Papa Leo XIV aliacha Cameroon na kufika Angola
Vatican News
Hafla ya kuaga Cameroon kwa namna ya kiafrika na Papa Leo XIV alipanda ndege ya "ITA Airbus A330-900neo" iliyomfikisha Angola, katika awamu ya tatu ya Ziara yake ya kitume.
Ndege iliyokuwa imembeba Papa na msafara wake iliondoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Yaoundé-Nsimalen saa 6:47 mchana kwa saa za huko.
Ndege ilitua Luanda saa 8:45 alasiri kwa saa za huko baada ya safari ya takriban saa mbili na nusu.
Muda mfupi kabla ya hafla ya kuaga katika uwanja wa ndege wa Cameroon, Papa Leo XIV, aliwasili baada ya Misa kumalizika iliyoadhimishwa katika Uwanja wa Ndege wa Yaoundé-Ville, alikutana na Rais Paul Biya katika chumba kidogo karibu na uwanja wa ndege. Yeye na Waziri Mkuu wa Cameroon, Joseph Dion Ngute, walisikiliza wimbo wa taifa ukiimbwa nje, wakisindikizwa na Walinzi wa Heshima.
Wote wawili kisha walifika chini ya ndege wakitembea kwenye zulia refu jekundu, wakiwasalimia mamlaka mbalimbali za kitaasisi na za kikanisa zilizokuwepo.
Katika maadhimisho kwa heshima Bikira Maria, Malkia wa Mitume, iliyohudhuriwa na waamini wapatao 200,000, Papa Leo XIV aliwahimiza watu wa Cameroon kubaki imara katika Kristo ili wawe "chumvi na nuru ya nchi hii!"
Telegramu za Ndani ya Ndege
Katika telegramu iliyotumwa kwa Rais wa Cameroon Biya, Papa alitoa shukrani zake kubwa "kwa msaada na ishara nyingi za udugu nilizooneshwa katika siku za hivi karibuni."
"Ninapoanza safari yangu ya kitume hadi Jamhuri ya Angola," aliongeza, "Ninaomba kwa moyo wote baraka za kimungu za amani na hekima kwa nchi yako."
Akimwandikia Rais wa Jamhuri ya Guinea ya Ikweta, Teodoro Obiang Nguema Mbasogo, Papa Leo XIV aliwahakikishia maombi yake "kwa kutarajia kwa furaha, ya ziara yangu iliyo karibu nchini mwako."
Papa alimwomba Mungu aipatie "ustawi na mshikamano wa kidugu" Gabon katika ujumbe wake kwa Rais Brice Clotaire Oligui Nguema.
Kwa Rais wa Jamhuri ya Congo Brazzaville, Denis Sassou-N'Guesso, Papa alimhakikishia maombi yake kwamba, "taifa libarikiwe na udugu na amani."
Ratiba ya Angola
Papa Leo XIV atakuwa Angola hadi Jumanne, Aprili 21, kabla ya kuhitimisha safari yake ya tatu ya kitume kwenda Guinea ya Ikweta. Kauli mbiu ya ziara hiyo ni: "Papa Leo XIV, mwanahija wa matumaini, upatanisho, na amani, aibariki Angola," huku nembo hiyo ikionesha marejeo ya bendera ya taifa ya nchi hiyo ya Kusini mwa Afrika, ikiwa na gurudumu la koni, mfano wa kazi, na petali zinazoashiria mulemba, mti wa mfano wa nchi hiyo.
Papa ana matukio mengi mbele yake, kuanzia alasiri mara tu alipofikia alianzia na ziara ya heshima kwa Rais João Manuel Gonçalves Lourenço ambaye alimpokea katika uwanja wa ndege. Hii ilifuatiwa na mkutano katika Banda la Itifaki na mamlaka ya kisiasa na kidini, viongozi wa biashara, na wawakilishi wa asasi za kiraia na utamaduni.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwenye jarida letu la kila siku. Just click here
