Pad.Allan Bukenya,SCA:Maisha ya Utawa ni mwaliko wa kumtumikia Kristo kwa furaha
Na Sr. Ernestina Patrick Lasway,SAC, - Arusha,Tanzania.
Tarehe tarehe 22 Julai 2026, Mama Kanisa akiadhimisha Sikukuu ya Mtakatifu Magadalena, mwanamke wa kwanza kushuhudia ufufuko wa Bwana, na kutangaza kwa wanafunzi wengine (Yh 20:11-18), Mhusika wa Watawa katika Jimbo Kuu Arusha, Tanzania, Padre Allan Bukenya, SCA, aliwataka Watawa kujitoa na kumtumikia Kristo kwa furaha ili kuwavuta wengi kwa Kristo. Aliyasema hayo mbele ya watawa waliokuwa wakifunga nadhiri za daima kwa Shirika la Masista wa Upendo la Mtakatifu Karoli Borromeo pamoja na wengine waliomshukuru Mungu kwa Jubilei ya miaka 25 ya Utawa. Hawa walikuwa ni Sr. Clara Ghimu, Sr. Rebecca Rwelamila, pamoja na Sr. Grace Mrwati, Sr. Regina Tesha, Sr. Colletha Mushi na Sr. Gemma Kavishe.
Woga wa Kujitoa
Padre Allan akiendelea na homelia yake aliwapongeza masista wa nadhiri za daima na Jubilei kujitoa bila kujibakiza kwa Kristo. Akianisha kuwa, “wito wa kweli unatoka kwa Mungu na mwanadamu anao wajibu wa kuitika kwa upendo, na kujitoa bila woga.”
Uzuri wa Maisha ya Wakfu
Kwa nadhiri za daima, alibainisha kuwa, “Kristo huwa Bwana Harusi wa watawa hawa na kuweka agano lisilovunjika naye. Hii ni ishara ya upendo na uaminifu kwa Kristo. Kwa kuvishwa pete, watawa wanajifungamanisha na Kristo kabisa na Kristo na kumtolea vipaji vyao, karama na hata udhaifu wao.”
Mfano wa Kumfuasa Kristo.
Kama Martha na Maria katika Injiili ya Matayo 10:38-42, watawa wanaalikwa kutunza vizuri muda wa kukaa miguuni kwa Yesu, kwa sala na matendo mema. “Huduma zitolewazo na masista wa Upendo wa Mtakatifu Carol Boprromeo, zitazaa matunda tu, pale ambapo mtawa amejikita katika Kristo, alikazia Padre Allan.
Miaka 25 ya Ushuhuda
Akiwageugia masista waliomshukuru Mungu kwa Jubilei ya miaka 25 ya utawa, Padre Allan aliwapongeza masista kwa kujitoa kwa dhati kwa Kanisa. “Maisha ya utawa kwa miaka 25 ya huduma ni ushuhuda wa imani na uaminifu kwa Kristo anayemuita mtawa kumtumikia kwa upendo.”
Hatima ya maisha ya mtawa
Mmmisionari huyo pia alibainisha kuwa, lengo la mtawa ni kuishi vizuri na Kristo na kujitolea kila siku hadi kufikia zawadi ya uzima wa milele. Padre Allan alitamatisha kwa kuwatakia maisha mema katika kumtumikia Mungu kwa furaha, kama tunavyoalikwa na Hayati Papa Francisco kuwa, “Penye mtawa pana furaha,” furaha ya kumtumikia Mungu ijidhihirishe katika maisha ya kila siku ya mtawa ili kuwavuta wengi zaidi kumfuata Kristo.”
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here.