Papa Leo XIV huko Tenerife:sisi sote ni wahamiaji,mahujaji tunapoelekea mbinguni!
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Baba Mtakatifu Leo XIV akikutana Ijumaa asubuhi tarehe 12 Juni 2026, na wahusika wanaoishi kituo cha mapokezi cha Las Raíces, huko Mtakatifu Cristóbal ya Kisiwa cha manispaa ya Tenerife, kikiwa ni kituo cha mwisho katika ziara yake ya kitume nchini Hispania iliyoanza tangu tarehe 6 Juni. Kwa njia hiyo miongoni mwa mengi aliyozungumza alisema kuwa kuondoka hakumanishi kupoteza, bali kuchukua ulimwengu wa ubinadamu, ndoto, na utamaduni, na kuutoa kwa nchi ambayo, kwa kuikaribisha, hujibadilisha yenyewe. Kwa sababu uhamiaji si mtiririko wa njia moja badala yake unawatajirisha wale wanaofika na wale wanaowakaribisha. Na zaidi alisisitiza kwamba sisi sote ni wahamiaji, mahujaji tunapoelekea nchi ya mbinguni, na maana ya safari iko katika kuifanya safari hiyo kuwa ya kibinadamu zaidi kwa wote, tukitoa kile ambacho kila mtu anaweza kufikia.
Sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu
Kwa njia hiyo Papa Leo XIV alianza kusema kuwa katika Kanisa leo tunaadhimisha Sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu, ambayo kwa Wakristo inawakilisha upendo wa Mungu wenye huruma na usio na kikomo kwa kila mwanadamu. Katika muktadha huo, ni jambo la Mungu kwamba tunaweza kukutana, kuonana, na zaidi ya yote tunajua kwamba, bila kujali mahali petu pa asili, upendo wa Mungu haujui mipaka, haufanyi tofauti, hujitolea kwa wote na kutukusanya pamoja katika umoja." Papa Leo XIV alisema kuwa kwa kutazama nyuso zao na kusikiliza shuhuda zao aliwaza mioyo yao iliyojeruhiwa na matatizo mengi lakini pia Papa akafarijika na upendo unaopokelewa kutokana na mioyo mingine iliyo wazi, yenye ukarimu, na yenye huruma.
Upendo wa Mungu,hutusaidia kuponya majeraha na kuonesha upendo kwa wanaoteseka
"Moyo wa Kristo uliteseka na kuchomwa kutokana na upendo, na pia ulifarijika na watu wenye huruma waliomkaribia ili kupunguza maumivu Yake. Kuelezea utandawazi wa upendo, Yesu alichukua kama mfano kitendo cha huduma ya mtu wa watu wengine na dini ambaye alikuwa na huruma kwa mtu aliyejeruhiwa na kutendewa vibaya (taz. Lk 10:25-37).Wakisukumwa na upendo wa Mungu, ambao hutusaidia kuponya majeraha na kuonesha upendo kwa wale wanaoteseka, Papa Leo XIV aliongeza Ndugu Mtakatifu Petro na Mtakatifu Joseph de Anchieta waliondoka Visiwa hivi vya Kanari ili kutangaza Injili huko Amerika, wakifungua upeo mpya wa kimisionari. Wao pia walikuwa wahamiaji walioelekea kwenye vitu visivyojulikana, wakibeba imani, tumaini, na upendo kama mali yao kuu. Katika nchi hizo zisizojulikana, wahamiaji watakatifu na wamisionari walijua jinsi ya kutoa kile walichokuwa nacho na wakati huo huo kukaribisha vitu vipya vilivyotolewa kwao."
Sisi sote ni wahamiaji,sisi sote ni mahujaji tunaosafiri kuelekea mbinguni
Kwa hivyo, Papa Leo XIV aliwaalika pia kutoa hazina ya ubinadamu, ndoto, na utamaduni waliouleta kwenye visiwa hivyo, na kuwa wazi kupokea kile walichopewa. "Lazima tuishi kwa uwajibikaji katika kubadilishana huku, tukifikiria mustakabali wa vizazi vijavyo, ambavyo tunataka kuwapa urithi wa ustaarabu wa upendo, ambapo uhamiaji una maana muhimu, kwa sababu "unaweza kuwa fursa ya kukutana na kutajirika kati ya watu" (Magnifica Humanitas, 81). Papa Leo XIV alizidi kusema kuwa " sisi sote, kwa namna fulani ni wahamiaji, sisi sote ni mahujaji tunaosafiri kuelekea nchi yetu ya mbinguni. Hebu tusaidiane kuifanya safari hii kuwa tukio la kibinadamu zaidi kwa kila mtu, tukitoa kile kinachoweza kufikiwa na kila mtu."
Yeyote anayemtumainia Bwana ni kama mti uliopandwa kando ya maji
Kwa mantiki hiyo, Papa alitoa shukrani kwa ushirikiano wa Serikali, wa taasisi mbalimbali na wanaume na wanawake wengi wenye mapenzi mema, wanaofanikisha misaada hii madhubuti ya kibinadamu, ambayo inarejesha matumaini na utu kwa watu wengi." Papa aliongeza kusema kuwa "Nilivutiwa na jina la kituo chenu cha mapokezi, kinachoitwa "Le Radici" yaani Mizizi.
Kwa kukumbuka Mtangulizi wake Baba Mtakatifu Francisko, ambaye alitamani sana kuwa nao Papa Leo XIV alisema kuwa "alipenda kutumia taswira ya mizizi kuashiria haja ya kutosahau asili yetu, kubaki na umoja na kumtumaini Bwana." Yeye alisema kuwa "Kwa maana yeyote anayemtumainia Bwana ni kama mti uliopandwa kando ya maji, unaopeleka mizizi yake kando ya kijito; hauogopi joto litakapokuja, lakini majani yake yatabaki mabichi" (Yer 17:8)" na (Christus Vivit, 133)."
Taswira hii ya mizizi iwasaidie kubaki imara katika Bwana
Papa Leo XIV alifafanua zaidi katika muktadha huo kuwa, Taswira hii ya mizizi iwasaidie kubaki imara katika Bwana (taz. Kol 2:7), ili dhoruba yoyote isiweze kuwatenganisha na uwepo wake, unaoimarisha na kutoa uhai." Kwa kuhitimisha Papa aliwahakikishia kuwa anawabeba moyoni mwake na kuwakumbuka katika sala zake. "Mungu awabariki ninyi, familia zenu, na wote mnaowapenda. Na Mwenyeheri Bikira Maria, Faraja ya Wahamiaji, aawasindikize kila wakati na kuwasaidia kwa ulinzi wake wa kimama."
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here
