Papa Leo XIV:njia za kuelekea amani lazima zifunguliwe Mashariki ya Kati
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV. mara baada ya Misa Takatifu, na kabla ya Sala ya Malaika wa Bwana katika Dominika ya Matawi tarehe 29 Machi 2026, katika Uwanja wa Mtakatifu Petro mjini Vatican, uliojaa waamini kutoka pande zote za Dunia, alianza kusema kuwa "Mwanzoni mwa Juma Takatifu, tuko karibu zaidi na Wakristo wa Mashariki ya Kati katika maombi, ambao wanateseka kutokana na matokeo ya mgogoro mbaya na katika visa vingi hawawezi kupata uzoefu kamili wa ibada za siku hizi takatifu.”
Hatuwezi kuwasahau wanaoshiriki mateso
Papa alisema kuwa “Hata Kanisa linapotafakari fumbo la Mateso ya Bwana, hatuwezi kuwasahau wale ambao leo wanashiriki kweli katika mateso yake. Jaribio lao linapinga dhamiri ya wote. Tunamwomba Mfalme wa Amani awasaidie watu waliojeruhiwa na vita na njia zilizo wazi za upatanisho na amani.
Papa awakabidhi kwa Bwana wahanga wa vita
Baba Mtakatifu Leo XIV aidha alisema “Pia nataka kuwakabidhi kwa Bwana mabaharia ambao ni wahanga wa vita. Ninawaombea marehemu, waliojeruhiwa, na familia zao. Dunia, anga, na bahari vimeumbwa kwa ajili ya uzima na amani. Na tunawaombea wahamiaji wote waliokufa baharini, hasa wale waliopoteza maisha yao katika siku za hivi karibuni nje ya kisiwa cha Crete,” huko Ugiriki.
Salamu kwa mahujaji wote na sala kwa Mama Maria
Papa alipenda pia kuwasalimia na kuwashukuru wote, kuanzia na warumi, mahujaji ambao wameshiriki katika sherehe hiyo. Kwa pamoja”, kuwaomba kumgeukia Bikira Maria, huku “tukimkabidhi maombi yetu yote kwa maombezi yake.” Papa aliongeza kusema “Hebu tujiruhusu kuongozwa naye katika siku hizi takatifu ili kumfuata Yesu, Mwokozi wetu, kwa imani na upendo.”
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata taarifa mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku:Just click here.
