Watu wa Cameroon wanatumaini ziara ya Papa italeta uponyaji katika nchi iliyogawanyika
Na Joseph Tulloch – Yaoundé na Sr. Christine Masivo, CPS
Katika kituo cha watoto yatima cha Ngul Zamba huko Yaoundé, watoto wengi walishughulikia usafi kwa furaha ya kuompokea Papa. Kulikuwa pia na bango lenye picha ya Papa Leo XIV akipunga mkono mahali hapo. Papa alitembelea kituo cha watoto Yatima, Jumatano, tarehe 15 Aprili 2026, saa chache tu baada ya kuwasili nchini Cameroon. "Watoto wengi hapa wanatoka katika malezi magumu," alielezea Sr. Christabel, ambaye anaishi katika Kituo cha watoto yatima na ni Mwalimu Mkuu wa Shule iliyo karibu na kituo hicho. Ziara ya Papa, alisema, ilikuwa wakati wa "furaha kubwa watoto watahisi kupendwa ... na kuhisi kubebwa na mamlaka ya Kanisa."
Ujumbe wa amani
Wafanyakazi wa kituo cha watoto yatima walitarajia faraja kutokana na ziara ya Papa. Nchi bado inasumbuliwa na vurugu zilizozuka baada ya uchaguzi mwishoni mwa mwaka jana. "Tunaamini ujumbe wa amani wa Baba Mtakatifu utaleta uponyaji mwingi," alisema Ngwa Colin Suh, mwandishi wa habari wa Kikatoliki wa eneo hilo. "Yeye ni mtu asiyeegemea upande wowote ... kiongozi wa kiroho badala ya mwanasiasa, na hicho ndicho tunachotarajia kukiona nchini Cameroon."
Hii ni nchi ambayo, kwa muongo mmoja sasa, imekuwa ikiteseka kutokana na migogoro kati ya pande mbili zinazozungumza Kiingereza na Kifaransa. Wengi wanaozungumza Kiingereza, katika maeneo ya kaskazini-magharibi na kusini-magharibi mwa nchi hiyo, wanahisi kubaguliwa na walio wengi wanaozungumza Kifaransa. Baadhi ya wengi wamechukua silaha katika jaribio la kuunda nchi tofauti linalozungumza Kiingereza. Bwana Suh alifikiri kwamba Papa anaweza kuzungumza na watu wa Cameroon wa asili zote. "Kila mtu"alifurahi kuhusu kuwasili kwa Papa alisema — wanaozungumza Kifaransa, Kiingereza, Waprotestanti, Wakatoliki, na Waislamu wote wanatumaini kwamba Baba Mtakatifu anaweza kuwatia moyo "kuishi pamoja, kufanya kazi pamoja, na kuelewana."
Mateso yaliyosahaulika
Sr. Claudine Boloum, ambaye hufanya kazi katika hospitali kaskazini mwa Cameroon, alichukua likizo fupi ili awepo Yaoundé kwa ziara ya Papa. "Baada ya uchaguzi, hali ya kisiasa hapa ni mbaya," alisema. "Watu wengi wanateseka, na tunafikiri kwamba hatuwezi kuendelea kuishi hivi." Mara nyingi, watu wa Cameroon huhisi wamesahaulika, Sr. Claudine alisisitiza, kana kwamba matatizo yao hayakuwa muhimu kwa ulimwengu wote. "Lakini tuliposikia Papa anakuja, ungeweza kuona furaha katika nyuso za watu. Ni kama ukumbusho kwamba sisi pia ni wanadamu."
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwenye jarida letu la kila siku. Just click here.