Tafuta

#SistersProject

Watawa Wakatoliki waongoza katika kusimulia historia zao wenyewe

"Kwa muda mrefu watu wengine walisimulia historia za watawa kulingana na mtazamo wao.Lakini Watawa wana uzoefu wa maisha yao,wanaishi katika jamii wanazohudumia,vijijini,katika jamii za ndani ya miji,lakini pia pembezoni.”Yamo katika mahojiano na Vatican News, Sr. Jane Wakahiu,Makamu Rais wa Operesheni za Programu na Mkuu wa Mpango wa Masista Wakatoliki katika Mfuko wa Conrad N.Hilton,akishirikisha uzoefu kuhusu huduma ya Masisita Wakatoliki.

Na Sr. Francine-Marie Cooper.

Pembeni mwa Kongamano la Dunia la SIGNIS, lenye mada “Mawasiliano ya Kidijitali kwa Uwiano wa Kiutamaduni na Ustawi wa Mazingira,” lililofanyika Kigali, Rwanda, Juma la kwanza la Agosti, kuanzia tarehe 3 hadi 8, 2026, Vatican News ilizungumza na Sr. Jane Wakahiu, PhD, Makamu Rais Mshiriki wa Operesheni za Programu na Mkuu wa Watawa Wakatoliki katika Mfuko wa Conrad N. Hilton.

Sr Jane Wakahiu (wa kwanza kulia)na Watawa wakati wa Kongamano la Dunia la Signis
Sr Jane Wakahiu (wa kwanza kulia)na Watawa wakati wa Kongamano la Dunia la Signis

Katika mahojiano hayo alitafakari umuhimu wa kuimarisha “uwezo wa mawasiliano wa Masista Wakatoliki kupitia mipango inayolenga, elimu na mafunzo, na kuwawezesha kuongeza matokeo  ya kazi zao katika jamii zilizotengwa ulimwenguni kote.”

Uzoefu wa watawa mara nyingi kusimuliwa na wengine

Sr. Jane Wakahiu alisisitiza umuhimu wa watawa “kusimulia historia zao wenyewe, hasa katika enzi ya mawasiliano ya kidijitali.” Kwa vizazi vingi, “uzoefu wa watawa mara nyingi umesimuliwa na wengine,” lakini alisema kwamba “watawa wenyewe wako katika nafasi nzuri zaidi ya kuelezea kazi zao kihalisi miongoni mwa jamii za vijijini, miji ya ndani na watu wanaoishi pembezoni.”

Sr Jane Wakahiu akizungumza na Sr Francine -Marie Cooper
Sr Jane Wakahiu akizungumza na Sr Francine -Marie Cooper

Mpango wa Pentekoste

Katika kufafanua zaidi, Sr Jane, aliakisi “Mpango wa Pentekoste, unaoungwa mkono kupitia ushirikiano na Baraza la Kipapa la Mawasiliano,” kama “mfano wa jinsi ya usimulizi wa historia za kidijitali unavyoweza kukuza sauti za Watawa na jamii wanazohudumia. Kupitia historia za kila Juma zinazochapishwa kwenye Tovuti ya Habari za Vatican/Vatican News, katika lugha 10, mpango huo unatafuta kutoa sauti kwa uzoefu wa watawa kutoka sehemu, jamii na maeneo ya vita ambayo mara nyingi hayazingatiwi, wakishirikisha  historia za matumaini, furaha na ustahimilivu.”

Sehemu ya Watawa washiriki wa Kongamano la Dunia la Signis 2026 huko Kigali,Rwanda
Sehemu ya Watawa washiriki wa Kongamano la Dunia la Signis 2026 huko Kigali,Rwanda

Watawa waishi kwa kutimiza utume wa Kanisa

Sr. Jane aliziita historia hizi ni “aina ya uinjilishaji,” akiwaonesha “watawa kuwa hawako katika  makanisa tu, bali wapo pamoja na watu katika maisha yao ya kila siku, wakitumiakia kwa huruma, upendo, imani na matumaini,” huku wakiishi “kwa kutimiza utume wa Kanisa na karama za mashirika yao.” Aidha, Sr Jane aliendelea kusisitiza kwamba, “watu wa nje hawapaswi kuwaona watawa kama watu mashujaa tu, bali kama watu wanaosindikizana  na jamii, wanaozungumza lugha zao, wanaoelewa uzoefu wao na kusaidia kurejesha matumaini na maelewano ya kiutamaduni.”

Washiriki wa Kongamano la Dunia la Signis 2026,Kigali Rwanda
Washiriki wa Kongamano la Dunia la Signis 2026,Kigali Rwanda
SR JANE WAKAHIU LSOSF AKIHOJIANA NA VATICAN NEWS

Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata taarifa mpya kwa kujisajili kwenye jarida letu la kila siku. Just click here.

 

13 Agosti 2026, 11:25