Mama Yetu wa Arabia Mama Yetu wa Arabia 

Mama Yetu wa Arabia:Uwepo wa Maria katika Moyo wa Ghuba

Kila mwaka,Jumamosi au pale inaporuhusiwa kikanisa,Dominika inayofuata Siku kuu ya Ubatizo wa Bwana,Wakatoliki wote wa Ghuba ya Arabia hukusanyika kusherehekea Sherehe ya Mama Yetu wa Arabia.

Na Sr. Christine Masivo CPS – Vatican.

Siku kuu ya Ubatizo wa Bwana, inayothaminiwa sana na waamini wa Ghuba, inashuhudia ibada ya kipekee ya Maria ambayo imekua kimya kimya lakini kwa uthabiti katika eneo ambalo maisha ya Kikristo yanaishi kwa unyenyekevu na busara. Kwa mujibu wa taarifa kutoka Shirika la Kipapa la habari za Kimisionari FIDES zinabainisha kwamba, Mwaka 2026 huko Bahrain, sherehe hiyo iliongozwa na Askofu Aldo Berardi, O.S.T., Askofu Mkuu wa Arabia Kaskazini, mnamo tarehe 10 Jaunair 2026 katika Kanisa Kuu la Mama Yetu wa Arabia huko Awali. Liturujia hiyo ilitanguliwa kuondoka kwa Askofu kwenda Kuwait, ambapo baadaye alimkaribisha Kardinali Pietro Parolin, Katibu Mkuu wa Vatican, kwa ajili ya kuwekwa wakfu kwa Kanisa la Mama Yetu wa Ahmadi kama Basilika Ndogo. Askofu Berardi pia alithibitisha kwamba Sherehe hiyo itaadhimishwa katika makanisa yote ya Vikariate ikiwa ni pamoja na Bahrain, Kuwait, Qatar, na Saudi Arabia mnamo Januari 17.

Kujitolea kwa Mama Yetu

Kujitolea kwa Mama Yetu wa Arabia ni sehemu ya utamaduni mpana wa Kikatoliki wa kumheshimu Bikira Maria chini ya wadhifa wa ndani na kitaifa. Ulimwenguni kote, Maria ameitwa kama mama mwenye upendo anayesindikizana na watu kupitia historia na mapambano yao maalum. Kuanzia Mama Yetu wa Luján huko Argentina hadi Bikira wa Tsuwano huko Japan, Sifa za Mama Maria zinaelezea imani ya Jumuiya zinazotambua ukaribu wa mama wa Maria katika muktadha wao wa kiutamaduni na kiroho. Kwa uzuri na kwa kuigwa kwa Mama Yetu wa Arabia ana nafasi ya kipekee. Cheo chake hakikutokea katika Jumuiya yenyewe ya  Wakristo wengi, bali katikati ya Ghuba ya Arabia, ambapo Kanisa linaundwa kwa kiasi kikubwa na wahamiaji na wageni. Kwa mamilioni wanaoishi mbali na nchi zao, Maria amekuwa ishara ya umoja, ulinzi, na nyumba ya kiroho, mama aliyepo kila wakati akitembea na Kanisa lililo nje ya nchi.

Asilia ya Ibada ya Maria

Asili ya ibada hii ilianzia mwishoni mwa miaka ya 1940, wakati wamisionari wa Wakarmeli (waitwao Peku) kutoka Iraq walipofika Kuwait kuhudumia idadi ya Wakatoliki inayokua kwa kasi. Wakitafuta kukuza imani ya Jumuiya  mbalimbali, walichonga Sanamu ya  Maria ambayo hatimaye ingejulikana kama Mama Yetu wa Arabia. Picha hiyo iliongozwa na sanamu ya Mama Yetu wa Mlima Karmeli ya 1919 kutoka Monasteri ya Stella Maris huko Haifa. Mchoro wa picha hii ulifika Ahmadi, Kuwait, mnamo tarehe 1 Mei  1948, na ibada ya Umma  ilianza kwenye Siku kuu ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili  mwaka huo huo chini ya uongozi wa Padre Teofano Ubaldo Stella, O.C.D., Askofu wa Kwanza wa Kitume wa Kuwait.

Kadiri ibada ilivyokua, sanamu mpya iliagizwa nchini Italia mnamo 1949. Ilichongwa kutoka mwerezi wa Lebanon, ilipelekwa kwa Papa Pio XII, ambaye aliibariki mwenyewe mnamo tarehe 17 Desemba 1949, na kuwa ishara ya ajabu ambayo iliashiria sana historia ya awali ya ibada hiyo. Sanamu hiyo ilifika Kuwait mnamo  tarehe 6 Januari  1950, katika Siku Kuu ya Tokeo la Bwana(EPIFANI)  na haraka ikawa kitovu cha sala katika Madhabahu ya Ahmadi. Usaidizi wa Papa uliendelea katika miaka iliyofuata. Mnamo 1957, Papa Pio XII alimtangaza rasmi Mama Yetu wa Arabia kuwa Msimamizi Mkuu wa Kuwait na Vikariati yake ya Kitume. Muongo mmoja baadaye, mnamo 1960, sanamu hiyo ilivikwa taji za dhahabu zilizopambwa kwa mawe ya thamani na lulu za Ghuba, katika sherehe iliyoidhinishwa na Papa Mtakatifu  Yohane  XXIII.

Mama wa Arabia, Msimamizi wa Ghuba nzima ya Arabia

Katika siku za hivi karibuni, Askofu Camillo Ballin, MCCJ, alitoa msukumo mpya kwa utambulisho huu wa Maria. Chini ya uongozi wake, sanamu hiyo ilivikwa taji rasmi mnamo 2011, na Papa Benedicto XVI alimkubali Mama Yetu wa Arabia kama Mlinzi Mkuu wa Ghuba nzima ya Arabia. Askofu Ballin pia alianzisha ujenzi wa Kanisa Kuu la Mama Yetu wa Arabia huko Bahrain, lililowekwa wakfu mnamo 2021. Leo hii, chini ya uongozi wa Askofu Berardi, ibada inaendelea kushamiri. Kuinuliwa kwa Madhabahu ya Ahmadi hadi kuwa Kanisa Kuu Ndogo mwaka  2025 kunasisitiza umuhimu wa kudumu wa uwepo wa Maria katika eneo hilo. Baada ya zaidi ya miaka 75, heshima isiyokatizwa ya Mama Yetu wa Arabia inasimama kama ushuhuda wenye nguvu wa imani, ustahimilivu, na ushuhuda wa utulivu wa Kanisa Katoliki katika Ghuba ya Arabia ishara hai kwamba Mama wa Mungu anawasindikiza   watoto wake popote walipo.

Mama Yetu wa Arabia

Asante kwa kusoma makala yetu. Unaweza kuendelea kupata habari mpya kwa kujisajili kwa jarida letu la kila siku: Just click here

 

14 Januari 2026, 17:14