Siku ya VI ya Babu na Wazee:Papa Leo XIV anawaalika wote wasiwasahau"
Na Angella Rwezaula, - Vatican
"Lakini sitakusahau kamwe" (Isaya 49:15) ndiyo itakuwa kauli mbiu ya Siku ya VI ya babu, bibi na Wazee, Ulimwenguni iliyoachaguliwa na Baba Mtakatifu Leo XIV itakayofanyika Dominika, tarehe 26 Julai 2026, siku ambayo Mama Kanisa anafanya kumbukizi ya babu na bibi wa Yesu, Watakatifu Joachim na Anna.
Upendo wa Mungu na familia
Kauli mbiu ya Siku, iliyochochaguliwa na Papa Leo XIV, inatoka katika kifungu cha Nabii Isaya ambayo inakumbusha jinsi upendo wa Mungu unavyoenea kwa kila mtu na haushindwi kamwe, hata katika udhaifu wa uzee. Wakati huo huo, imekusudiwa kuwa kama ukumbusho kwa familia na jumuiya za kikanisa kutowasahau babu na bibi na wazee na kutambua ndani yao uwepo wa thamani na baraka. "Baraza la Kipapa la Walei, Familia na Maisha linahimiza Makanisa, yote, vyama na jumuiya maalum za kikanisa ulimwenguni kote kutafuta njia za kutangaza Siku hiyo katika muktadha wao wa ndani na baadaye litaweka vifaa maalum vya kichungaji kwa kusudi hilo," kwa mujibu wa taarifa za vyombo vya habari kutoka Baraza hilo la Kipapa.
Misa katika kila kanisa kuu la Jimbo
Papa Leo XIV aidha anawaalika watu wote kusherehekea Siku hiyo kwa liturujia ya Misa Takatifu katika Kanisa Kuu la kila Jimbo Ulimwenguni. Mwaka 2025, siku hiyo iliadhimishwa tarehe 27 Julai 2025 na Papa Leo XIV alikuwa amewasihi "kila Parokia, kila chama, kila kundi la Kanisa" kuwa "watetezi wa 'mapinduzi' ya shukrani na utunzaji," mapinduzi "yanayopatikana kwa kuwatembelea wazee mara kwa mara," ambao, katika jamii zetu, mara nyingi hutengwa na kusahaulika. Hili ndilo hasa lilikuwa lengo la Papa Francisko alipoanzisha Siku hiyo mwaka 2021, ili iadhimishwe Dominika ya nne ya Mwezi Julai ili: "kuunda fursa ya kuleta pamoja ukaribu wa Kanisa kwa wazee na kuthamini mchango wao kwa familia na jamii nzima ya binadamu."
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata taarifa mpya kwa kujisajili kwenye jarida letu la kila siku: Just click here.
