Papa Leo XIV:Mitandao ya kihalifu:Tubuni!machozi na damu ya kaka na dada humlilia Mungu
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV amerudia tena wito wake wa nguvu kwa ajili ya ujumuishaji wa wahamiaji akisisitiza kwamba makaribisho lazima yaendane zaidi ya usaidizi wa dharura na uwe mchakato unaorejesha heshima, umiliki na fursa. Alisema hayo wakati wa kukutana na vikundi vya Kanisa, mashirika ya upendo na mashirika ya kiraia huko Mtakatifu Cristóbal Pwani ya Tenerife siku ya Ijumaa tarehe 12 Juni 2026, ikiwa ni siku ya mwisho ya Ziara yake ya Kitume nchini Hispania iliyoanza tangu Juni 6. Baba Mtakatifu Leo XIV katika hotuba yake alielezea jukumu ambalo Visiwa vya Kanari vinaendelea kuchukua kama moja ya njia kuu za uhamiaji barani Ulaya.
Papa ashukuru kazi ya mashirika ya upendo na kiraia
Papa alishukuru kazi ya mashirika yanayowasindikiza wahamiaji baada ya kuwasili kwao kwenye visiwa hivyo na kutoa changamoto kwa jamii kusonga mbele zaidi ya hofu na kutojali. Tangu mwanzo wa hotuba yake, Papa Leo XIV alirejea maelezo aliyoyasikia kuhusu Pwani hiyo kama "mji usio na kuta." Alipendekeza kwamba picha hiyo inaashiria changamoto kubwa zaidi. Alieleza kuwa "vizuizi ambavyo ni vigumu zaidi kuvivunja si mara zote vinatengenezwa kwa mawe" na kwamba badala yake "wakati fulani vinalala katika mitazamo yetu, kwa hofu au kutojali." Visiwa vya Kanari vimekuwa mojawapo ya mipaka ya Umoja wa Ulaya yenye shughuli nyingi zaidi za uhamiaji katika miaka ya hivi karibuni. Vikiwa karibu kilomita 100 kutoka pwani ya kaskazini-magharibi mwa Afrika, visiwa vya Hispania mara nyingi ni eneo la kwanza la Ulaya kufikiwa na wahamiaji na wakimbizi wanaotoka nchi kama Senegal, Mauritania, Mali na Gambia.
Njia ya Atlantiki inachukuliwa kuwa hatari zaidi za uhamiaji
Njia ya Atlantiki inachukuliwa kuwa mojawapo ya njia hatari zaidi za uhamiaji duniani, huku maelfu wakijaribu kuvuka kila mwaka katika boti zilizojaa watu na ambazo mara nyingi hazifai baharini. Wengi hufika wakiwa wamechoka baada ya siku au juma baharini, huku wengine wengi wakiwa hawamalizi safari hiyo."Bahari inayozunguka visiwa hivi hutuletea historia ambazo hatujui kuzitafsiri kila wakati: historia za maumivu, za matumaini na za kutafuta. Tafakari ya Papa Leo XIV ilisisitiza wazo kwamba ujumuishaji unahitaji njia tofauti ya kuona. Kwa kutumia mfano wa Braille njia ya kusoma kwa nundu, na aina za mawasiliano zinazogusa, alipendekeza kwamba watu lazima wajifunze "kusoma" hata maisha ya wahamiaji kupitia ukaribu na kukutana badala ya namba au kategoria za kiutawala. "Kuna wale ambao macho yao yanaona, lakini hayatambui. Wanageuza uso kuwa namba, historia ya mtu kuwa faili na utofauti kuwa umbali." Badala yake Injili inafundisha njia ya kuona yenye mizizi katika uvumilivu, usindikizaji na mshikamano wa vitendo, Papa alisema.
Mshikamano hauwezi kupunguzwa kuwa hisani au vitendo vya ukarimu
Papa Leo XIV aliendelea kusisitiza kwamba mshikamano hauwezi kupunguzwa kuwa uhisani au vitendo vya ukarimu vya mara kwa mara, karibu hufungua mlango; ujumuishaji humsaidia mtu kuvuka kizingiti." Msaada huponya jeraha, na ujumuishaji hujenga upya mustakabali." Papa aliendelea kukataa mbinu ambazo hulazimisha wahamiaji kuacha utambulisho wao au kuhimiza jamii kuishi kando bila mwingiliano wenye maana. Badala yake, ujumuishaji, ni safari ya pande zote ambapo wageni hujifunza lugha, sheria na desturi za makazi yao mapya huku wale wanaowapokea wakijifunza kupanua upeo wao bila kupoteza utambulisho wao wenyewe. Papa kwa kutazama mmoja, mmoja wa wahamiaji hao alimtia moyo kila mtu kushiriki kikamilifu katika maisha ya jamii zao mpya na kutoa vipaji na uzoefu wao kwa manufaa ya wote.
Uhamiaji usiwe sababu ya masuala ya kisiasa au kiutawala
Papa Leo XIV pia alipinga mitazamo inayopunguza uhamiaji kuwa masuala ya kisiasa au kiutawala. Alieleza kwamba "zaidi ya yote, tunazungumzia watu walioumbwa kwa mfano na sura ya Mungu, "badala ya makundi ya kisheria au matatizo yanayopaswa kusimamiwa. Kisha alitafakari baadhi ya ushuhuda aliokuwa amesikia muda mfupi, ikiwa ni pamoja na ule wa wanaume wawili wahamiaji wanaoitwa Khalid na Mbacke. Papa alibainisha kuwa watu wengi wanaofika kwenye visiwa hivi wanatafuta sio tu usalama bali pia uwezekano wa kujenga upya maisha yao. "Wanatafuta mtu wa kuwaambia kupitia vitendo badala ya maneno: maisha yako si bure; mateso yako hayaonekani; heshima yao haijaoshwa katika maji waliyoyavuka." Wakati huo huo, hawa wanatafuta fursa za kufanya kazi, kuchangia na kushiriki, badala ya kubaki wameainishwa kabisa na udhaifu, Papa alifafanua.
"Meli ya kimya kimya"
Papa Leo XIV alizungumza kuhusu kile alichokielezea kama "meli ya kimya kimya" ambayo inaweza kutokea baada ya wahamiaji kufika salama. Huku wengi wakifa wakijaribu kuvuka bahari, wengine wanakabiliwa na kutengwa, unyonyaji na kutengwa baada ya kufika wanakokwenda. "Pia kuna meli ya kimya kimya inayotokea baada ya kufika," alionya, akielezea wale walioachwa "bila sauti, bila mahusiano, kazi au hisia ya usalama." Kwa hiyo "ujumuishaji unamaanisha kuzuia meli hiyo ya pili." Kwa sababu hiyo, alisifu kazi ya Caritas Jimbo, ofisi za uhamiaji, Parokia na Mashirika ya ndani ambayo yanawasindikiza wahamiaji zaidi ya awamu ya dharura ya haraka na kuwasaidia kuanzisha maisha thabiti ndani ya jamii.
Acheni na tubuni
Papa Leo XIV aliendelea kuelekeza wito wake kwa wale wanaofaidika na uhamiaji na mateso ya wanadamu. Akihutubia wafanyabiashara haramu wa binadamu, wanyonyaji na mitandao ya uhalifu inayohusika katika harakati na unyanyasaji wa watu walio katika mazingira magumu. "Acheni." Tubuni! Kwa kila maisha yaliyopotea, kila familia inayodanganywa, kila mwili unaotiishwa, kila mwanamke anayetishiwa, kila mfanyakazi anayenyonywa, itabidi mwende mbele ya haki ya Mungu,"alisema. Kisha aliwalaani wale wanaopanga njia hatari za uhamiaji, wanaowanyonya wafanyakazi, wanaowatishia wanawake na kufaidika kutokana na kukata tamaa, akionya kwamba "machozi na damu ya kaka na dada hawa humlilia Mungu. "Fedha zilizochukuliwa kutoka kwa udhaifu wa maskini hazitaleta amani, wala heshima, wala mustakabali," na hivyo aliwaomba wale waliohusika kuwakomboa wale wanaowanyonya, kurejesha kile kilichochukuliwa na kutafuta maridhiano kabla haijachelewa.
Ujumuishaji hauwezi kutazamwa tu kama mradi wa kijamii
Baba Mtakatifu Leo XIV aliendelea kuwakumbusha kwamba ujumuishaji hauwezi kutazamwa tu kama mradi wa kijamii. Pamoja na usaidizi wa vitendo kama vile makazi, usaidizi wa lugha, ajira na ulinzi wa kisheria, wahamiaji wanapaswa kukutana na jumuiya za Kikristo zenye uwezo wa kutoa urafiki, ushuhuda na usindikizaji. Kanisa linalokaribisha pia ni Kanisa linalotangaza," alisema, akisisitiza kwamba Injili lazima ishirikishwe "bila kuilazimisha" na kila wakati kwa heshima ya uhuru wa dhamiri. Baba Mtakatifu akihitimisha hotuba yake, alielekeza kukimbia kwa Familia Takatifu nchini Misri kama ishara ya kudumu kwa wahamiaji na wakimbizi katika historia yote. Familia Takatifu ya Nazareti," inabaki kuwa kielelezo na kimbilio kwa kila familia ya wakimbizi, kila mhamiaji na kila mtu aliyelazimishwa kuondoka katika nchi yake."
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here
