Tafakari Dominika ya Tatu ya Kipindi Cha Kwaresima Mwaka A: Yesu Ni Kisima Cha Wokovu
Na Padre Joseph Herman Luwela, - Vatican.
UTANGULIZI: Karibu mpenzi msikilizaji na msomaji, wa tafakari ya Neno la Mungu kutoka hapa Vatican News, Katika safari yetu ya Kwaresima, Dominika ya Tatu inatuleta kisimani. Mtakatifu Exupery anasema Kisima ni chemchemi ya maisha. Mwanamke katika Injili ya leo licha ya kubahatika kukutana na wanaume wengi katika maisha yake, lakini bado aliendelea kukabiliana na ukame na kiu ya upendo wa dhati na kweli. Kumbe, imani kwa Kristo Yesu na Kanisa lake, Maisha ya Sala na Tafakari ya Neno la Mungu; Kufunga na Matendo ya huruma: kiroho na kimwili ni mambo yanayozima kiu ya dhamiri nyofu. Jangwa la maisha ya binadamu linaweza kustawi na kushamiri ikiwa kama litamwagiliwa na chemchemi ya Neno la Mungu, Sakramenti za Kanisa pamoja na matendo ya huruma: kiroho na kimwili. Kumbe, Kisimani ni mahali pa kiu, mahali pa uchovu, mahali pa kukutana na Mungu uso kwa uso. Yesu leo hakai hekaluni wala sinagogi; anakaa kando ya kisima, akisubiri mtu mwenye kiu. Hii inatuambia jambo moja muhimu: Mungu hutukuta pale tulipo, si pale tunapojifanya watakatifu. Kwaresima ipo ‘online’, maazimio ya Jumatano ya majivu je yanatekelezeka? au hali si njema? tunasali? tunafunga? Tunajinyima kwa ajili ya wahitaji? Labda tunajitahidi, Mungu atusaidie katika nia hiyo njema, au labda tunashindwa, Mungu atusaidie pia tuinuke na kujirekebisha, safari ni lazima iendelee kusudi Kristo afufuke kwenye nafsi zilizojiandaa. Neno la Mungu linatupa namna bora ya kuiishi Kwaresima, ndio kuwa na KIU YA NENO LA MUNGU.Dunia ya leo imejaa kiu nyingi: kiu cha amani katika ulimwengu unaotikiswa na vita, kiu cha haki katika jamii zilizojaa dhuluma, kiu cha upendo katika familia zinazovunjika, na zaidi ya yote, kiu cha Mungu katika mioyo iliyokauka kiroho. Ndani ya hali hii, Neno la Mungu leo linatupa jibu: Kristo ndiye maji yaliyo hai.
Katika somo la kwanza, tunawaona Wanawaisraeli jangwani. Wana kiu kali, wanaogopa kufa, wanaanza kulalamika na hata kumshuku Mungu. “Je, Bwana yuko kati yetu au la?” Maji ni muhimu… husafisha, hutupatia uzima utokao kwa Mungu, hupooza kiu, hustawisha mimea na kuleta nguvu; tunabatizwa na kutakaswa kwa maji; maji ni uhai; tukiyakosa tunakufa kwa kiu, tunanuka kwa uchafu, tunaugua magonjwa ya mlipuko, hatufui, hatupiki, na maisha huwa magumu; katika uchovu mwili huburudishwa kwa maji ya kunywa na kuoga, tulapo chakula twahitaji maji ya kunywa. Hitaji muhimu hivi linakosekana jangwani na Waisrael licha ya msaada na makubwa yote waliyotendewa na Mungu kabla bado wanamnung’unikia Mungu na Musa... Mungu bado anaonyesha upendo wake wa kibaba, anasimama mbele ya watu hawa wakali mwambani ili apigwe wao wapone… vile alivyowapenda Waisraeli bila kuhesabu makosa yao anataka nasi tuone anavyotupenda bila kuhesabu makosa yetu. Lakini Mungu hamwachi mtu wake. Anamwagiza Musa augonge mwamba, na maji yanatoka. Mwamba huo ni ishara ya Kristo, ambaye baadaye atagongwa msalabani, na kutoka kwake zitatoka maji na damu kwa wokovu wa ulimwengu. Mungu anatuonyesha leo kwamba hata pale tunapolalamika, hata pale imani inapoyumba, Yeye bado ni mwaminifu.
UFAFANUZI: Mtume Paulo katika Somo la Pili anatufungua macho kwa ukweli wa kina, “Kristo alikufa kwa ajili yetu tulipokuwa tungali wenye dhambi.” Huu ni msingi wa imani yetu. Mungu hakutusubiri tubadilike kwanza; alitupenda kwanza. Msalaba wa Kristo ni ushahidi wa upendo huu. Yesu aliyesema kisimani “nipe maji ninywe”, atasema tena akiwa msalabani: “Nina kiu.” Hii si kiu ya maji tu, bali ni kiu ya wokovu wa kila mmoja wetu. Katika dunia ya leo ambako watu wengi wanahisi hawapendwi, hawathaminiwi, au wameachwa, msalaba unasema wazi: hakuna mtu aliyesahaulika mbele ya Mungu. Kiu sharti ipozwe, inapompata mtu mwili hukosa utimamu wake. Kristo anataka tuwe na kiu ya imani; kiu hiyo hufungua chemchemi ya maji ya uzima katika Roho Mtakatifu anayetukumbusha kumwamini Mwana wa Mungu aliyeshuka duniani akiiacha enzi ya uwingu kwa ajili yetu (Filp 2:8). Sisi pia tuna kiu... ipi hiyo? ni kiu halali? Ikiwa hivyo halafu twende kwa Yesu tutapata maji ya Neno lake. La ikiwa sio kiu halali halafu hatutatosheka kamwe, tutaendelea tu kupata kiu za kidunia za udanganyi, ubinafsi, chuki, uchoyo, kutojali, tamaa, wizi... Haya yanayumbisha imani na kutufanya tusithamini kazi na mateso aliyoyapata Kristo kwa ajili yetu. Kiu ya dhambi haiwezi kwisha tusipofanya juhudi za pekee na za makusudi kuachana na dhambi hizo. Injili ya leo inatuletea simulizi ndefu lakini ya kuvutia sana. Yesu anakutana na mwanamke Msamaria mtu aliyekuwa ametengwa kijamii na kidini. Yesu anavunja mipaka yote: ya kabila, ya jinsia, na ya maadili ya jamii. Anamwambia: “Yeyote atakayekunywa maji nitakayompa hataona kiu tena.” Enzi za Yesu, kisimani palikuwa mahali pa kukutania, waliofika kuchota maji walipeana habari mpya “zinazotrendi” japokuwa wengine walisimuliwa habari za uwongo na umbeya na wakazichukua kama zilivyo na kuziweka ndoa zao matatani sababu ya maneno ya kisimani.
Pia, wachumba walikutana hapo kuzungumza mipango yao na wengine walifika kufanya biashara. Wengi walichota maji asubuhi na jioni kwa vile mchana jua liliwaka sana. Hata hivyo wapo waliofika kuchota maji mchana sababu ya dhambi zao, walitengwa na jamii na waliogopa kufika kisimani wakati watu wakiwa wengi kwa hofu ya kuchekwa, akina mama wanaelewa zaidi kinatokeaga bombani. Yesu ametumia nafasi hii kumtoa dhambini na kumjalia imani ya kweli kwa Mwokozi aliyengojewa. Mosi anamuhamisha kutoka wazo la maji ya kawaida yanayozima kiu ya mwili na kumwelewesha juu ya maji ya uzima ambayo ukiyanywa hupati kiu milele. Yesu alimwomba maji lakini mama anamwambia asimwombe kutokana na uhasama uliokuwepo kati ya Wayahudi na Wasamaria, kwa jibu lake Yesu anaonekana ‘adui.’ Kristo Yesu anamwelimisha vema hatimaye mama anabadili mwono na kumwona Yesu kwanza kama ‘Nabii’, kisha kama ‘Masiha’ na hatimaye kama ‘Mwokozi wa dunia’… ni safari ya imani inayoanza taratibu na kufikia kipeo chake hatua kwa hatua kwa mama kufunua ukweli wa maisha yake na kukiri makosa yake. Mwanamke huyu alikuwa na kiu ya ndani ambayo haikuzimwa na uhusiano mwingi wala jitihada zake. Yesu anamwonyesha kwamba kiu ya moyo wa mwanadamu ni kiu ya Mungu mwenyewe. Cha kushangaza ni kwamba mwanamke huyu anabadilika kutoka mtu anayejificha, anakuwa mshuhuda wa Injili. Anakimbia kwenda mjini na kuwaleta wengine kwa Yesu. Mtu aliyekunywa maji yaliyo hai anakuwa chemchemi kwa wengine.
Ndugu wapendwa, mwaka huu Kanisa linamuenzi Mtakatifu Francisko wa Assisi, miaka 800 baada ya kifo chake. Maisha yake ni mfano hai wa mtu aliyegundua kwamba mali, heshima na raha haviwezi kuzima kiu ya moyo. Mt. Francisko wa Assisi alipoangalia Msalaba, alielewa upendo wa Kristo mwenye kiu ya wokovu wa wanadamu. Akaacha yote, akamfuata Kristo maskini na aliyeteseka. Aliona uso wa Yesu katika maskini, wagonjwa na viumbe vyote. Katika dunia ya leo inayokumbwa na Ukame wa mazingira, Uharibifu wa uumbaji, Na ukame wa kiroho, mfano wa Mtakatifu Francisko unatualika sisi nasi kuwa walinzi wa uhai, watetezi wa maskini, na chemchemi ya matumaini. Kisima cha Yakobo kiligeuka Mimbari ambapo Habari Njema ilihubiriwa na Kristo na kumgeuza mama huyu na baadaye Wasamaria wengi wakaamini. Kisima kilijipatia hadhi mpya na kuwa mahali pa kuzungumzia mambo makuu ya Mungu na hivi kuwa mahali pa wokovu. Je, tunapokuwa kisimani tunaongea na kupanga mipango gani? Visima vya leo ndio vijiwe vya bodaboda, saluni za kike na za kiume, viwanja vya michezo, vilabu vya pombe, ofisini, dukani, shuleni...nk. Ni mazungumzo gani yanayotawala huko Visimani?
Ni kuhusu maji ya uzima yaani Neno la Mungu au ni mazungumzo na mipango mikakati mibaya? Tunajadili namna nzuri ya kupata kiu ya Mungu au tunajaribu kunywa maji yatakayotuletea kiu zaidi? mara nyingi maongezi ni juu ya wenzetu, dua zetu ni katika maanguko yao, nia zetu ni kuwadondosha na kuidanganya jamii iwaone wabaya na wadhambi kupindukia.. tukitenda hivyo tunaua mwili na kamwe hatuwezi kuiua roho; tutulie kisimani tukinywa maji ya uzima atupayo Kristo tutaishi. Kwaresima itusaidie kutambua weusi wetu na kuweka nia ya usafi kwa kitubio. Tukumbuke ahadi yetu ya ubatizo ya kumkataa shetani na kumsadiki Mungu. Dhambi zetu ni ishara kuwa tumeshindwa kuyashika tuliyoahidi. Mama Msamaria baada ya kuambiwa amlete mume wake alikiri kuwa hana, aliyemwacha nyumbani ni mume wa tano naye sio wake. Mama huyu alikubali kufunua uovu wake akapoke Yesu bado anasema leo: “Nipe maji ninywe.” Anatuomba imani yetu, mioyo yetu, na utayari wetu wa kubadilika. Tukinywa maji yaliyo hai kutoka kwa Kristo Yesu, kama yule mwanamke Msamaria na kama Mt. Fransisko wa Assisi, nasi tutakuwa vyanzo vya uzima kwa ulimwengu wenye kiu ya haki, amani, mapatano, usawa, uwajibikaji na ukweli unaoleta uhuru wa kila binadamu. Amina.