Papa Leo XIV:Mungu anatufanya watoto tuwe kama Yeye katika ubinadamu wetu dhaifu
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Ikiwa urafiki unaweza kuisha kwa sababu ya kitendo fulani kikubwa cha kuvunjika au kupuuzwa kila siku ambacho huharibu uhusiano hadi kufikia hatua ya uharibifu, basi kudumisha urafiki na Mungu kunahitaji kujitolea. Na Ikiwa Yesu anatuita kuwa marafiki, tusipuuze wito huu. Tuupokee, tuutunze uhusiano huu, na tutagundua kwamba urafiki na Mungu ndio wokovu wetu. Ni wito mzito wa Baba Mtakatifu Leo XIV, wakati wa Katekesi yake kwa waamini na mahujaji waliokusanyika katika Ukumbi wa Paulo VI, mjini Vatican, tarehe 14 Januari 2026 ambapo Baba Mtakatifu aliendeleza tafakari yake kuhusu Mwendelezo wa Katiba ya Mtaguso II wa Vatican ya Dei Verbum.
Papa akianza alisema “Wapendwa Kaka na dada habari za asubuhi na karibuni! Tumeanza mfululizo wa Katekesi kuhusu Mtaguso wa Pili wa Vatican. Leo hii tunaanza kuchunguza kwa undani zaidi Katiba ya Kidogmatic ‘Dei Verbum’ kuhusu Ufunuo wa Kimungu. Ni mojawapo ya hati nzuri na muhimu zaidi za Mtaguso, na ili kuanza, tunaweza kuona ni muhimu kukumbuka maneno ya Yesu: "Siwaiti tena watumwa, kwa maana mtumwa hajui afanyalo Bwana wake; lakini nimewaita ninyi rafiki, kwa maana yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewajulisha" (Yh 15:15).
Baba Mtakatifu Leo XIV alisisitiza kuwa, hili ni jambo la msingi la imani ya Kikristo, ambalo Dei Verbum inatukumbusha, kwamba: Yesu Kristo anabadilisha uhusiano wa mwanadamu na Mungu kwa kiasi kikubwa; kuanzia sasa, itakuwa uhusiano wa urafiki. Kwa hivyo, sharti la kipekee la Agano jipya ni Upendo. Mtakatifu Agostino katika kutoa maoni yake kuhusu kifungu hiki kutoka Injili ya Nne, alisisitiza juu ya mtazamo wa neema, ambao pekee unaweza kutufanya kuwa marafiki wa Mungu kupitia Mwanawe. Hakika, kauli mbiu ya kale ilisema: "Amicitia aut pares invenit, aut facit," yaani "Urafiki huibuka kati ya walio sawa au huwafanya wawe sawa."
Papa alibainisha tena kwamba sisi si sawa na Mungu, lakini Mungu Mwenyewe hutufanya tufanane Naye katika Mwanawe. Kwa sababu hiyo, kama tunavyoweza kuona katika Maandiko, katika Agano kuna wakati wa awali wa umbali, kwani makubaliano kati ya Mungu na wanadamu daima hubaki bila ulinganifu: Mungu ni Mungu na sisi ni viumbe; lakini, kwa kuja kwa Mwana katika mwili wa kibinadamu, Agano linafunguka kwa lengo lake kuu: katika Yesu, Mungu hutufanya watoto na anatuita tuwe kama Yeye katika ubinadamu wetu dhaifu.
Kwa hivyo, Papa alisistiza kwamba kufanana kwetu na Mungu hakufikiwi kupitia uasi na dhambi, kama nyoka alivyopendekeza kwa Eva (taz. Mw 3:5), bali katika uhusiano na Mwana aliyemfanya mwanadamu. Maneno ya Bwana Yesu ambayo tumeyakumbuka: “Nimewaita marafiki” yanachukuliwa tena hasa katika Katiba ya Dei Verbum, ambayo inasema: “Kwa Ufunuo huu, kiukweli, Mungu asiyeonekana (taz. Kol 1:15; 1 Tim 1:17) kutokana na wingi wa upendo wake huzungumza na watu kama marafiki (taz. Kut 33:11; Yh 15:14-15) na anaishi kati yao (taz. Bar 3:38), ili kuwaalika na kuwapokea katika ushirika naye”(n. 2).
Mungu katika Kitabu cha Mwanzo tayari alishiriki katika mazungumzo na wazazi wetu wa kwanza (rej. Dei Verbum,3); na mazungumzo haya yalipoingiliwa na dhambi, Muumba hakuacha kutafuta kukutana na viumbe vyake na kuanzisha agano nao mara kwa mara. Katika Ufunuo wa Kikristo, wakati Mungu, akitutafuta, alipokuwa mwili katika Mwanawe, mazungumzo yaliyoingiliwa yanarejeshwa kabisa: Agano ni jipya na la milele; hakuna kinachoweza kututenganisha na upendo wake. Kwa hivyo, Ufunuo wa Mungu una tabia ya mazungumzo ya urafiki na, kama inavyotokea katika uzoefu wa urafiki wa kibinadamu, hauvumilii ukimya, lakini unalishwa na kubadilishana maneno ya kweli.
Katiba ya Dei Verbum pia inatukumbusha hili: Mungu huzungumza nasi. Ni muhimu kuelewa tofauti kati ya maneno na mazungumzo: ya mwisho hubaki ya juu juu na hushindwa kuunda ushirika kati ya watu, ilhali katika mahusiano ya kweli, maneno hayatumiki tu kubadilishana taarifa na habari, bali pia kufichua sisi ni nani. Maneno yana mwelekeo wa ufunuo unaounda uhusiano na wengine. Hivyo, kwa kuzungumza nasi, Mungu hujifunua kama Mshirika anayetualika kuwa marafiki naye. Kwa mtazamo huu, mtazamo wa kwanza wa kukuza ni kusikiliza, ili Neno la Mungu liweze kupenya akili na mioyo yetu; wakati huo huo, tumeitwa kuzungumza na Mungu, si kumwambia kile ambacho tayari anajua, bali kujifunua kwetu wenyewe. Kwa hivyo kuna hitaji la maombi, ambapo tumeitwa kuishi na kukuza urafiki na Bwana.
Hili linafanikiwa hasa katika sala ya kiliturujia na ya pamoja, ambapo hatuamui cha kusikiliza kutoka kwa Neno la Mungu, bali Yeye mwenyewe huzungumza nasi kupitia Kanisa. Zaidi ya hayo, linatimizwa katika sala ya kibinafsi, ambayo hufanyika ndani ya moyo na akili. Siku na Juma ya Mkristo lazima lijumuishe muda uliotengwa kwa maombi, na kutafakari kwa kina. Ni wakati tu tunapozungumza na Mungu ndipo tunaweza pia kuzungumza kumhusu. Uzoefu wetu unatuambia kwamba urafiki unaweza kuisha kwa sababu ya kitendo fulani kikubwa cha kuvunjika, au kwa sababu ya mfululizo wa mambo ya kila siku ambayo huharibu uhusiano hadi upotee. Yesu akituita kuwa marafiki, hebu tujaribu kutouacha wito huu usisikilizwe. Tuupokee, tuutunze uhusiano huu, na tutagundua kwamba urafiki na Mungu ndio wokovu wetu.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here.
