Safari inayomfunua Papa
Andrea Tornielli
Siku ya kwanza ya safari ya Papa Leo XIV barani Afrika na mbili zilizofuata ziliakisiwa, kwenye vyombo vya habari, na maoni kuhusu kauli za Rais Donald Trump. Utata ambao Papa mwenyewe alitaka kuupuuza, mbele ya hatari kwamba kila neno ambalo angesema wakati wa safari lingetafsiriwa katika muktadha wa uhusiano kati ya Vatican na Ikulu ya ‘White House.’ Hivyo ulififia nyuma, na karibu kusahaulika, msemo muhimu sana ambao Mrithi wa Petro alitamka asubuhi ya Jumatatu, Aprili 13, katika salamu yake ya kwanza kwa waandishi wa habari kwenye ndege iliyokuwa ikimpeleka Algiers: Ziara ya Afrika "ilitakiwa kuwa safari ya kwanza ya Papa. "Tayari mwaka jana, mwezi Mei, nilisema ningependa kufanya safari yangu ya kwanza barani Afrika." Kwa hivyo, mara tu alipochaguliwa, Papa Leo XIV alielezea hamu hii maalum kwa washirika wake. Hata hivyo, ombi hili halikuweza kutimizwa kwa sababu za kimkakati, lakini linazungumzia mengi kuhusu jinsi Papa wa kwanza mzaliwa wa Marekani alivyobuni utume wake. Kiukweli, hatupaswi kusahau kipengele cha msingi cha wasifu wa Robert Francis Prevost: kwamba alikuwa Padre mmisionari, sifa ya kipekee na adimu katika historia ya karne za mwisho za upapa.
Papa Leo XIV alitumia miaka mingi kama mmisionari na Paroko wa Parokia huko Peru, kisha akarudi kuhudumu kama Askofu, kwa kuteuliwa na Papa Francisko. Ni kwa kuzingatia wito huu ndipo tunaweza kuelewa hamu ya Ziara yake ya kwanza barani Afrika na kinachoendelea siku hizi, huku Papa akitabasamu na kwa utulivu anapofuatilia nyimbo zenye mdundo na ngoma za kitamaduni zinazoambatana na sherehe za Misa; anapojitolea kukutana na kuwakumbatia wadogo, anapotumia muda mwingi kushikana mikono na kusalimiana. Lakini zaidi ya yote, anapozungumzia upyaisho wa Injili, ambayo hukutana na tamaduni na watu, na kuwa nguvu inayosukuma amani na mabadiliko. Hili lilionekana huko Bamenda, Cameroon, ambapo Askofu wa Roma alikuja kuunga mkono ujenzi wa amani na kuishi pamoja katika muktadha ulioakisiwa sana na vita vya wenyewe kwa wenyewe. Au huko Yaoundé, alipohutubia ulimwengu wa Chuo Kikuu, alizungumzia umuhimu wa "kuunda dhamiri huru na takatifu zisizotulia" kama "sharti la imani ya Kikristo kuonekana kama pendekezo kamili la kibinadamu, lenye uwezo wa kubadilisha maisha ya watu binafsi na jamii, kuleta mabadiliko ya kinabii kuhusiana na mikasa na umaskini wa wakati wetu."
Sio kwa bahati mbaya kwamba Papa Leo XIV alionesha uamsho na kina cha Wosia wa kitume wa Papa Francisko, Evangelii gaudium, kama mpango wa kazi kwa ajili ya mkutano ujao. Hati hiyo ya kiprogramu ya mtangulizi wake, kumbukumbu ya kwanza ya kifo chake Aprili 21, inapendekezwa tena kwa Kanisa kwa sababu inafafanua kile ambacho utume unajumuisha: kerygma, yaani, tangazo la kiini cha imani, uso wa Kanisa linalojua jinsi ya kuwa karibu na wale wanaoteseka kwa kushiriki misiba ya wanadamu, kujitolea kubadilisha jamii kwa njia ya kibinadamu na ya haki zaidi.
Kanisa, kama tunavyosoma katika Waraka wake wa Dilexi te, linalotambua upendo kwa maskini kama sehemu muhimu ya ujumbe wa Kikristo, kwa sababu "kuwasiliana na wale wasio na nguvu na ukuu ni njia ya msingi ya kukutana na Bwana wa historia." Msisitizo wa amani, kurudi kwa mazungumzo, na kuheshimu sheria za kimataifa, uingiliaji kati ambao umesababisha matokeo katika siku za hivi karibuni, ni sehemu ya muktadha huo. Na husaidia kufafanua tena asili ya huduma ya Kanisa na hasa Mrithi wa Petro, ambaye hafanyi kama mwanasiasa bali kama mchungaji. Lakini ni asili yake kuwa mchungaji, mbali na upunguzaji wowote wa kiroho na usio na mwili, kuwa na amani ya moyoni, haki, mazungumzo, kukutana, ujenzi wa jamii zenye haki zaidi, ukaribu na wale wanaoteswa au kubaguliwa dhidi yao, ukaribu na waathiriwa wasio na hatia wa vita, unabii wa mtu anayejali hatima ya ubinadamu katika "saa hii kubwa ya historia."
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwenye jarida letu la kila siku. Just click here.
