Papa amechagua mada ya siku ya Wagonjwa 2026:"Huruma ya Msamaria"
Vatican News
Huruma ya Msamaria: kupenda kwa kubeba maumivu ya wengine ndiyo kauli mbiu iliyochaguliwa na Baba Mtakatifu Leo XIV kuongoza Siku ya Wagonjwa Duniani ijayo inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 11 Februari. Baraza la kipapa la Huduma ya Maendeleo Fungamani ya Bindamu ilitoa mada hiyo siku ya Ijumaa tarehe 26 Septemba 2025 kupitia Ofisi ya Vyombo vya Wanahabari, Vatican.
Mada hii kwa hakika inahusu sura ya Injili ya Msamaria, ambaye anaonesha upendo kwa kumjali mtu anayeteseka ambaye alikutana na wanyang'anyi. Inaakisi sehemu kuu ya upendo kwa jirani: upendo lazima udhihirishwe kupitia vitendo madhubuti vya ukaribu, kwa kuchukua mateso ya wengine na hasa wale ambao ni wagonjwa, na mara nyingi pia walio hatarini kwa sababu ya umaskini, kutengwa, au upweke. Kwa mujibu wa Baraza hilo liliandika katika taarifa iliyochapishwa kwamba "Siku ya Wagonjwa Ulimwenguni, iliyoanzishwa na Mtakatifu Yohane Paulo II mnamo 1992, inatoa wakati wa upendeleo wa sala, ukaribu wa kiroho, na tafakari kwa Kanisa zima na kwa asasi za kiraia, ambao wote wameitwa kutambua uso wa Kristo ndani ya kaka na dada zetu wagonjwa na walio hatarini.”
Kama vile Msamaria Mwema aliyeinama kumsaidia mtu aliyejeruhiwa njiani, Jumuiya ya Kikristo pia inaitwa kusimama kidete kwa ajili ya kuwasaidia wale wanaoteseka na kuwa mashuhuda wa kiinjili ya ukaribu na huduma kwa wagonjwa na walio hatarini zaidi."
