Papa akihojiwa  wakati akitoka  Castel Gandolfo. Papa akihojiwa wakati akitoka Castel Gandolfo. 

Papa Leo XIV:Tunaweza kupaza sauti zetu na kutafuta mazungumzo daima na sio vurugu

Kutoka Castel Gandolfo,usiku Januari 27,Papa alitoa taarifa fupi kwa waandishi wa habari nje ya Villa Barberini.Akitoa maoni yake kuhusu hali ya Mashariki ya Kati,alihimiza maombi ya amani.Akikumbuka Mauaji ya Kimbari,katika Siku ya Ukumbusho wa Mauaji ya Kimbari leo hii,alisema:"Tunapambana dhidi ya aina zote za chuki dhidi ya Wayahudi."

Na Angella Rwezaula, - Vatican

"Ninasema tu kwamba lazima tuombe sana kwa ajili ya amani." Ni jibu katika taarifa fupi ya Papa Leo XIV, iliyotolewa na Televisheni ya Italia (Tg2), usiku Jumanne tarehe 27 Januari 2026 na vyombo vingine vya habari alipokuwa akiondoka Villa Barberini, katika makazi yake huko Castel Gandolfo, mahali ambapo Papa alitumia siku yake ya kawaida ya kila Juma kupumzika na kufanya shughuli zake za kawaida.

"Sisi wadogo tunaweza kupaza sauti"

Aliulizwa swali na  waandishi wa habari kuhusu hali katika Mashariki ya Kati, hasa uwepo wa kundi la mashambulizi ya majini linaloongozwa na meli ya Marekani 'Abraham Lincoln' katika maji ya Mashariki ya Kati, ambapo Papa alirudia kutoa  wito wake wa amani kwamba: "Sisi wadogo tunaweza kupaza sauti zetu na kutafuta mazungumzo kila wakati na sio vurugu ili kutatua matatizo haya," alisema, "hasa ​​katika siku hii ya kuadhimisha siku ya Mauaji ya Kimbari."

Akikumbuka kumbukumbu hiyo, Papa Leo XIV alirudia huko Castel Gandolfo kile alichokuwa amesema mapema leo,  katika chapisho kwenye akaunti yake ya X @Pontifex kwamba: "Leo, Siku ya Ukumbusho wa Mauaji ya Kimbari, ningependa kukumbuka kwamba Kanisa linabaki aminifu kwa msimamo thabiti wa Tamko la "NostraAetate "dhidi ya aina zote za chuki, dhidi ya Wayahudi na linakataa ubaguzi au unyanyasaji wowote kwa misingi ya ukabila, lugha, utaifa au dini".

Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata taarifa mpya kwa kujisajili kwenye jarida letu la kila siku: Just click here.

27 Januari 2026, 21:22