Ufilipino:Miaka arobaini baada ya “Mapinduzi ya Rozari”
Na Sr. Christine Masivo CPS – Vatican.
Miaka arobaini baada ya Mapinduzi ya kihistoria ya Nguvu ya Watu, yanayojulikana duniani kote kama “Mapinduzi ya Rozari,” Kanisa nchini Ufilipino linahimiza taifa lisiruhusu roho ya EDSA kutoweka kwenye kumbukumbu zao. Epifanio de los Santos Avenue ambayo kwa kawaida hujulikana kwa kifupi chake EDSA, ni barabara kuu inayozunguka Metro ya Manila, nchini Ufilipino na inapita katika vitengo 6 kati ya 17 vya serikali za mitaa vya Metro ya Manila, kutoka kaskazini hadi kusini,(Caloocan, Quezon City, San Juan, Mandaluyong, Makati, na Pasay).
Kwa njia hiyo EDSA ni muhimu kwa sababu ilikuwa mahali pa Mapinduzi ya Nguvu ya Watu ya 1986, ambapo mamilioni ya Wafilipino walikusanyika katika barabara hiyo kwa amani kuandamana na kurejesha demokrasia. Kulingana Shirika la Kipapa la Habari za Kimisionari Fides, Askofu Mkuu Gilbert Garcera, rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki wa Ufilipino, alizungumza wakati wa misa ya ukumbusho akisema kwamba Wafilipino sasa wanakabiliwa na aina mpya ya mapambano "uchovu wa maadili" unaozidi kupungua dhamiri na ujasiri. Mnamo Februari 1986, karibu watu milioni mbili walijaza Barabara ya Epifanio de los Santos Avenue (EDSA), wakikabiliana kwa amani na ukandamizaji na ufisadi wa utawala wa Ferdinand Marcos. Kilichotokea kuanzia Februari 22 hadi 25 kikawa sura muhimu katika historia ya taifa, uasi usio na vurugu uliotokana na sala, umoja, na hitaji lisiloyumba la kurejeshwa kwa demokrasia.
Onyo Dhidi ya "Uchovu wa Maadili"
Wakati wa misa takatifu katika Madhabahu ya Kitaifa ya Maria Malkia wa Amani, Askofu Mkuu Garcera alitafakari jinsi uhuru unavyoweza kupotea kimya kimya unapochukuliwa kama masalio ya zamani badala ya jukumu hai. "Uchovu wa maadili," alielezea, huanza wakati uhuru "unapunguzwa kuwa kumbukumbu tu," imani inakuwa "ibada bila ujasiri," na amani inafuatiliwa "bila haki." Wakati upotoshaji huu unapoanza, alionya, "roho ya EDSA inakufa polepole." Ujumbe wa Askofu Mkuu ulikuwa wa wazi akisisitiza kwamba, uhuru, amani, na imani vyote vinahitaji uwajibikaji. Ni lazima Kanisa liendelee kutumika kama sauti ya kinabii "sio ya kuridhika, si ya kimya, bali ya uaminifu." Alisisitiza ukimya mbele ya ukosefu wa haki, si utakatifu bali ni ushirikina.
Kukumbuka "Muujiza wa EDSA"
Ujumbe wa pamoja wa maaskofu kwa ajili ya maadhimisho hayo, wenye kichwa "Kumbuka maajabu ambayo Bwana ameyafanya," unakumbuka jinsi EDSA ilivyokuwa "kanisa kubwa la wazi la imani na uasi wa amani." Mamilioni walikusanyika chini ya vazi la Bikira Maria, wakisali rozari, wakisherehekea Misa, wakiimba, na kusimama bila silaha mbele ya vifaru na askari. Udikteta haukuanguka kupitia vurugu bali kupitia kile ambacho maaskofu wanakielezea kama uvumilivu wa kimya na imani ya pamoja inayolilia haki. Wanaita uasi huo "muujiza wa EDSA, “Nguvu ya Watu” si tu ushindi wa kisiasa, bali ishara ya neema ya Mungu katika magumu. Katika kuadhimisha tukio hilo, maaskofu wanatoa shukrani kwa neema iliyowezesha na kueleza majukumu matatu matakatifu kwa leo: kukumbuka, kutubu, na kujibu.
Wito wa Kuongoka Kabla ya 2028
Kukumbuka ni kuwaheshimu mashujaa wasiojulikana ambao imani yao ilithibitika kuwa na nguvu kuliko silaha. Kutubu ni kukubali kwamba zawadi ya EDSA imepotea kupitia kuridhika, ufisadi, na kutojali maskini - hali halisi inayoonyeshwa katika umaskini unaoendelea, uaminifu wa umma uliopungua, na maendeleo duni. Lakini ukumbusho na toba lazima ziongoze kwenye majibu. Maaskofu wanatoa wito wa ujasiri na upendo unaoonyeshwa kwa uaminifu, uangalifu, na uraia hai. Ukweli lazima utafutwe na kudumishwa, uongo lazima ukataliwe. Maaskofu walisistiza kwamba, mabadiliko huanza na uongofu wa kibinafsi uadilifu wa kila siku wa kutenda mema hata wakati hakuna mtu anayeangalia, na huenea hadi mageuzi ya pamoja, huku taasisi zikiacha mazoea yanayoendeleza ufisadi. Kwa uchaguzi wa 2028 ukikaribia, wanawasihi Wafilipino kuwaunga mkono viongozi waaminifu na wenye uwezo waliojitolea kwa manufaa ya wote na kuimarisha elimu kwa uraia na utawala unaowajibika. "Haya yote," ujumbe unahitimisha, "yanahitaji mapinduzi, na haswa, mapinduzi ya moyo."
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here