Mashariki zinahifadhiwa, zinalindwa, na zinajulikana zaidi.” Kwa hisia hizo, “ninaomba kwamba siku hizi za mapumziko, tafakari, na ufufuko jijini Roma ziwaimarishe na kuwatia moyo. Ninawakabidhi ninyi na wapendwa wenu ulinzi wa kimama wa Maria, Mama wa Mungu na Mama wa Kanisa. Kama ahadi ya ukaribu wangu, kwa hiari yangu ninatoa Baraka yangu ya Kitume.”
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here
