Kenya:Watawa wa Huruma huko Turkana wabadilisha hali ya maisha
Na Sr.Michelle Njeri, OSF
Huko Lokori, Tukana Kenya katika kitovu cha utume huu ni Sr. Selina Mbuli, ambaye utume wake umekuwa wa muhimu na wa msaada mkubwa sana kwa makundi yaliyo katika mazingira magumu ikiwa ni pamoja na watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi(HIV/AIDS),familia za wahamiaji, watoto walio katika mazingira magumu na walezi wao ambao ni wazee.
Huduma jumuishi huku rasilimali zikipungua
Katika Kituo cha Afya chao cha Masista wa Huruma Lokori, wagonjwa hapo awali walipata huduma kamili, ikiwa ni pamoja na huduma za kliniki zinazohamishika ambazo zilihudumia familia za wahamaji wanaohama kutafuta malisho ya mifugo wao na maji. Leo hii, mfumo huu uko chini ya shinikizo kutokana na kupunguzwa kwa ufadhili kufuatia kuondolewa kwa wafadhili wa kimataifa, ambayo imeathiri sana huduma.
"Tulikuwa tumeajiri na kuwapa ushauri timu imara ya wafanyakazi wa afya, tukiwaunda katika maadili yetu. Wengi sasa wanaondoka kutokana na kupunguzwa kwa mishahara na kutafuta fursa bora zaidi. Licha ya changamoto hizi, waamini wangu wanaendelea kuunga mkono utoaji wa huduma jumuishi kwa wagonjwa wa Virusi vya Ukimwi," alisema Sr. Mbuli.
Kupambana na Virusi vya Ukimwi
Kila mwaka, Kituo cha Afya cha Lokori huadhimisha Siku ya Virusi vya Ukimwi Duniani(iadhimishwayo ifikapo Desemba 1 ya kila mwaka) kwa kutoa dawa,(….) msaada wa chakula, na elimu ya afya. Kwa miaka michache tu iliyobaki kufikia lengo la kimataifa la 2030 la kukomesha ugonjwa wa Virusi vya Ukimwi kama tishio la afya ya umma, Sr. Mbuli alitafakari:
"Bado tunashindana dhidi ya muda. Virusi vya Ukimwi ni kitu ambacho kipo kwa hakika. Ili kushughulikia unyanyapaa na changamoto katika kupata matibabu, tumeanzisha mifumo ya usaidizi kupitia ushauri nasaha, shughuli za matibabu, na mifumo iliyorekebishwa iliyoongozwa na Walevi Wasiojulikana."
Kuwezesha jamii kupitia riziki
Zaidi ya huduma ya afya, Masista wa Shirika la Huruma wameanzisha shughuli za kuzalisha mapato ili kushughulikia umaskini, njaa, na utegemezi. "Tumeanzisha Jumuiya za akiba na mikopo (vikundi vya SILC), vyenye wanachama zaidi ya 290 katika vikundi 10 vya benki ya mezani. Pia tunawapa wanachama elimu ya msingi ya kifedha, ujuzi wa ujasiriamali, na upatikanaji wa mikopo midogo. Zaidi ya hayo, tuna Lokori Fresh Bakery, (utengenezaji wa mikate) mpango unaounda ajira kwa wakazi wa eneo hilo. Tunataka watu wachukue umiliki wa maendeleo yao na kurejesha heshima," Sr. Mbuli alisema huku akitabasamu.
Kutoka jangwa hadi kijani, Lokori Green
Wakiongozwa na Laudato Si' na kukita mizizi katika utunzaji wa watu na mazingira, watawa hao walizindua Mpango wa Lokori Green. "Tuhamaisha utunzaji bora wa mazingira na uponyaji wa kibinafsi kupitia mpango huu. Tulianza kwenye ardhi yenye miamba, tasa. Kwa pamoja, tulileta udongo, tukaendeleza shamba la mazingira, na kupanda miti. Leo hii, pia tunafuga nyuki zenye mizinga 41 ya nyuki. Tumewapa watu matumaini na kurejesha heshima yao," Sr. Mbuli aliongeza.
Kuelimisha na kulinda kwa kusaidia kizazi kijacho
Watawa hawa wamejitolea kuwaelimisha wakazi wa eneo hilo kuhusu mila za kitamaduni hatari ili kuwawezesha vijana. "tunafanya kazi na viongozi wa eneo hili na tunawasaidia wasichana kuepuka ndoa za mapema na kulazimishwa na tukishirikiana na watu wenye nia njema tunawasaidia katika masomo yao. Pia tunayo pia shule za wachungaji misituni, ambapo wavulana na wakati mwingine na wasichana wanaochunga mifugo wakati wa mchana uhudhuria masomo ya jioni. Kupitia elimu, tunawezesha jamii," alisema Sr. Mbuli.
Bwana Sylvester Lokuto, alikuwa mchungaji wa mifugo alipokuwa mvulana mdogo, sasa ni mratibu wa Mpango wa Kijani wa Lokori. "Nilipojiunga na shule ya wachungaji, masista walitambua uwezo wangu wa kitaaluma na kuniunga mkono kupitia elimu rasmi hadi chuo kikuu. Masista wa Huruma wamekuwa na athari kubwa katika maisha yangu. Nilirudi kutoa na kuinua jamii yangu," alisema. Alipoulizwa kuhusu motisha yake, aliongeza na kusema kwamba, "shauku yangu ni kuwatia moyo watu wangu. Ndoto yangu ni kuona Mpango wa Lokori Green ukiigwa katika jamii zetu ili kushughulikia mabadiliko ya hali ya hewa na kurejesha mazingira. Natumai tunaweza kuwa na kisima, kwasababu watu hapa hutembea umbali wa kilomita nyingi kupata maji."
Dhamira yenye mizizi katika huruma
Licha ya maendeleo yaliyofanywa Lokori, uhaba wa maji unabaki kuwa changamoto kubwa. "Wanawake hukaa siku nzima chini ya jua, wakipanga foleni kutafuta maji na kutembea umbali mrefu. Hii inawaweka katika hatari na kupunguza uzalishaji. Asubuhi ya leo, niliwauliza wanawake walikuwa wakiomba nini, nao wakasema, maji," alisema Sr. Mbuli, sauti yake ikiwa na wasiwasi. "Kisima kimoja kilicho karibu kingebadilisha maisha ya mamia ya familia." Kwa Sr. Mbuli, kazi hii ni zaidi ya huduma, ni wito. "Karama ya Masista wa Huruma inanitia moyo. Ninaweza kuona matokeo mazuri hapa Lokori, miti inakua, watoto wanaelimishwa, maisha yanarejeshwa. Maono yangu ni mustakabali ambapo kila mtoto apate elimu, Virusi vya Ukimwi havitakuwa, tishio tena, na jamii zinawezeshwa kujiendeleza. Inawezekana kuleta mabadiliko, tunahitaji tu kuendelea kufanya kile tuwezacho,” alihitimisha.
Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku. Just click here