Papa Leo XIV:Tuombe amani na urafiki kati ya watu na isiyo silaha!
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV aliongoza tafakari kabla ya Sala ya Malaika wa Bwana ikiwa ni ya kwanza kwa Mwaka mpya 2026 kwa waamini takriban 40,000 waliokusanyika katika Uwanja wa Mtakatifu Petro mjini Vatican, Januari Mosi, kwa ajili ya sala hiyo. Ikiwa ni Sherehe ya Bikira Maria Mama wa Mungu ni sanjari na Siku ya 59 ya Amani Duniani. Papa alianza kusema, “Kadri mdundo wa miezi unavyojirudia, Bwana anatualika tupyaishe wakati wetu, hatimaye tukianzisha enzi ya amani na urafiki miongoni mwa watu wote. Bila hamu hii ya mema, haingekuwa na maana kugeuza kurasa za kalenda na kujaza shajara zetu. Jubilei, ambayo inakaribia kumalizika, imetufundisha jinsi ya kukuza tumaini la ulimwengu mpya: kwa kugeuza mioyo yetu kwa Mungu, hivyo kubadilisha makosa kuwa msamaha, maumivu kuwa faraja, na maazimio ya wema kuwa matendo mema.
Kwa njia hiyo, kiukweli, Mungu mwenyewe anaishi katika historia na kuiokoa kutokana na usahaulifu, akiupatia ulimwengu Mkombozi: Yesu. Yeye ndiye Mwana Mzaliwa wa kwanza ambaye anakuwa ndugu yetu, akiangaza dhamiri za mapenzi mema, ili tuweze kujenga mustakabali kama nyumba ya ukarimu kwa kila mwanaume na mwanamke anayekuja kwenye nuru.
Katika suala hilo Papa alisisitiza kuwa, “siku kuu ya Noeli leo inaelekeza macho yetu kwa Maria, ambaye alikuwa wa kwanza kuhisi moyo wa Kristo ukidunda. Katika ukimya wa tumbo lake la bikira, Neno la uzima linajitangaza kama mapigo ya neema. Mungu, Muumba mwema, amejua moyo wa Mariamu na wetu wenyewe. Kwa kuwa mwanadamu, anatujulisha sisi: kwa hivyo, moyo wa Yesu unadunda kwa kila mwanaume na kila mwanamke. Kwa wale walio tayari kumkaribisha, kama wachungaji, na kwa wale wanaokataa, kama Herode. Moyo wake haujali wale ambao hawana moyo kwa jirani zao: unadunda kwa ajili ya wenye haki, ili waweze kudumu katika kujitolea kwao, na kwa ajili ya wasio haki, ili waweze kubadilisha maisha yao na kupata amani.
Mwokozi anakuja ulimwenguni, aliyezaliwa na mwanamke: hebu tusimame kuabudu tukio hili, ambalo linang'aa katika Maria Mtakatifu na linaakisiwa katika kila mtoto ambaye hajazaliwa, likifunua taswira ya kimungu iliyochorwa kwenye miili yetu. Katika Siku hii, sote tuombe pamoja kwa ajili ya amani: kwanza miongoni mwa mataifa yaliyojaa damu kutokana na migogoro na umaskini, lakini pia katika nyumba zetu, katika familia zilizojeruhiwa na vurugu na maumivu. Tukiwa tumeshawishika kwamba Kristo, tumaini letu, ndiye jua lisilofifia la haki, tunaombe kwa ujasiri maombezi ya Maria, Mama wa Mungu na Mama wa Kanisa.
Siku ya amani
Na mara baada ya sala ya Malaika wa Bwana, Papa Leo XIV aliwasalimia kwa upendo wote waliokusanyika “katika Uwanja wa Mtakatifu Petro na kwamba katika siku hii ya kwanza ya mwaka. Ninawatakia amani na baraka zote! Namshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Italia, Sergio Mattarella. Tangu tarehe 1 Januari 1968, kwa utashi wa Papa Mtakatifu Paulo VI, leo hii inaadhimishwa Siku ya Amani Duniani.” Papa aliongeza, “Katika Ujumbe wangu, nilitaka kurudia hamu ambayo Bwana alinipatia msukumo wa kutoa aliponiita kwenye huduma hii: "Amani iwe nanyi nyote!" Amani inayoondoa silaha na isiyo na silaha, inayotoka kwa Mungu, zawadi ya upendo wake usio na masharti, iliyokabidhiwa jukumu letu." Kwa Papa aliendelea kusema: “Wapendwa, kwa neema ya Kristo, tuanze leo kujenga mwaka wa amani, tukiondoa silaha mioyoni mwetu na kujiepusha na vurugu zote.”
Shukrani kwa mipango mingi ya amani
“Ninatoa shukrani zangu kwa mipango mingi isiyohesabika iliyoandaliwa katika tukio hili ulimwenguni kote. Hasa, nakumbuka Maandamano ya Kitaifa yaliyofanyika jana (Desemba 31) usiku huko Catania na nawasalimu washiriki katika moja iliyoandaliwa leo na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio. “Pia ninawasalimu kundi la wanafunzi na walimu kutoka Richland, New Jersey, na Warumi na mahujaji wote waliopo.”
Miaka 800 ya kifo cha Mtakatifu Francis wa Assisi
“Mwanzoni mwa mwaka huu, ambao unaashiria miaka mianane ya kifo cha Mtakatifu Francis, ningependa kutoa baraka zake kwa kila mtu, zilizochukuliwa kutoka katika Maandiko Matakatifu: "Bwana awabariki na kuwalinda; awaoneshe uso wake na kuwahurumia; awageuzie macho yake na kuwapa amani." Mama Mtakatifu wa Mungu atuongoze katika safari ya mwaka mpya. Ninawakatika siku kuu njema wote!”
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwenye jarida letu la kila siku. Just click here
