Afrika Kusini,Papa Leo XIV,IMBISA:"kazi ya taasisi yenu itawezesha ushiriki hai wa Uinjilishaji wa Kanisa"
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Shirikisho la Mabaraza sita ya Maaskofu Kusini mwa Afrika wamekuwa na Mkutano tangu tarehe 24 Septemba 2025 huko Lodge ya Esibayeni katikati mwa Ufalme wa Eswatini, ukiwa ni Mkutano Mkuu wa XIV na kusherehekea Jubilei ya Dhahabu ya IMBISA(Shirikisho la Kikanda la Maaskofu wa Kusini mwa Afrika). Hii inaadhimisha miaka 50 ya historia, changamoto, na maamuzi ya kichungaji katika miktadha ambayo si rahisi kila wakati, ambayo mara nyingi huaakisiwa na kutokuwa na dini na mivutano ya kijamii na kisiasa.
Kwa maaskofu wa Angola, Botswana, Eswatini, Lesotho, Msumbiji, Namibia, São Tomé na Príncipe, Afrika Kusini, na Zimbabwe, Papa Leo XIV anatuma baraka zake, zilizojaa "shukrani za dhati." Alifanya hivyo katika barua iliyosomwa tarehe 25 Septemba 2025, wakati wa ufunguzi wa mkutano huo, iliyotiwa saini na Mwakilishi wa Sekretarieti ya Vatacan, Askofu Mkuu Edgar Peña Parra, Katibu Msaidizi wa Vatican akimweleka Askofu Mkuu Liborius Ndumbukuti Nashenda Askofu Mkuu wa Windhoek na Rais wa IMBISA.
Katika Ujumbe huo anaandika “Baba Mtakatifu kuwa amepokea barua yako ya tarehe 7 Agosti iliyopita, iliyotumwa kwa niaba ya Maaskofu wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu wa Afrika Kusini(IMBISA), kuhusu Mkutano wa Baraza la XIV na maadhimisho ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwake.” Baba Mtakatifu “anaonesha shukrani zake za dhati kwa huduma muhimu ambayo Baraza lenu limetoa kwa jumuiya za Kikristo katika eneo hilo kwa muda wa miaka hamsini iliyopita.”
Papa “Anaamini kwamba, kazi ya taasisi hii ya kimaeneo itaendelea kuwezesha ushiriki hai wa Watu wa Mungu katika utume wa Uinjilishaji wa Kanisa. Pia anaomba kwamba, kwa kuimarishwa na vifungo vya mshikamano wa kidugu, safari yenu ya sinodi ipate lishe ya kudumu kutoka katika moyo wa huruma wa Bwana mnapofanya kazi kwa ajili ya manufaa ya Kanisa na jamii pana.”
Kwa kuhimitisha anabainisha kuwa: “Juu yenu, ndugu zenu Maaskofu, wakleri, watawa na waamini walei katika kanda ya Kusini mwa Afrika na wote waliohudhuria katika maadhimisho ya Jubilei ya Baraza lenu huko Eswatini, Baba Mtakatifu anawatumia kwa moyo mkunjufu Baraka yake ya Kitume kama dhamana ya amani na upendo kwa Bwana. KNawatakia matashi mema."
