Watawa wa Kivietinamu wanatoa hazina ya imani na upendo kuwahudumia walioathiriwa na Ukoma
Na Sr. Christine Masivo, CPS
Mnamo 2025, Vietnam ilirekodi visa vipya 38 tu vya ukoma, ni idadi ya chini kabisa kuwahi kuripotiwa nchini. Hii inaashiria uboreshaji mkubwa ikilinganishwa na miaka ya awali. Kati ya 2012 na 2016, zaidi ya visa 1,000 viligunduliwa kote nchini.
Visa vya Ukoma Vinavyopungua Vietnam
Wataalamu wa afya wanahusisha kupungua huko na programu bora za matibabu na usimamizi bora wa visa ndani ya jamii. Leo, majimbo na miji yote nchini Vietnam inatambuliwa rasmi kama maeneo yasiyo na ukoma, huku maambukizi mapya yakionekana mara kwa mara. Licha ya maendeleo haya, takriban watu 6,000 nchini bado wanaishi na matokeo ya ugonjwa huo. Wengi waliambukizwa miaka iliyopita na tangu wakati huo wamepona kutokana na bakteria, lakini wanaendelea kuteseka kutokana na matatizo ya kudumu kama vile ulemavu na maumivu sugu.
Maisha katika Jamii Zilizotengwa
Wengi wa wagonjwa hawa hutunzwa katika vituo zaidi ya kumi kote nchini ambavyo hujulikana kama "koloni za wenye ukoma." Makazi mengi haya yalianzishwa mwanzoni mwa karne ya kuambikuzwa iliposababisha mamalaka kuwatenga wale walio na ugonjwa huo kutoka kwa idadi ya watu wa ujumla. Maeneo kama vile Quy Hoa katikati mwa Vietnam, yaliyoanzishwa mwaka wa 1929, na Bien Hoa kusini mwa Vietnam, yaliyoanzishwa mwaka wa 1968, yalijengwa katika maeneo ya mbali. Ingawa uelewa wa kimatibabu kuhusu ukoma umeimarika sana, wakazi wengi wanabaki huko kwa sababu hawana mahali pengine pa kwenda.
Maisha katika jamii hizi yanaweza kuwa magumu. Huduma za msingi ni chache, na wakazi mara nyingi husongwa na mawazo ya unyanyapaa na ubaguzi. Ukoma hauaribu mwili tu, lakini pia unaweza kuacha makovu makubwa ya kisaikolojia. Bi. Lo Thi Coc, ambaye amepona ugonjwa huo, bado anaugua matatizo ya kuona na ulemavu wa miguu unaouma. Anakumbuka kukataliwa alikopitia hapo awali. "Mimi na familia yangu tulikuwa maskini sana, na watu walituepuka kwa sababu waliogopa kuambukizwa," alikumbuka. "Wakati mmoja hata nilifikiria kutoroka kuishi peke yangu msituni. Lakini kwa msaada wa mwanangu, niliamua kuendelea."
Huruma ya masista watawa
Kwa wakazi wengi, masista katika sehemu hii wamekuwa chanzo cha matumaini na utulivu. Masista wa shirika la Wafransiskani Wamisionari huhudumu katika makoloni haya, wakiwatunza wagonjwa, wazee, na watoto walioathiriwa na ugonjwa huo. Kazi yao inaenea zaidi ya matibabu. Wanawasaidia wagonjwa na shughuli za kila siku, hutoa msaada wa kihisia, na kuunda hisia ya familia kwa watu ambao mara nyingi wameachwa. "Sina jamaa hapa," alisema Joseph That, mgonjwa wa miaka 78 katika koloni la Ben San lenye ukoma katika jimbo la Binh Duong. "Lakini watawa wakatoliki walioko hapa na mashirika tofauti hunisaidia, kwa hivyo maisha ni rahisi kidogo." Maisha ya Joseph yalibadilika sana baada ya kugundulika kuwa na ukoma. Mkewe alimwacha baada ya kujua kuhusu ugonjwa wake, na hajawahi kusikia kutoka kwake tena. Leo anatembea na miguu bandia baada ya kukatwa viungo vilivyoathiriwa na ugonjwa huo na anaishi na ulemavu mkubwa mikononi mwake. Licha ya magumu haya, huduma anayopata kutoka kwa watawa hao imemsaidia kuvumilia.
Katika kijiji cha ukoma cha Quy Hoa, mgonjwa mmoja alisema masista hao wanaheshimiwa sana na wakazi. "Wanapigania haki zetu, na tunawaona kama familia," alisema. Kwa baadhi, huruma yao imechochea mabadiliko makubwa. Mwanamume mmoja aliyefika koloni mwaka wa 1960 baadaye alibadili dini na kuwa Mkatoliki baada ya kushuhudia kujitolea kwa masista hao. Leo anasaidia kuwatunza wakazi wengine kwa kukata nywele kwa wagonjwa wazee na kuwatembelea wale wanaohisi upweke.
Usaidizi zaidi
Huduma isiyochoka ya watawa hawa imepata kutambuliwa ndani ya Kanisa na kutoka kwa serikali ya Vietnam. Sr. Anna Nguyen Thi Xuan, ambaye ametumikia katika hiki kituo kwa karibu miaka 40 akiwatunza wagonjwa katika koloni la wenye ukoma la Qua Cam huko Bac Ninh, alipewa Nishani ya Kazi ya Daraja la Tatu na Rais wa Vietnam na kupokea pongezi kutoka kwa Waziri Mkuu kwa michango yake kwa ustawi wa jamii. Wakati huo huo, jamii za Wakatoliki kote Vietnam zinaendelea kuwasaidia watu walioathiriwa na ukoma kwa kuwatembelea, kutoa michango, na uhamasishaji wa kichungaji. Wakati wa sherehe za Mwaka Mpya wa Lunar mnamo Februari 5, Jimbo la Thai Binh iliandaa mkutano na wagonjwa wa ukoma katika Kikanisa cha Dong Tho katika Parokia ya Thai Sa. Hafla hiyo ilijumuisha sherehe na utoaji wa zawadi ili kuwatia moyo wale wanaoishi na ugonjwa huo.
Katika mkutano huo, Askofu Dominic Dang Van Cau alihimiza Wakatoliki kuwakaribisha na kuwasindikiza wale walioathiriwa na ukoma kwa huruma. "Hili si tendo la huruma tu," alisema, "bali pia ni njia halisi ya kuishi fumbo la ushirika katika Kanisa." Jimbo la Thai Binh pia inajenga kituo kipya ambacho kitatoa makazi salama na thabiti kwa watu wanaougua ukoma na kuwapa sio tu makazi bali pia mahali ambapo wanaweza kuishi kwa heshima. Kupitia kujitolea kimya kimya na matendo ya kila siku ya utunzaji, watawa hawa wa Kivietinamu wanaendelea kubadilisha maisha, wakithibitisha kwamba huruma na imani vinabaki kuwa nguvu zenye nguvu hata katika pembe zilizosahaulika zaidi za jamii.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata taarifa mpya kwa kujisajili kwenye jarida letu la kila siku. Just click here.