Papa amemteua Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu la Bamenda,Camerun
Vatican News.
Baba Mtakatifu amemteua John Berinyuy Tata, ambaye kwa sasa alikuwa ni Gambera wa Chuo Kikuu Katoliki cha Camerun huko Bamenda, kuwa Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu la Bamenda (Camerun).
Wasifu wake
Askofu Mteule John Berinyuy Tata alizaliwa tarehe 18 Desemba 1975, huko Mbuluf-Shisong, katika jimbo la Kumbo. Alisoma Falsafa na Taalimungu katika Seminari Kuu ya Mtakatifu Thomas Aquinas huko Bambui (Bamenda). Alipewa daraja la upadre mnamo tarehe 30 Machi 2005.
Ameshika nafasi zifuatazo na kuendelea na masomo zaidi: Majukumu katika Parokia ya Mtakatifu Yosefu huko Bafut (2005-2006) na Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Patrick huko Babanki-Tungo (2006-2010); masomo ya Tasaufi katika Monasteri ya Wadomenikani huko Bambui; Shahada ya Uzamivu katika Taalimungu na utaalamu katika Anthropolojia ya Kikristo kutoka Kitivo cha Taalimungu cha Kipapa cha Teresianum Roma; Mkurugenzi wa Kiroho na Profesa katika Seminari Kuu ya Mtakatifu Thomas Aquinas huko Bambui; Msimamizi wa Harakati ya Karismatiki (CARIS) ya Jimbo na, hadi sasa, Gambera wa Chuo Kikuu Katoliki cha Camerun huko Bamenda.
