Papa Leo XIV,mahujaji wa Hispania:Maskini si mtu wa kusaidia tu ni uwepo wa kisakramenti wa Mungu
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV, Jumatatu tarehe 29 desemba 2025 alikutana mjini Vatican na kikundi cha wanahija kutoka Parokia ya Mtakatifu Thomás wa Villanuova, nchini Hispania. Katika hotuba yake kwa lugha ya kihispania alionesha furaha ya kukutana nao katika siku ya Oktava ya Noeli na kuwakaribisha. Kama Jumuiya ya Parokia, alisema kwamba waliweza kujiandaa kwa jitihada kubwa katika hija ya kijubilei na wakati wa mwaka huu kwa namna ya pekee kwa Kanisa ambapo walimsindikiza Mfuasi wa Mtume Petro kwa sala zao na kwa ukarimu wao. Papa aliwashukuru kwa ishara hiyo ya muungano na ukaribu.
Katika hotuba yake Papa Leo XIV kadhalika alisisitiza kuwa Parokia yao kama Msimamizi wao Mtakatifu Thomas wa Villanuova, Mtawa wa kiagostinian, wa kihispania alikuwa na wazo katika matendo ya Mungu kwa maisha yake, ambapo uwezekano wake ulipelekea kufanya mema mengi kwa Kanisa na kwa Jamii ya wakati wake. Wao wanajua vema wasifu wake na mji wa Alcalá de Henares, na mahali ambapo wanaishi, inahifadhi ishara muhimu ya hatua zake za maisha. Kwa kushukuru ushuhuda na kujikita kwao na uaminifu wa Mtakatifu Askofu huyo, Papa alipenda kushirikishana nao baadhi ya tabia zake zilizomtambulisha, ambazo zinaweza kusaidia kutafakari kwa ngazi ya kibinafsi, kifamilia na kijumuiya.
Katika maisha yake na maandishi yake, yeye alijionesha katika utafutaji bila kuchoka wa sala inayoendelea, yaani kusema kuwa wasiwasi mtakatifu kwa kuwa na uwepo wa Mungu kila wakati. Hii ina maana ya ndani kabisa na kujitoa ili kusikiliza na kumwacha Bwana atende. Zaidi ya maisha yake ya Kiroho, Mtakatifu Thomas wa Villanuova anajipambanua kwa ajili ya kujishughulisha. Mantiki hii, katika ulimwengu ambao unatafikiri unatoa kwetu yote kwa namna ya haraka zaidi na rahisi, inatuuliza maswali. Utulivu na urahisi wake, kujitolea kwake kufanya kazi, hasa katika mazingira ya chuo kikuu na bidii yake ya kitume hutufanya tuamini kwamba ni lazima tutambue vipaji tulivyopokea na kuviweka katika huduma ya jumuiya, kwa kujitolea, ili viweze kuongezeka kwa manufaa ya wote.”
Hatimaye, Papa Leo XIV alipenda kusisitiza upendo wake kwa maskini jambo lililompatia jina la kuwa "mwombaji wa Mungu." Papa alieleza jinsi alivyoambiwa kuwa katika Parokia yao, mantiki hiyo ipo sana, katika ishara na katika matendo ya dhati. Papa aliwashukuru kwa umakini huo kwa sababu, Maskini si mtu wa kusaidia tu lakini ni uwepo wa kisakramenti wa Bwana(Dilexi te, 44). Kwa kuhitimisha, Papa aliwatia moyo wa "kuendelea mbele kwa kufuata nyayo za Kristo, mashuhuda wa watakatifu ambao wanatutia moyo na kutuhuisha katika ari ya safari. Bwana awabariki na Mama Yetu wa Val awasindikize daima.
